google-site-verification: googleabbfd1327a3af7a3.html

DIRA YA MAFANIKIO

Badili maisha yako sasa kwa kuwa na fikra sahihi.

Kujifunza zaidi juu ya maisha na mafanikio, nakualika kwenye kundi la whats app kujifunza kwa kina. Tututumie ujumbe kwa njia ya whats app kwenda 0687449428 kupata utaratibu wa kujiunga.

Dec 23, 2014

Linalokuhuzunisha Si Tatizo Kubwa Sana, Unajitesa Bure.

No comments :
Nafahamu kwamba katika maisha ya kila siku hayakosekani mambo ya kuumiza. Sina shaka kuugua, kufiwa, kukosa chakula, kusalitiwa katika mapenzi, kudhurumiwa, kufilisika, kutotimiza malengo tuliyojiwekea na pengine kufutwa kazi ni mambo ambayo huzaa huzuni na machozi miongoni mwa watu wengi. Lakini jambo la kujiuliza ni kwamba tunalia au kuhuzunika kwa sababu matatizo yetu ni makubwa au ni kwa sababu yametuumiza sana na tumejikuta tukiwa ni watu ambao hatujui nini cha kufanya?

Hebu tujiulize ni wangapi tunahuzunikia mishahara midogo tunayolipwa makazini mwetu? Je katika huzuni hizo tulishawahi kuwaza kwamba kuna binadamu wengine hawana kazi na wanahangaika kutafuta shilingi mia tano kwa kuuza mihogo na karanga kwenye kona za mitaa huku wakiwa juani?. Kama hao wapo ukubwa wa tatizo la mshahara kidogo unaotuliza kila siku uko wapi? Uko wapi ukubwa wa tatizo la kutokuzaa wakati kuna waliozaa na watoto wote wakafa.

Kimsingi uwiano wa shida na uhimili wake unaopatikana baina ya mtu na mtu, kamwe sifa ya huzuni hailetwi na ukubwa wa tatizo, isipokuwa ni kukosekana kwa sanaa ya kuishi, yenye maono na hisia za kupunguza mambo makubwa kuwa madogo. Katika hisia, mwanadamu hawezi kuzuia machozi ya furaha au huzuni yasitoke, ni kitu ambacho hakiwezekani kabisa. Ifahamike kwamba kila mwanadamu ana uwezo wake wa kufanya, zaidi ya tatizo analokutana nalo.

Bila shaka umewahi kuona au kuwasikia watu wanalia kila siku kwa kuhitaji utajiri, lakini hawafikii malengo kwa sababu wanaona umasikini ni jambo kubwa na kuufikia utajiri ni jambo kubwa pia. Kitakachotokea hapo kama mambo yote ni magumu ni huzuni ndani mwao. Unaweza pia ukajiuliza mwenyewe ni kitu gani kinakuliza? Fahamu kwamba hulii au kuhuzunika kwa sababu matatizo ni makubwa, bali umekosa ufahamu wa maono.


Hebu chukua jukumu la kudharau shida zako kwa kujilinganisha na wengine ambao ambao wana matatizo makubwa kuliko yako. Fanya hivyo kila unapokabiliwa na tatizo, usilione tatizo ni kubwa kwa takwimu, lichukulie kuwa ni dogo kisha uanze kulishughulikia, utaona linamalizika kwa ushindi mkubwa. Kamwe usijaribu kulitatua kwa kulikuza sana, hutapata matokeo mazuri. Kuwa na mtizamo chanya kwenye tatizo lako, itakusaidia kukabiliana nalo vizuri.

Ya nini ulie na kuhuzunika kila siku? Ukiwa ni umasikini, kutokuzaa, kukosa kazi, kuteswa na mume na matatizo yote yatakayokukuta katika maisha yako yaone ni madogo kisha tumia nguvu zako zote kuyakabili nina hakika utayashinda kirahisi. Jaribu kupunguza matatizo, badala ya kuyakuza kwa kuona hayawezekani kutatuliwa, utaona majibu yake. Tambua kuwa tatizo lako si kubwa bali unalikuza katika mawazo yako, kwa kuwa wapo wenye matatizo makubwa zaidi yako na hawalii kama wewe.

Ili uweze kuwa mshindi na usihuzunike tena kumbuka hili siku zote ‘nyakati ngumu katika maisha hazitaisha, ni jukumu lako kukabiliana nazo tu.’ Jiulize tena mwenyewe, kama ni kulia utalia kwa mangapi? Dunia haina usawa, jifunze kuyakabili matatizo yako kwa mtazamo chanya hapo utakuwa mshindi. Acha kuwa na huzuni na simanzi kupitiliza linalokuhuzunisha siyo tatizo kubwa sana. Wapo watu ambao walishashavuka tatizo kama lako jifunze kwao, kisha songa mbele.

