google-site-verification: googleabbfd1327a3af7a3.html

Badili maisha yako sasa kwa kuwa na fikra sahihi.

Kujifunza zaidi juu ya maisha na mafanikio, nakualika kwenye kundi la whats app kujifunza kwa kina. Tututumie ujumbe kwa njia ya whats app kwenda 0687449428 kupata utaratibu wa kujiunga.

Jun 16, 2015

Kama Utaujua Ukweli Huu…Hakuna Maisha Yatakayokushinda.

No comments :
Kuna wakati huwa tunajikuta ni watu wa kushindwa katika maisha yetu siyo tu kwa sababu hatuna dira, mipango, malengo ama mwelekeo sahihi, hapana. Kuna wakati huwa tunashindwa katika maisha yetu kutokana na kujidanganya sana na kushindwa kuujua ukweli halisi tunaotakiwa kuufuata ili kufanikiwa. Mara nyingi huwa tunayachukulia maisha yetu kwa juu juu sana kama mchezo fulani hivi.

Kwa kuyachukulia maisha yetu hivyo, wengi hujikuta ni watu wa kushindwa kufika katika kilele cha mafanikio. Tumekuwa ni watu wa kushindwa kujua ukweli ambao unaweza kutupitisha katika nyakati ngumu katika maisha. Kwa kadri tunavyoujua ukweli huu ndivyo tunavyojikuta tunamudu na kuyatawala maisha yetu. Na tukiujua ukweli huu kuhusu maisha yetu, hakuna kitu ama maisha yatakayotushinda ni lazima tufanikiwe.

1. Maumivu ni sehemu ya maisha.
Mara nyingi huwa tunajikuta ni watu wa kuumizwa na hili ama lile katika maisha yetu. Ni maumivu hayohayo ambayo huweza kutufanya tuyaone maisha hayafai au hayana maana kabisa. Lakini hiyo haitoshi, maumivu haya wakati mwinginehutufanya tuanze kujiona tumekata tamaa kabisa na kusahau kuwa maumivu ni sehemu ya maisha.

Huu ndiyo ukweli muhimu kwako unaotakiwa kuujua kuhusu maisha yako, kuwa maumivu ni sehemu ya maisha. Unapoujua ukweli huu unakusaidia sana kuweza kukua na kuyaona maisha kwa upana wake. Hiyo haitakufanya ulalamike wala kulaumu bali itakusaidia kujua kumbe kuumizwa ni sehemu ya maisha hivyo wakati mwingine ni lazima kuweza kuvumilia bila kuchoka.



2. Jipe muda zaidi kufikia malengo yako makubwa.
Inawezekana ni kweli unataka kufikia ndoto zako kwa haraka zaidi, hilo ni sawa lakini jipe muda. Pasipo kujipa muda wa mafanikio unayoyataka utakuwa unajidanganya wewe. Jiwekee mikakati na kisha anza kuitekeleza kidogokidogo na ni lazima utaweza kuifanikisha bila shida.

Watu wengi huwa ni watu wa kutaka mafanikio ya haraka zaidi na kusahau kuwa hakuna mafanikio ya haraka na ya mkato. Kama utaendelea kutafuta mafaniko ya haraka katika maisha yako basi elewa hutafanikiwa kwa viwango vya juu sana, zaidi. Tambua tu kuwa chochote ujachokifanya hata kikiwa kidogo vipi kina maana kubwa sana kwako.


3. Kile unachokiogopa sana hakiwezi kukutokea.
Wakati mambo yetu yanapokuwa magumu katika maisha mara nyingi huwa siyo rahisi kufuata kile ambacho moyo unataka tukifanye zaidi huwa tunaisikiliza sana hofu. Hofu ambayo huwa imetutawala ndiyo fikra zetu hutaka kuiamini zaidi na kujua huwa ndiyo ukweli ulipo huko, kumbe inawezekana hata kile tunacho kihofia kisitokee.

Na kile tunachokiogopa sana wakati mwingine huwa ni sawa na sisi wenyewe kuogopa vivuli vyetu wenyewe. Huwa tunashindwa kusonga mbele kwa kuogopa hofu ambazo hazipo. Hiki ndicho kitu kinachoua ndoto za wengi sana kuliko kitu chochote kile hapa duniani. Ukija kuangalia maisha ya wengi yameharibwa kutokana na hizi hofu. Huu ndiyo ukweli unaotakiwa kuujua ili kufanikiwa zaidi kuwa, hofu nyingi unazoziogopa huwa hazitokei kama unavyozifikiria.


4. Usiruhusu watu wengine wakupangie maisha yako.

Ili kuweza kufanikiwa katika maisha yako, moja ya kitu ambacho unatakiwa kukisimamia wewe mwenyewe ni kuhakikisha hakuna mtu anayekupangia maisha yako. Unatakiwa ukae na kutambua kuwa hayo ni maisha yako, hivyo ni muhimu sana kusikiliza moyo wako zaidi kuliko watu wa nje ambao wanaweza kukuharibia maisha.

Kwa kufuata ukweli huu elewa hakuna mtu ama kitu kitachoweza kukuzuia kufanikiwa.  Unajua hii ni kwa nini? Hiyo yote itakuwa ni kwa sababu utakuwa unafanya kile ambacho moyo wako unakutuma na si vinginevyo. Kwa kufanya kile ambacho kipo ndani ya mapenzi ya moyo wako itakuwa ni rahisi sana kwako kufanikiwa kuliko unavyofikiri.


5.  Unahitaji msaada, hauko peke yako.
Katika safari ya mafanikio unahitaji msaada wa watu wengine li kuweza kufika kule unakotaka kufika. Haiwezekani ukawa wewe kama wewe, msaada wa wengine katika mafanikio yako ni muhimu sana kuliko unavyofikiria. Acha kuwa na fikra za kuamini kuwa wewe ni jeshi kamili la mtu mmoja hutafika mbali sana, utaishia kuwa mtu wa kawaida sana.

Ili uweze kufanikiwa unahitaji msaada wa wengie uwe wa ushauri au hata mawazo ni muhimu sana kwako. Hiyo itakusaidia wewe kuweza kubioresha mbinu mbalimbali za kimaisha na kukuwezesha kufika mbali kimafanikio. Hivyo huu ni ukweli muhimu kwako pia kuujua utakaokusaidia kufika mbali kimafanikio.

Tunakutakia kila la kheri katika safari yako ya mafanikio, endelea kutembelea mtandao huu wa DIRA YAMAFANIKIO kwa elimu na maarifa bora yatakayoboresha maisha yako. Na pia endelea kuwashirikisha wengine kujifunza mambo mazuri yanayoendelea hapa.

DAIMA TUPO PAMOJA MPAKA MAISHA YAKO YAIMARIKE,

IMANI NGWANGWALU,
0713 048035,

No comments :

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.