google-site-verification: googleabbfd1327a3af7a3.html

Badili maisha yako sasa kwa kuwa na fikra sahihi.

Kujifunza zaidi juu ya maisha na mafanikio, nakualika kwenye kundi la whats app kujifunza kwa kina. Tututumie ujumbe kwa njia ya whats app kwenda 0687449428 kupata utaratibu wa kujiunga.

May 16, 2015

Huu Ndio Msingi Halisi Wa Mafanikio Unayoyatafuta.

No comments :
Inaonekana tulio wengi tunadhani kwamba, watu wanaopata utajiri, ni wale ambao wanatengeneza fedha nyingi kwa mpigo au wale ambao wamerithi fedha kibao. Kuna ukweli ambao wengi hatuujui kuhusu jambo hili. Kwa kuangalia idadi ya watu ambao wametajirika kwa njia halali, tunaona wazi kwamba, wengi wamefikia hali hiyo kutokana na kuweka akiba kwa muda mrefu sana.

Mtaalamu mmoja wa uchumi wa marekani, Ric Edelman, katika kitabu chake cha Ordinary people, Extraordinary Wealth anaonyesha kile kinachofanya watu matajiri kuendelea kuwa matajiri. Anasema kitu hiki ni kule kuendelea kwa watu hao kufanya mambo yaliyowafanya kuwa matajiri. Kinachowafanya watu maskini nao kuendelea kuwa maskini ni kuendelea kufanya yale yaliyowafanya kuwa maskini.

Huu ni ukweli mtupu, hasa kama mtu hataangalia jambo hili kwa jicho la siasa. Kwenye siasa tunaambiwa umaskini wetu ni matokeo ya wengine kupura raslimali, kujilimbikizia na kutokujali. Huenda kuna ukweli, lakini mimi siyo mwanasiasa, hivyo sina vigezo vya kuunga mkono au kukanusha nadharia hizo.

Ric Edelman anasema , umaskini ni dhana ya kwenye mawazo wakati kuishiwa ndiyo dhana ya mfukoni. Unaweza kukabiliana na kuishiwa lakini ni vigumu kukabiliana na umaskini. Kukabiliana na kuishiwa kunafanyika kwa njia moja tu, ya kufanya kazi kwa bidii, kuweka akiba, kuweka tena akiba na tena na tena kwa muda mrefu. Baada ya kufanya hivyo, itakuwa ni vigumu sana kwako kuweza kuishiwa.


Lakini umaskini haukabiliki kwa hivyo, kwani uko kwenye mawazo yako, ni hadi ukubali kutoka humo. Mtu ambaye ana mawazo ya kimaskini hawezi kamwe kuweka akiba, kila anachopata, kiwe kidogo au kikubwa, hukitumia chote. Anategemea kwamba, kuna siku itazuka kutoka pasipo kujulikana bahati ya kupata fedha nyingi kwa mkupuo, ambapo atakuwa tajiri mkubwa.

 
Kwa watanzania tulio wengi, hayo ndiyo maradhi yetu, kuweka akiba kwa ajili ya kupata utajiri ni jambo linaloonekana vituko mawazoni mwetu.  Hata wale waliofanikiwa wengi wao hawakuanza kuwekeza kwa mamilioni ya fedha, bali fedha kidogo , wakawekeza tena mahali pengine na kupata kidogo na baada ya miaka kumi hadi ishirini wakawa wamefanikiwa.

Hapa kwetu ukimwambia mtu aweke akiba katika kile kidogo anachokipata ili baada ya miaka kumi au ishirini awekeze mahali, atakutazama kuanzia juu hadi chini. Tumelelewa katika mfumo wa kutaka leoleo, hatukujengewa msingi wa kujenga dhana thabiti ya kutunza kidogo na kuwa na subira. Tunataka tupate hapohapo na kwa wingi. 