Nakutakia maisha mema yawe na amani na furaha, ansante kwa kutembelea DIRA YA MAFANIKIO endelea kujifunza na kuhamasika zaidi.

DAIMA TUPO PAMOJA MPAKA MAISHA YAKO YAIMARIKE,

IMANI NGWANGWALU,

0713 048 0345/dirayamafanikio@gmail.com   



Dec 20, 2014

Kama Unafanya Mambo Haya, Utajiri Kwako Ni Lazima.

No comments :
Kuwa na mafanikio makubwa na hatimaye kuwa tajiri ni kitu ambacho kinaonekana kuwa kigumu kwa wengi ama hakiwezekani kabisa. Hii yote inatokana na wengi kutokujua njia au mambo muhimu ya kufanya hadi kufikia mafanikio makubwa. Kutokana na hili wengi wamekuwa wakijiuliza wafanye nini au kitu gani kitakachowafanikisha katika maisha yao.

Kiuhalisia, katika maisha kuna vitu ambavyo ukifanya iwe kwa kukusudia au bahati ni lazima uwe tajiri na pia kuna vitu ambavyo ukifanya, sahau mafanikio katika maisha yako. Vitu hivi vinaweza kuwa tabia zetu au mienendo tuliyonayo ambayo inakuwa inaathari kubwa kwetu na hii ndiyo naweza sema ni siri kubwa iliyofichika kati ya watu wenye mafanikio na ambao hawana.

Watu wenye mafanikio wamemudu kwa kiasi kikubwa kufanya mambo yanayowafanya wawe matajiri, huku maskini wakiwa hawajui hilo na kuendelea kufanya vitu vinavyowafanya kuwa maskini. Kwa wewe kulijua hilo tu, tayari una nafasi kubwa ya kufanikiwa na kufanya mambo makubwa katika maisha yako. Kama kweli umechoshwa na umaskini, na umedhamiria kweli kuwa tajiri hakikisha unafanya mambo haya:-

1. Hakikisha unajiwekea mipango na malengo makubwa.

Kama kweli unataka kufanikiwa na kuwa tajiri ni lazima ufanye hili. Huwezi kufanikiwa kwa kiasi kikubwa kama una tabia ya kujiwekea malengo kidogo. Watu wote wenye mafanikio huwa ni watu wa kujiwekea malengo makubwa na ambayo huanza kuyafatilia kila siku na kuhakikisha mpaka yanatimia.

Acha kujidharau au kujiona hufai eti kwa sababu huna pesa na ukashindwa kujiwekea mlengo yako. Panga mipango yako vizuri, kama ni pesa zitakuja zenyewe wakati unaendelea kutekeleza mambo mengine. Ukiwa na malengo makubwa hii itakusaidia kufanya kazi kwa bidii kubwa na hautaweza kukata tamaa mapema. Chukua tabia hii muhimu ikusaidie kukufanikisha.


2. Hakikisha unatumia muda wako vizuri.

Muda ni kitu muhimu sana katika maisha yetu. Kama wewe ni mtunzaji mzuri wa muda na haupotezi muda hovyo, elewa kabisa kufanikiwa kwako ni lazima. Watu wengi kutokana na kutokujua ama mazoea ambayo wanayo toka mwanzo, ni watu wa kupoteza muda sana. Kama tabia hii ndiyo unayo, kufanikiwa na kupiga hatua mbele itakuwa ngumu katika maisha yako. Jifunze kutunza muda utaona mafanikio makubwa sana ambayo hukufikiri hapo mwanzo.

3. Hakikisha unajifunza vitu vipya kila siku.

Tatizo kubwa walilonalo watu wengi ni kutopenda kujifunza vitu vipya.. Wengi ni wavivu wa kusoma hali ambayo  hupelekea kukosa vitu vizuri vyenye uwezo mkubwa wa kubadilisha maisha yao. Kama unataka mafanikio makubwa katika maisha yako, ni lazima uwe msomaji mzuri pia. Hii itakusaidia wewe kupambana na changamoto kwa kujua wengine waliweza kukabiliana nazo vipi. Ni lazima ujenge utaratibu wa kujisomea vitu vitakavyobadili maisha yako.

