google-site-verification: googleabbfd1327a3af7a3.html

Badili maisha yako sasa kwa kuwa na fikra sahihi.

Kujifunza zaidi juu ya maisha na mafanikio, nakualika kwenye kundi la whats app kujifunza kwa kina. Tututumie ujumbe kwa njia ya whats app kwenda 0687449428 kupata utaratibu wa kujiunga.

Jun 28, 2020

Hivi Ndivyo Unavyoweza Kunufaika Kwa Ufugaji Wa Samaki.

No comments :
Habari yako ndugu msomaji wa mtandao huu wa DIRA YA MAFANIKIO . Leo nataka tujikite kujadili ufugaji wa samaki na jinsi ambavyo tunavyoweza kunufaika na ufugaji huu na kuweza hata kuongeza kipato chetu.
Kwanza kabisa samaki ni kitoweo kinachotumika na kupendwa sana hapa nchini na duniani kwa ujumla, zaidi ya kupendwa tu ni kitoweo chenye faida kubwa kwa mwili wa binadamu ambapo inaongeza protini ya kutosha na madini na hivyo kuwa na mchango mkubwa kwenye mlo kamili.
Kwa hiyo basi kutokana na uhitaji mkubwa wa samaki, watu wengi sasa wameamua kuanza ufugaji katika maeneo yao, na imekuwa biashara nzuri sana. Ningependa basi kuwashirikisha katika mambo ya kitaalamu yanayotakiwa kuzingatiwa katika ufugaji huu. Karibuni.
Ukitaka kuchimba bwawa la samaki lazima kwanza uchague eneo linalofaa. Katika kuchagua eneo linalofaa, kuna mambo ya kuzingatia kama ifuatavyo;
i) Eneo lenye vyanzo vya maji vya uhakika kama vijito, chemi chemi, na mifereji.
ii) Eneo lenye mwinuko wa  wastani ili kurahisisha uchimbaji na uvunaji wa samaki kwa kukausha bwawa.
iii) Eneo lisilo na miti yenye kuleta kivuli.
iv) Eneo lililo karibu na nyumbani ili iwe rahisi kuhudumia bwawa na kuzuia maadui wa samaki.
v) Eneo lenye udongo unaofaa.
Ninaposema udongo unaofaa ni ule wa mfinyanzi unaotuamisha maji, kwa mfano udongo unaotumika kufyatulia tofali au kutengenezea vyungu.
Njia mbili hutumika kujaribu kama udongo unafaa au la. Njia ya kwanza ni kuchukua udongo kwenye kiganja kilichojaa, lowanisha na maji na kisha finyanga kama tonge la ugali. Tupa juu tonge la udongo lililofinyangwa na lidake linaporudi chini au liache lianguke chini.
Kama tonge litabaki limeshikamana, kuna uwezekano kuwa udongo huo unafaa na unatuamisha maji. Kama litatawanyika inaashiria kuwa udongo huo una mchanga mwingi zaidi ya mfinyanzi hivyo hautatuamisha maji.

Njia nyingine na ya uhakika zaidi ni ile ya kuchimba shimo lenye kina cha kiuno. Jaribu udongo wa chini shimoni kama ulivyofanya kwenye jaribio la kwanza. Kama tonge litatawanyika udongo huo haufai na kama tonge litabaki limeshikamana, endelea na jaribio lingine.
Mapema asubuhi jaza maji shimoni ili kuona kama udongo utatuamisha maji. Finika shimo kwa kutumia matawi au kitu chocho ili kizuia kuvukizwa ( evaporation). Jioni jaza tena maji iwapo yatakuwa yamenywea ardhini. 
Kama asubuhi inayofuata maji mengi yatakuwa yamebaki shimoni, basi hilo ni eneo zuri la kuchimba bwawa la samaki. Udongo huo utakuwa una uwezo wa kutunza maji ya kutosha ambayo ni muhimu kwa samaki bwawani mwako.
Unaweza kuchimba bwawa lenye ukubwa wowote unaopenda. Uchimbaji wa bwawa kubwa unahitaji muda, eneo, virutubisho na vilishio vingi zaidi kuliko uchimbaji wa bwawa dogo. Hata hivyo utapata samaki wengi kutoka kwenye bwawa kubwa.
Mfano bwawa lenye upana wa mita 10 na urefu mita 10 litakupa samaki takribani 200. Bwawa lenye ukubwa wa mita 15 kwa 15 litakupa samaki kama 450 hivi.
Vitu vitakavyoamua ukubwa wa bwawa lako ni eneo ulilonalo, upatikanaji wa mbolea ya kurutubisha maji na vyakula vya kulishia samaki. Ikiwa huna mbolea na vyakula vya kutosha, ni bora kuchimba bwawa dogo.
Bwawa moja linalohudumiwa vizuri, litakupa mazao mengi zaidi ya mabwawa mengi yenye huduma mbaya. Hivyo ni vema kuwa na bwawa moja linalohudumiwa vizuri kuliko kuwa na mabwawa mengi yenye huduma duni.
Kama chanzo chako cha maji ni kijito, itabidi utengeneze sehemu ya kuingizia maji upande wenye kina kifupi. Maji yanapaswa kuwa safi kabla ya kuingia bwawani. Njia rahisi kuhakikisha kuwa maji yanayoingia bwawani ni safi ni kuchimba shimo dogo nje ya bwawa kwenye mfereji wa kuingizia maji. Maji yataingia kwenye shimo dogo na kutulia kabla ya kuingia bwawani. Kama kijito hicho chenye chanzo chako cha maji kina samaki, zuia samaki kutoka kwenye mtoni wasiingie bwawani kwa kuweka wavu kwenye mfereji. Weka wavu nje kidogo ya bwawa kabla maji hayajaingia bwawani.
Kumbuka kuwa Bwawa la samaki lina sehemu mbili kwa ndani, sehemu yenye kina kirefu na sehemu yenye kina kifupi.
Itabidi pia ujenge sehemu ya kutunzia mbolea kwa kutumia mianzi au miti kwenye moja ya kona upande wenye kina kirefu. Sehemu ya kutunzia mbolea inatakiwa iwe na ukubwa wa asilimia 20 ya ukubwa wa bwawa lote.
Sehemu ya kutunzia mbolea itahifadhi mbolea ambayo utaweka kwa ajili ya kurutubisha maji ya bwawa. Mbolea hii inatengeneza chakula cha asili cha samaki.
Ukimaliza kuchimba bwawa, panda nyasi juu ya tuta kuzuia mmomonyoko wa udongo inaoweza kuletwa na mvua. Baada ya yote hayo bwawa lako liko tayari kujazwa maji, kurutubishwa kwa mbolea na hatimaye kupandikizwa vifaranga vya samaki.
Katika makala ijayo Utapata maelezo zaidi ya jinsi utakavyoweza kuwalisha samaki wako. 
Endelea kufuatilia.
MAKALA HII IMEANDIKWA NA MTAALAMU WA KILIMO MARCODENIS MISUNGWI.
MAWASILIANO:-
0768 470 808


No comments :

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.