Tumezoeshwa kuishi kwa njia za mkato sana tangu  tukiwa watoto nyumbani, shuleni na ukubwani. Tunachofikiria ni nafsi ya kuiba, kupata rushwa nzito au kudhulumu wengine ili tuwe matajiri kwa haraka sana.

Mtu ambaye anakushangaa ukimwambia aweke akiba kidogokidogo ili baada ya miaka ishirini aje awekeze na kuanza kuvuna, ukija kukutana naye baada ya hiyo miaka ishirini, utamhurumia. Hali yake itakuwa ni mbaya zaidi kuliko ilivyokuwa hiyo miaka ishirini nyuma.


Kama utaweza kumkumbusha, atajuta kwamba kama angejua angekusikia. Watu wa namna hii kazi yao ni kusema, ‘fulani tulikuwa naye juzijuzi hapa hapa, analala chumba kimoja, lakini hivi sasa mambo yake mazuri sana.’ Miaka ishirini kwake ni juzijuzi, lakini alishindwa kuutumia muda huo kwake kwa kuuona ni milele.

Kuna wakati niliwahi kukutana na kijana mmoja mfanyabiashara ya mikononi. Aliweza kunishawishi sana hadi nikanunua kisagio(blender) alichokuwa akiuza. Nilivutiwa sana na uwezo wake wa kushawishi. Nilimuuliza malengo yake ni nini hasa maishani? Alisema anatamani sana kuja kuwa na duka kubwa la jumla.

Niliendelea kumuuliza tena anachukua hatua zipi kuweza kufikia lengo lake na anatarajia ni baada ya muda gani atakuwa amefanikiwa, alisema, ‘sijaanza bado, nikipata fedha nyingi nitafungua, mwaka wowote mambo yakiwa safi, basi nitafungua duka’.

Nilimhurumia sana lakini pia niliwahurumia watanzania wenzangu wengi ambao naamini tunaishi kwa mkabala huo. Nilimwambia kwamba, ni vizuri akawa na juhudi za makusudi za kuanza kuelekea kwenye lengo lake na ni vizuri akajiwekea muda ambapo anaamini atakuwa amefikia lengo lake.


Hebu fikiria kama wewe ndo ungekuwa huyu kijana ama  unafanya biashara za mkononi, jiulize mwenyewe, una malengo gani, kutembea kutwa-kuchwa kwa miaka mingapi? Lazima ulenge jambo, hata kama jambo hilo ni la kufanya biashara ya mkononi maisha yako yote, basi uwe umelenga na kuamua, siyo ufanye tu kwa sababu inabidi ufanye.

Namkubuka  mwalimu wangu mmoja aliyenifundisha kipindi cha nyuma wakati nikiwa shule ya msingi. Mwalimu huyu alikuwa akiandika kila kitu ambachoangetarajia kukinunua kwa mwezi husika kabla ya mshahara. Nakumbuka tulikuwa tukicheka sana tulipokuwa tukiziona karatasi zake za bajeti( tulikuwa tunapata nafasi hiyo kwani tuliweza kuingia kwake tutakavyo, akiwa ni rafiki wa familia yetu) . tulicheka kwa sababu tuliona ni kichekesho mtu kuandika hata penseli ambayo atainunua na kuitumia mwezi ujayo.

Lakini nakumbuka pia nikiwa kidato cha tano niliweza kuambiwa kuwa mwalimu yule kwa sasa amejenga nyumba kubwa na ya kisasa kwao. Nilifurahi sana na kujifunza kwamba kuweka akiba ni msingi halisi wa njia ya kuelekea kwenye kipato bila kujali unapato la kiwango gani. Mwalimu wangu huyu aliweza kujenga kwa mshahara wa ualimu wa shule ya msingi bila mkopo wa benki au taasisi yoyote ya fedha. Pamoja na kuwa ilichukua zaidi ya miaka kumi, lakini lengo lake lilifikiwa.