4. Hakikisha usiwe mtu wa kulaumu tu.

Wapo watu ambao siku zote ni watu wa kulalamika tu na kulaumu wengine ndio waliopelekea wao kuwa hivyo. Hawa ni watu ambao mara nyingi hufikiri kuwa wao wamekuwa maskini pengine kutokana na wazazi hawa kuwasaidia au hawakusoma na visingizio vingi tu. Hii ni tabia ambayo haiwezi kukufikisha popote, zaidi ya kukurudisha nyuma. Kama nia yako kubwa ni mafanikio achana na visingizio, chukua hatua za kusonga mbele. Vipo vitu vingi vya kufanya na ukaondokana na kulaumu kwako. (Unaweza ukasoma pia Huu Ndio utajiri mkubwa utakaoupata kama utaamua kufanya biashara hii)

5. Hakikisha unaye ‘mentor’ wa kukuongoza kwenye mafanikio yako.
Asilimia kubwa ya matajiri wote walioko duniani wanao watu waliowaongoza katika maisha yao hadi kufanikiwa. Ni muhimu hata kwako wewe kuwa na ‘mentor’ au mtu ambaye atakuongoza kwenye mafanikio yako. Mara nyingi huwa hatujui kila kitu katika maisha yetu. Kama katika kitu ulichochagua kufanya yupo mtu ambaye tayari amefanikiwa katika hilo eneo ni vizuri ukamtumia ili akakuongoza ili usije ukapotea kiurahisi na kufanya makosa ambayo pengine hukustahili kuyafanya.

6. Hakikisha unaepuka madeni yasiyo ya lazima.

Kama umekopa mkopo benki, hakikisha huo mkopo unakusaidia kuongeza kipato chako. Acha kukopa mkopo halafu unaamua kujengea nyumba au kununua gari, na matokeo yake pesa zote unazipoteza unaanza kuhangaika namna ya kulilipa deni hilo. Kati ya vitu ambavyo vimewafanya wengi kujuta na kujilaumu katika maisha yao ni mikopo. Kama umeamua kukopa, uwe mwangalifu ili usije ukaumia baadae wakati unarudisha hilo deni. Kikubwa jifunze kutumia mkopo vizuri.

7. Hakikisha unaweka akiba ya kutosha .

Kila pesa unayopata hakikisha unajiwekea akiba yako. Wataalamu wengi wa masuala ya mafanikio wanashauri angalau asilimia kumi ya kile unachokipata iweke kama akiba yako. Pesa hii inapokuwa nyingi itakusaidia wewe kuwekeza katika miradi yako mbalimbali. Hakikisha pesa hii unaiwekeza na usiitumie katika matumizi mengine yasiyo ya lazima. Kama ukifanya hivi kwa pesa hii utakuwa upo kwenye nafasi ya kupata mafanikio makubwa katika maisha yako.

Kwa kufanya mambo hayo unao uwezo mkubwa wa kubadilisha  maisha yako kwa jinsi unavyotaka na kuwa tajiri. Kumbuka hukuzaliwa maskini au mlalahoi kama unavyodhani, kikubwa jifunze kuwa na fikra sahihi zitakazo badili maisha yako na kisha chukua hatua sahihi kuelekea malengo yako uliyojiwekea. Hakuna kinachoshindikana kila kitu kinawezekana endapo tu ukiamua.

Nakutakia kila la kheri katika safari yako ya mafanikio na endelea kutembelea mtandao huu wa DIRA YA MAFANIKIO kwa kujifunza na kuhamasika zaidi.

DAIMA TUPO PAMOJA MPAKA MAISHA YAKO YAIMARIKE,

IMANI NGWANGWALU,






                                              

Dec 18, 2014

Kanuni Muhimu Katika Kuendesha Biashara Yako, Ili Iwe Na Mafanikio Makubwa Unayoyataka.

No comments :
Wengi wetu tumekuwa tukibuni, tukiiga na hata kuanzisha biashara mbalimbali ambazo, zimekuwa hazidumu wala kuendelea kwa muda mrefu kwa sababu ya kufilisika. Kukwama na kufilisika au kutokuendelea kwa biashara zetu hizi, limekuwa ndilo tatizo sugu au kikwazo kigumu kwa wafanyabiashara walio wengi, wakubwa kwa wadogo.

Wengi wetu tumekuwa tukilitafutia dawa au suluhisho la kudumu tatizo hili bila mafanikio. Kuendelea kudumu kwa tatizo hili, kumesababisha baadhi ya watu kukata tamaa kabisa ya kuendelea kufanya biashara. Hata hivyo maelezo na mifano halisi nitakayoitoa hapa, inaweza kutusaidia kutupatia majibu ya uhakika au suluhisho la kudumu nini kifanyike.

Ni muhimu kwetu kufata maelezo haya au kanuni hizi ikiwa endapo tumedhamiria kutimiza wajibu wetu wa kufanya biashara tuzipendazo, ili kuboresha maisha yetu na jamii kwa ujumla. Kanuni hizi ni muhimu hasa kwa watu walioamua kuanzisha biashara ndogondogo na wanazomiliki wenyewe, pengine baada ya kuchoshwa na kazi za kuajiriwa au kwa sababu nyingine.

