google-site-verification: googleabbfd1327a3af7a3.html

Badili maisha yako sasa kwa kuwa na fikra sahihi.

Kujifunza zaidi juu ya maisha na mafanikio, nakualika kwenye kundi la whats app kujifunza kwa kina. Tututumie ujumbe kwa njia ya whats app kwenda 0687449428 kupata utaratibu wa kujiunga.

May 23, 2016

Mambo Ya Msingi Kuhusu Mafanikio Unayotakiwa Kuyajua.

No comments :
Ili uweze kufanikiwa kwa jambo lolote, ni lazima uwe na msingi imara wa jambo hilo kwanza. Pasipo kuwa na misingi imara utasumbuka sana katika kufikia mafanikio kwa kile unachokifanya. Lakini hiyo haitoshi unatakiwa pia kulielewa kwa mapana zaidi jambo unalolifanya ili likufanikishe. Hata kwenye maisha yako binafsi, huwezi kufanikiwa kama hujui mafanikio ni nini kwako au yanataka nini.
Wengi kwa sababu ya kutokujua hili hujikuta wakisaka mafanikio kwa muda mrefu na kuambulia patupu. Kama unataka kufanikiwa kweli, kuanzia leo anza safari yako ya mafanikio kwa kuyapata mtazamo chanya wa kitofauti. Ni lazima ujue mambo ya msingi yanayohusu mafanikio ili uweze kufaniwa na kuwa mtu wa tofauti. Acha kun’gang’ania kukaa kwenye umaskini, toka hapo na uufuate utajiri.
Karibu sana na twende pamoja kujifunza mambo ya msingi yanayohusu mafanikio.
Mafanikio ni hatua.
Hakuna ambaye amewahi kulala na kuamka asubuhi akiwa tajiri. Hakuna ambaye aliyeweka juhudi kubwa kwa muda mfupi halafu akawa tajiri. Hakuna mafanikio ambayo yanapatikana kwa muda mfupi. mafanikio yote unayoyajua wewe yanatengenezwa kwa hatua. Ndio, mafanikio ni matokeo ya kupiga hatua kwa hatua kila siku.
Usitishike na kuona mafanikio makubwa ya watu ukafikiri walianzia hapo walipo. Kama unawaza hivyo, unajidanganya. Mafanikio yao yalijengwa kidogo kidogo, siku kwa siku na hata miaka. Ikiwa unataka kufika huko waliko acha kukurupuka. Jipange na anza kuelekea kwenye mafanikio yako hatua kwa hatua. Baada ya miaka michache utakuwa mbali sana.

Mafanikio ni hatua kwa hatua, usikate tamaa.
Mafanikio ni kujitoa.
Siku zote mafanikio ni kujitoa tena kwa moyo wote. Hakuna mafanikio ambayo unaweza ukayapata kama haupo tayari kujitoa. Iwe unataka au hutaki ni lazima ujitoe na kukubali kupoteza baadhi ya vitu ili uweze kufanikiwa. Upo wakati ambapo ni lazima utapoteza marafiki, muda wako, pesa kwa ajili ya mafanikio.
Yanapotokea hayo yote usijali sana, kwani kumbuka kama nilivyosema mafanikio yanahitaji kujitoa. Kwa wale rafiki zangu ambao wanataka mafanikio lakini wakati huo huo hawako tayari kupoteza baadhi ya vitu ili kufanikiwa, huwa  sio rahisi kwao kufanikiwa. Ili kufanikiwa unahitaji kujitoa mhanga kwa mambo mengi sana ikiwemo pamoja na kuwa mgumu kwenye mambo yako. Bila kujitoa kikamilifu mafanikio utayasikia kwa wengine.