Kuna walioko kwenye ualimu kwa miaka thelathini ambao hawana viwanja, tena vijijini na pengine wansingizia udogo wa mishahara wanayopata. Inawezekana, ikawa ni kweli kabisa mishahara hairidhishi. Lakini kabla hatujakimbilia kwenye mishahara, tumewahi kujiuliza kuhusu matumizi yetu na juhudi zetu katika kutaka kufanikiwa?

Mwalimu wangu yule hatajwi tu kwa kuweka akiba, bali hata kwa kuamua kujifunza zaidi ili apande na pato litune kidogo. Je, sisi tumefanya hivyo au tunatafuta ‘mchawi’ tu? Tusione aibu. Hata kama tuko karibu na kustaafu, tukijiuliza kuhusu malengo yetu na kuyabaini, tukaanza leo kuyafuata, tutamudu kufanikiwa. Kumbuka kufanikiwa ni hatua isiyo na kikomo, siyo kituo. 


Wengi mara tunatafuta visingizio ni kwa nini inakuwa vigumu kwetu kuweka akiba. Tutasema matatizo ya kifamilia, tutasema kulikuwa na mgonjwa, tutasema hatuna kipato cha kutosha, tutasema mabadiliko ya kipato na mengine mengi tu. Lakini ukweli unabaki palepale kwamba, kama tumeamua kuweka akiba, tutaweka tu, bila kujali ni matukio yanatokea kwenye maisha yetu. 

Kama tunaweza kuvaa, kupata chakula, kulipa kodi ya nyumba na kumudu matumizi mengine , hata kama ni kwa shida sana, tunaweza pia kuweka akiba kwa shida sana hivyohivyo, tukiamini kwamba ni jambo muhimu kabisa. Lakini huwa tunashindwa kwa sababu akiba tunaichukulia kama siyo kitu cha lazima sana katika maisha yetu. Kumbe kitu pengine ambacho hujui, kuweka akiba huu ndio msingi wa mafanikio halisi unayoyatafuta.

Kwa kuthibitisha hili kuna akina mama hapa nchini ambao wamefungua biashara, kujenga nyumba kubwa, kusomesha watoto na kufanya mengine ya maana kutokana na kuweka akiba kwenye michezo yao inayofahamika kama ‘upatu’. Wameweza kufanya hivyo, kwa sababu akiba hii ni ya lazima, ukishaingia itabidi ujinyime hata kula ili uweke, vinginevyo upate matatizo hasa. Ukichukulia suala la akiba kama ni lazima, utamudu kuweka akiba na kufanikiwa.

Nijuavyo mimi ni kwamba, usingizie au usisingizie, bado kuweka akiba kutabaki kuwa muhimu sana katika maisha yako. Ni wewe ambaye unatakiwa kuamua kuhusu hatma yako kimapato. Bila kujali una kiasi gani cha kimapato au umri gani, naamini ili mradi unapata chochote katika kutafuta kwako, unaweza kuweka akiba. Unachohitaji sio mamilioni, bali uwezo wa kumudu kuwekeza kidogo mahali ili uzalishe na kupata nguvu ya kuweza tena kuzalisha mahali pengine au kuongeza pale ulipowekeza kidogo.

Usidanganywe hata kidogo, bila kuweka akiba ni kazi bure. Kuna watu ambao kazi yao ni kusema tu, fulani kapata kwa sababu ya magendo au rushwa, kwa sababu hawajui ukweli. Mahali pasipo na uwekaji wa akiba hakuna mavuno. Akiba ndio msingi pekee wa mafanikio yako hata kama unaanzia chini kabisa.

Tunakutakia kila la kheri katika safari yako ya mafanikio, endelea kuwashirikisha wengine kutembelea mtandao huu wa DIRA YA MAFANIKIO kwa kujifunza zaidi.

DAIMA TUPO PAMOJA MPAKA MAISHA YAKO YAIMARIKE,

IMANI NGWANGWALU,
0713 048035,

No comments :

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.