Ukiweza kuzitumia kanuni hizi ndogondogo vizuri katika biashara yako, itakuletea mafanikio makubwa unayoyataka na hutajuta tena. Huna haja ya kulalamika tena wala kulaumu kwa sababu ya biashara zako kwenda hovyo, ni wajibu wako sasa kuzitumia kanuni hizi ili uone manufaa yake katika biashara yako. Unajua kanuni hizi ni zipi?

Hizi ndizo kanuni muhimu katika kuendesha biashara yako, ili iwe na mafanikio makubwa.

1. Ifanye biashara yako iwe ya thamani na ubunifu kila siku.

Kushindwa kutambua thamani ya ubunifu, ni jambo ambalo hupaswi kulifanya. Ni rahisi kuangukia kwenye mtego wa dhana kwamba lengo la biashara ni kutengeneza fedha tu. Lakini lengo sahihi la biashara ni kutengeneza thamani. Wakati si rahisi kutengeneza fedha katika kipindi kifupi bila kutengeneza thamani, kutengeneza fedha bila thamani si kitu cha kudumu.

Ni lazima biashara yako iweze kujenga thamani kwa ajili yako na wateja wako. Kwa jinsi utakavyotambua thamani ya kile unachotoa, ndivyo utakavyoweza kuelekeza nguvu zako zaidi. Kama biashara yako ni ya michezo kama ya kompyuta ama mingine, basi ujue thamani unayotengeneza hapo ni kuburudisha akili.

Ni kwa kutambua hivyo tu, ndipo utakapoweza kujitahidi kufanya huduma yako iwe bora zaidi na kuthamini wateja wako. Imetokea mara nyingi wamiliki wa biashara wameshindwa kutambua thamani wanayojaribu kutoa. Hawa hubaki tu wakitarajia makubwa bila ya kujua watayafanya vipi, kwani hawajui hata lengo la biashara yao. Ukitoa thamani kwa huduma unayotoa, wateja utapata tu.


2. Acha kujaribu kuuzia watu wasio sahihi.

Wakati mauzo ni kitu muhimu ili biashara iweze kudumu, huna haja ya kuhamanika kwa hilo na kudhani unalazimika kumlazimisha kila mtu unayekutana naye kufanya nawe biashara, ikiwa ni pamoja na marafiki zako na watu wa familia yako. Ni kupoteza wakati kujaribu kuwauzia watu ambao unajua wazi hawahitaji kile unachouza.

Kuuzia watu wasio sahihi ni pamoja na kujaribu kumuuzia kila mtu unayemwona mbele yako. Wapo wateja ambao ni rahisi kuwauzia kile ulichonacho kuliko wengine. Kwa mfano unafanya kazi ya kutengeneza tovuti halafu unakutana na mtu asiyejua chochote kuhusu intaneti na unaanza kumtangazia biashara yako ya tovuti, ni wazi utapoteza wakati wako kwani huyu si mteja wako sahihi.

Unatakiwa uwe na uwezo wa kukataa kuwapatia maelezo wateja wanaoonekana wazi kuwa na uwezekano wa kukuletea matatizo kuliko faida katika biashara yako. Waache wapinzani wako wafanye kazi ya kuwauzia badala yake. Kwa kufanya hivyo utajiokoa na matatizo ya kuumia kichwa kwa kuongea na watu ambao sio sahihi katika biashara yako.

3. Acha kutumia pesa nyingi kupita kiasi.

Kama biashara yao bado ni changa, acha kutumia pesa nyingi kupita kiasi mpaka utakapokuwa na mtiririko wa uhakika wa fedha zinazoingia. Usitumie fedha za kufanyia biashara hadi pale itakapokuwa muhimu sana na kwa manufaa yaliyo wazi kwa biashara yako. Hapa itabidi ujifunze kutokufanya matumizi yasiyo ya lazima katika biashara yako.

Ili kufanikiwa katika suala hili la kutokutumia pesa nyingi kupita kiasi, ni muhimu kujua utumie nini, kwa sababu ya nini, na kwa nini. Ikumbukwe pia katika malengo ya kawaida ya biashara, biashara inatakiwa kuingiza fedha mfukoni mwako, hivyo kabla ya kuwekeza unatakiwa ujue namna ya fedha ulizotoa mifukoni mwako kuwekeza zitakavyorudi.

4. Acha ugumu (ubahili) katika kutumia fedha.

Wakati kutumia pesa nyingi bila umuhimu ni kosa katika biashara, ni kosa pia kufanya biashara yako huku ukiweka mbele matumizi yaliyotawaliwa na ugumu katika matumizi ya fedha zako hata pale inapokuwa muhimu. Usiruhusu ugumu au ubahili ukwamishe ufanisi wa kazi yako.