Soma; Tabia Zinazoua Ndoto Na Mafanikio Ya Wengi.
Mafanikio ni uchaguzi.
Kila siku katika maisha yetu huwa tuna chaguzi nyingi ambazo tunazifanya. Kwa mfano huwa ni watu wa kuchagua chakula tunachokula. Huwa ni watu wa kuchagua mavazi, njia na mambo chungu nzima yanayofanana na hayo. Halikadhalika, na mafanikio unayoyatafuta nayo ni uchaguzi. Ni lazima uchague kufanikiwa ili ufanikiwe bila kufanya hivyo, hutafanikiwa.
Kwa bahati mbaya wengi huwa hatuna uchaguzi na maisha ya kimafanikio tunayoyataka. Kwa mfano nikuulize wewe, umeshawahi kujiuliza unataka kufanikiwa kwa viwango vipi? Usitoe macho tu, ulishawahi kujiuliza hivyo? Kama huwa unajiambia nataka tu kufanikiwa, lakini hujui kwa viwango vipi ni sawa na kama hujafanya uchaguzi kabisa. Fanya uchaguzi sahihi wa kufanikiwa kwako na ujue unataka kufika wapi na kwa muda upi?
Mafanikio ni kuona fursa.
Ili ufanikiwe ni lazima utumie kila aina ya fursa inayokuja mikononi mwako vizuri. Lakini hiyo haitoshi, kama huna uwezo wa kuona fursa za kukusaidia kufanikiwa pia hutaweza kufanikiwa. Ni muhimu sana kuzijua fursa ambazo unatakiwa uzitumie ili kufanikiwa. Bila kufanya hivyo utahangaika sana kutafuta mafanikio bila kuambulia kitu.
Watu wanaopata mafanikio mazuri kwenye maisha yao, siku zote wanatumia fursa. Ni jambo ambalo kwa sasa unatakiwa kulijua na kulizingatia vizuri sana kichwani mwako kwamba mafanikio pia huwa yanakuja kwa kuona na kutumia  fursa vizuri. Ikiwa utakuwa unaona na kutumia fursa vizuri kila wakati, uwe na uhakika hakuna wa kukuzuia kufanikiwa.

Soma; Mambo 7 Ya Kujifunza Kutoka Kwa Bilionea Bill Gates.
Mafanikio ni kutatua matatizo.
Katika safari ya mafanikio wakati mwingine inakuwa ni safari yenye kila aina ya vizuizi. Na wakati mwingine kutokana na vizuizi hivi hutufanya tuumie na hata kulia. Sasa ili uweze kufanikiwa unapaswa kutambua pia mafanikio wakati mwingine ni ule uwezo wa kutatua matatizo. Kwa kadri unavyotatua matatizo ndivyo ambavyo unajikuta unazidi kufanikiwa.
Kama unafikiri natania mafanikio sio kutatua fursa, kuanzia leo anza kutatatua matatizo yaliyo katika kijiji chako au eneo unaloishi. Kwa kutatua matatizo hayo utajikuta ukijipatia pesa kwa wingi sana. Hiyo yote inadhihirisha kwamba mafanikio ni kutatua matatizo. Jifunze juu ya hili na tatua matatizo muhimu kwenye jamii na hakika utafanikiwa.
Mafanikio ni kufanya kazi kwa bidii.
Hakuna ubishi wowote ili uweze kufanikiwa ni lazima ufanye kazi kwa bidii. Kama ulikuwa huna mtazamo huu mwanzoni unalazimika kuwa nao na kujua kwamba mafanikio ni kufanya kazi kwa bidii zote. Hakuna lelemama katika kutafuta mafanikio. Unatakiwa kujituma sana tena sana kila siku ili ufanikiwe. Vinginevyo usipozingatia hili hutaweza kufanikiwa.
Kwa kuhitimisha makala hii, nifupishe kwa kusema mafanikio ni hatua, mafanikio ni kujitoa, mafanikio ni uchaguzi, mafanikio ni fursa, mafanikio ni kutatua matatizo ya jamii na mafanikio pia ni kufanya kazi kwa bidii. Kwa kujua mambo haya yatakusaidia sana kujiwekea mtazamo tofauti juu ya mafanikio ambao utakupa msukumo mkubwa wa kuweza kusonga mbele na kufanikiwa.
Ansante kwa kuwa nami na endelea kujifunza kupitia DIRA YA MAFANIKIO kila siku.
DAIMA TUPO PAMOJA MPAKA MAISHA YAKO YAIMARIKE,
Ni wako rafiki,
Imani Ngwangwalu,
Simu; 0713 04 80 35,

No comments :

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.