Kama itatakiwa kuwatumia wataalamu wazuri wenye uwezo wa kufanya kazi Fulani vizuri kuliko utakavyofanya mwenyewe ama watakavyoweza kufanya watu wasio na uhakika, wa bei rahisi ni vizuri ukawatumia hao. Nunua vifaa imara na vinavyofanya kazi vizuri ikiwa una hakika fedha zako zitarudi.

Na mwisho kabisa, ukumbuke pia biashara ya kudumu na endelevu, huhitaji mtu awe amejiandaa na kujidhatiti kifikra, kimtazamo na awe tayari kubadilika kulingana na hali au mazingira ya kibiashara yanayomzunguka, kwani bila ya mambo au kanuni hizo kuzizingatia suala la kufilisika halitakuwa geni kwetu.

Nakutakia kila la kheri katika mafanikio ya biashara yako na endelea kutembelea mtandao huu wa DIRA YA MAFANIKIO kila siku kujifunza zaidi, karibu sana.

MAISHA YAKO YAIMARIKE,

IMANI NGWANGWALU,


Dec 15, 2014

Mbinu Kubwa Ambayo Ukiitumia Itakupa Utajiri Ni Hii Hapa.

No comments :
Kuwa na mafanikio makubwa na hatimaye kuwa tajiri ni kitu ambacho wengi wanapenda sana kitokee katika maisha yao ingawa wengi huwa sio wawazi. Kama ambavyo nimekuwa nikisema mara katika  makala zangu nyingi kwamba,  zipo siri nyingi za jinsi gani unavyoweza kutengeneza pesa zako mwenyewe na hatimaye kuwa tajiri ambazo unaweza ukazitumia kila siku katika maisha yako.

Pamoja na siri hizo muhimu ambazo umekuwa ukijifunza mara kwa mara na zenye uwezo wa kukufanya kuwa tajiri au 
bilionea kabisa wa kesho, leo katika makala hii nataka nikupe siri moja muhimu na kubwa ambayo pengine unaijua au huijui lakini ukiitumia vizuri itakuletea mafanikio makubwa sana katika maisha yako ya kuelekea kwenye utajiri.

Hii ni siri ambayo nimekuwa nikiitumia katika maisha yangu binafsi na wengine wengi waliofanikiwa huitumia pia na imewasidia sana kufikia malengo makubwa waliyojiwekea. Kama siri hii ya kupata utajiri imefanya kazi kwao na kwako pia itafanya kazi. Ukiweza kuitumia siri hii vizuri katika maisha yako itakujengea uwezo mkubwa wa kumudu kufanikiwa kwa chochote unachofanya katika maisha yako.

Watu wengi wenye mafanikio wanaijua vizuri siri hii na ndiyo inayowafanya wawe juu siku zote. Wengi wanaoshindwa kufanikiwa na kujikuta mbio zao nyingi zinaishia kati katika maisha yao ni kutokana na kushindwa kuitumia siri hii vizuri, nami sitaki uwe miongoni mwao nataka uwe mshindi ili tuwe pamoja katika kilele cha mafanikio.



Pengine unajiuliza ni siri ipi hasa unayoweza kuitumia na kuleta mafanikio makubwa kwako. Siri hii unayotakiwa kuwa nayo ni siri ya kujikubali mwenyewe na kuamini unaweza kufikia malengo makubwa uliyojiwekea.

Wataalamu mbalimbali wa elimu za mafanikio akiwemo Dr. Vicent Norman Pealle wameeleza hili sana ili uweze kuwa na mafanikio yoyote makubwa ya kimaisha hatua ya kwanza unayotakiwa kuchukua ni kujikubali mwenyewe na kuamini kuwa uwezo huo wa kufanikiwa unao.

Haijalishi watu wengine wanasema nini juu yako iwe kwa mabaya au mazuri, udhaifu fulani au ubora kinachotakiwa ni kujikubali mwenyewe na kuamini unaweza kufikia mafanikio yoyote bila ya kuzuiliwa na kitu chochote kumbuka ndani yako una uwezo mkubwa sana kuliko unavyofikiri.

Wengine wanasubiri mpaka wasifiwe katika nyanja fulani ya maisha ndipo wajikubali wenyewe kuwa wanaweza kufanikiwa na wanapokuwa wanaacha kusifiwa basi kujikubali huanza kufifia pole pole na pengine kufa kabisa. Kitu usichokijua unaposhindwa kujikubali mwenyewe na kuamini kuwa unaweza kufanikiwa unakuwa unazuia mafanikio mengi sana ambayo yangeonekana kwako. Hiyo inakuwa ni sawa na kupoteza maisha yako.

Tatizo walilonalo watu wengi kutokana na mazoea yao au malezi waliyokulia huwa sio rahisi kujikubali wenyewe na kuamini kuwa wanaweza kufanikiwa na kufikia mafanikio makubwa kabisa katika maisha yao. Ni wepesi sana kuwakubali wengine kutokana na yale wanayoyafanya kuliko kujikubali wenyewe.

Watu wa namna hii mara nyingi huwa sio rahisi kusimama peke yao kwenye maisha na kufanikiwa, kwani wao wanaamini wapo watu wanaoweza zaidi yao kufanikiwa na kujikuta ni watu wa kujishusha tu na kujiweka pembeni na kusubiri hao wanaoweza waweze. Ni kweli kutokana na kutokujikubali kwao hao wanaoweza hujikuta wakiweza kweli huku wenyewe wakijikuta wakiwa ni watu wa kushindwa katika mambo mengi katika maisha yao.

Jiulize mwenyewe binafsi unajikubali na kujiamini kwa kiasi gani kwamba unaweza kufikia ndoto na malengo yako uliyojiwekea bila ya kuzuiwa na kitu chochote kile. Kama hujiamini ujue kabisa kwako itakuwa ngumu kufikia ndoto zako. Chukua hatua ya kujiamini ili uweze kuishi maisha ya mafanikio unayotamani kila siku kuyafikia.

Hii ndiyo siri kubwa ya mafanikio unayopaswa kuitumia katika maisha yako. Nakutakia ushindi mkubwa katika safari yako ya mafanikio. Endelea kuwashirikisha wengine kujifunza mambo mengi mazuri yanayoendelea katika mtandao wa DIRA YA MAFANIKIO na hakikisha usikose kusoma kila siku kwa ajili ya kujifunza zaidi na kuweka hazina kubwa itakayokusaidia katika maisha yako yote.

DAIMA TUKO PAMOJA MPAKA MAISHA YAKO YAIMARIKE.

IMANI NGWANGWALU – 0713048035/dirayamafanikio.blogspot.com


Dec 10, 2014

Huu Ndio Utajiri Mkubwa Utakaoupata, Kama Utaamua Kufanya Biashara Hii.

3 comments :
MAKALA HII IMEANDIKWA NA MESHACK MAGANGA WA IRINGA TANZANIA.
Kwa muda mrefu nimekuwa nikitoa hamasa kwa vijana wenzangu wa kike na kiume na watu wa kada mbalimbali, wito wangu umekuwa nikuwataka vijana wenzangu kauanza utamaduni wa kuwekeza kwa muda mrefu na kujifunza ujasiriamali. Ninaandika makala hii kutoa ushuhuda wa niliyoyafanya kwa muda wa zaidi ya miaka miwili iliyopita na kuniletea mafanikio makubwa.

Nilianza kujishighulisha na ujasiriamali nilipokuwa chuo kikuu mwaka wa pili, kwa kuuza vocha na  kazi ya ‘steshenari’ na uuzaji wa laptop, sikuendelea nazo sana kwa sababu ya kubanwa na masomo yachuo. Nilipomaliza chuo 2010, nilianza kilimo cha mboga na kufuga kuku hapa Iringa mjini, baada ya hapo kaka yangu alianza kunihimiza kuhusu kilimo cha miti ambacho yeye mwenyewe anafanya.

Na baadaye nikakutana na rafiki yangu Albert Sanga ambaye pia anajishughulisha sana na kilimo cha miti. Tangu 2011 nilinunua shamba la ekari 10 na kuzipanda miti hela ambayo niliipata baada ya kuuza matango niliyolima kijijini Kalenga, nikaongeza bidii zaidi ya kulima matango na kununua mashamba, leo nina ekari nyingi.

Albert sanga, mjasirimali na mwekezaji alipata kuandika haya kuhusu mimi:-
UNASUBIRI UPATE MTAJI? OPSss! UNAWEZA KUFA MASIKINI! Nina rafiki yangu mpambanaji kweli kweli na msomi wa chuo kikuu wa mambo ya maendeleo na elimu; na mtaalamu wa IT, anaitwa Meshack Maganga. Wakati fulani huko nyuma alinifuata na kuniambia, "Sanga nimeamua kuanza kui-invest katika mashamba ya miti; mtaji wa kuanzia nina tsh elfu ishirini na tano, (25,000?/=).


Nikamwambia "Kupata ekari moja si chini ya laki sita na wewe una tsh 25,000/= utawezaje?" Akanijibu "Nitaweza!", Sikumwelewa! Kumbe alikuwa anaona mbali! Alichofanya alichukua hiyo 25,000/= akaenda nayo eneo moja linaitwa Kalenga (km 20 kutoka Iringa mjini) huko akalima matango. Angalia mchanganuo: Shamba nusu eka akakodi kwa tsh 10,000/=, mbegu za matango akanunua Tsh. 7,000/=.

Kwenye kulima akalima kwa mikono yake akisaidiana na kibarua mmoja. Fedha iliyobaki 8,000/= akalipa kibarua na kununulia dawa ya kuua wadudu. Alipokuja kuvuna akapata tsh 800,000/= (laki nane). Alipokuja na fedha hii tukaenda kutafuta shamba la miti akaanza na ekari moja huku pesa nyingine akairudisha shambani.

Hivi leo Bw. Maganga ana ekari zisizopungua hamsini za mashamba ya miti na anaendelea na kilimo cha umwagiliaji. Lakini HAPO amefika kwa kutumia tsh 25,000/= tu. Tunaposema hauhitaji mamilioni kujiajiri tunatamani ujifunze kutoka kwa waliofanikiwa kama Bw. Maganga. Unaweza kumwandikia” Akaendelea kwa kusema:-

Kuhusu kilimo cha miti ninacho kifanya mimi na nimepania kwelikweli ndani ya nchi yangu niipendayo Tanzania ni kwamba, kimepata umaarufu wa ghafla miaka ya hivi karibuni kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo ongezeko la mahitaji ya mazao ya miti na changamoto ya mazingira. Katika Tanzania mkoa wa Iringa ni moja ya mikoa maarufu inayoongoza kwa misitu mikubwa ya kupandwa.

Miti inatumika kwa mbao, nguzo za umeme, nguzo za kujengea pamoja na utengenezeaji wa karatasi. Ukiacha mahitaji haya tuliyoyazoea; hivi sasa kumeibuka fursa nyingine mpya ambapo mashirika ya kimazingira kutoka Magharibi yananunua hewa ukaa. Kwa maana hiyo unaweza kupanda shamba la miti halafu ukawa unakusanya dola kwa kuuza hewa ukaa wakati ukisubiri miti ikomae uvune mbao, nguzo ama miti ghafi ya kutengenezea karatasi.

Hii ni sawa na kutegeneza hela ukiwa umelala. Mbali na kuuza hewa ukaa, vile vile unaweza kufuga nyuki na kuendelea kuvuna asali wakati unasubiri kukusanya mamilioni kwa kuuza miti ya nguzo, karatasi ama mbao.Kilimo hiki cha miti ni uwekezaji wa muda wa kati na mrefu (middle& long term investments). Kiutamaduni watanzania wengi huwa hawavutiwi na uwekezaji wa muda mrefu.

Hata hivyo kama una mpango wa kuwa na “financial freedom” usikwepe kufikiria uwekezaji wa muda mrefu. Waingereza husema “Information is power”. Wengi hawajachangamkia fursa hii kwa kukosa taarifa tu. Kazi yangu leo ni kukupa taarifa hizi za utajirisho. Miti ya mbao inatumia wastani wa miaka sita hadi 8 au saba, tangu kupandwa hadi kuvunwa kwake.

Hii ina maana inapofikisha umri wa miaka sita huwa tayari kwa kuanza kuvunwa kwa mbao ndogo. Ekari moja ya shamba inachukua wastani wa miti mia sita (600). Wastani wa chini wa mti mmoja kwa sasa uliokomaa ni shilingi elfu ishirini (30,000 hadi 60,000,inategemea na ukubwa wa mti). Ina maana katika ekari moja ukiwa na miti iliyokomaa unakusanya jumla ya shilingi milioni kumi na nane (18,000,000). 

Fedha hiyo (kadirio la chini kabisa) utaipata ikiwa unaamua kuuza kwa bei ya jumla miti ikiwa shambani. Lakini kama ukiamua kupasua mbao wewe mwenyewe unaweza kuvuna mbao hadi za milioni thelathini na mbili (32,000,000) kwa ekari moja. Hadi sasa uhitaji (demand) wa mbao katika soko ni mkubwa kuliko ugavi (supply) hivyo kwa miaka 10 ijayo hatutarajii kushuka kwa soko la mbao, nguzo ama malighafi za karatasi.

Gharama ya kununua shamba tupu ni kati ya shilingi  laki moja na 20 elfu (120,000) na laki moja, kutegemea na maeneo husika unayotaka ama kupata. Gharama za kuandaa shamba, kununua miche na kupanda ni kati ya shilingi laki moja  na nusu,na laki moja. Hii ina maana unaweza kumiliki ekari moja ya msitu wa miti kwa hadi shilingi laki sita tu! Kutegemea na umri wa miti unayotaka.

Mtu unaweza kuona kuwa pengine kununua shamba tupu na kuanza kuhangaika na upandaji miti itakuwa ni mlolongo mkubwa; kukusaidia katika hilo nimekuwa na utaratibu wa kumilikisha mashamba yenye miti (kuuza) kwa bei nafuu sana. Yapo mashamba yenye miti ya kuanzia mwaka mmoja, miaka miwili, miaka mitatu na miaka minne.

Uponunua mashamba haya kutoka kwangu, mimi naendelea na upandaji wa mashamba mapya kupitia fedha hizo. Kilimo cha miti ni rahisi sana kwa sababu ukishapanda hakihitaji uangalizi mkubwa sana na wala hauhitajiki uwe karibu na shamba/mradi muda wote. Kuna kazi chache ambazo zinahitajika ukishapanda shamba lako.

Mvua inyeshe ama isinyeshe mti wa mbao, nguzo ama karatasi ukishachipua huwa haufi kwani huendelea kutumia unyevu wa ardhini. Kazi namba moja unapokuwa umeshakamilisha upandaji wa miti kwenye shamba; ni kutengeneza njia za kuzuia moto walau mara moja kwa mwaka, kazi ya pili ni kufyekea miti inapokua walau kwa mwaka mara moja (prooning).

Gharama zote hizo yaani kutengeneza njia za moto, kufyekea na kulinda moto haizidi laki mbili kwa mwaka mzima. Kwa maana hii gharama za kuhudumia shamba la miti ekari moja kutoka kupandwa hadi kuvunwa ni wastani wa shilingi milioni moja tu. Gharama hizi ninazopiga ni ikiwa utaamua kununua shamba leo na kama ungekuwa tayari una shamba ambalo unalihudumia leo.

Hata hivyo nadhani wote tunafahamu kuwa ardhi ni rasilimali inayopanda thamani kila siku. Vile vile tunatambua kuwa suala la mazingira ni tete kwa sasa na katika karne zijazo kama wataalamu wanavyotuthibitishia. Hii ina maana kuwa ukiwa na shamba la miti leo; thamani ya ardhi hiyo inazidi kupanda kila siku na miti uliyopanda inazidi kupanda thamani kila kukicha.

Jambo la uhakika ni kuwa hata kama bei ya miti, mbao, nguzo itayumba hutaweza kupoteza mtaji uliotumia na wala hutakosa kuzalisha faida kwa shamba utakalokuwa umemiliki, iwe ni eka moja, kumi, mia ama elfu moja. Mbali na hivyo unaweza ukaona, ahaa, miaka sita hadi kumi ni mingi mno; bado una nafasi ya kupata faida hata ndani ya mwaka mmoja, miwili au mitatu.

Ukishapanda shamba la miti ekari moja kisha baada ya mwaka mmoja ukaamua uuze utauza si chini ya milioni mbili hadi nne. Kukusanya milioni nne kwa mtaji wa laki sita, pasipo kutumia muda mwingi ama usumbufu wa kusimamia; hakika ni faida nono.

Huenda hadi kufika hapa unaweza ukawa umeshavutiwa na biashara hii. Wengi wenu mnaweza kujiuliza maswali mkubwa mawili; “Ninatamani nifanye mradi huu lakini Iringa sikufahamu na hata kama nakufahamu nitaanzia wapi kupata hayo maeneo?” Pili: Niko mbali na sina muda wa kushinda Iringa, Je, ni nani atanisaidia kupanda, kusimamia na kuendesha hayo mashamba?

Ili kutimiza ndoto yangu hiyo nimeweka utaratibu ufuatao utakaohakikisha kila mwenye ndoto, kiu na hamasiko la kuwekeza kwenye kilimo cha miti anafanikiwa.  Jisikie huru wakati wowote kuwasiliana nami kwa ufafanuzi na msaada wa fursa hii. Natamani watanzania tuache kulalamika kuhusu wageni kuvamia ardhi yetu, badala yake tuchangamke kumiliki na kufanya uzalishaji katika ardhi yetu.

Inawezekana! Kwa kutumia sheria ya ardhi ya mwaka 1999 sheria namba 5 utapata documents za umiliki; kwa kuzingatia taratibu na tamaduni zote za wenyeji zinazohusiana na umilikaji ardhi nitahakikisha nakusaidia ili ndoto yako itimie.

Yupo Baba yangu anaishi Mafinga ambae siku za karibuni amepewa Tuzo ya Rais kwa kuwa mpandaji namba moja wa miti na utunzaji wa mazingira, ameahidi kutoa msaada kwa Mtanzania wa ndani na nje ya Tanzania kumsadia kupata eneo la kupanda miti na kauli ya siku zote ni
“USIKUBALI KUWA MNYONGE WA KIUCHUMI NDANI YA TANZANIA.

UNAWEZA KUWASILIANA NA MWANDISHI WA MAKALA HII MESHACK MAGANGA KWA 0713 486 636