google-site-verification: googleabbfd1327a3af7a3.html

DIRA YA MAFANIKIO

Badili maisha yako sasa kwa kuwa na fikra sahihi.

Kujifunza zaidi juu ya maisha na mafanikio, nakualika kwenye kundi la whats app kujifunza kwa kina. Tututumie ujumbe kwa njia ya whats app kwenda 0687449428 kupata utaratibu wa kujiunga.

May 30, 2015

Haya Ndiyo Mambo Mawili Usipokuwa Nayo Makini Yatakutesa Na Kukusumbua Sana Katika Maisha Yako.

No comments :
Hebu jaribu kufikiria iwapo unaona kwamba maisha yako hayakuendei vema, huku watu wengine unaofahamiana nao, pamoja na majirani zako, maisha yao yakiwaendea vizuri bila shida yoyote ile. Wenzako hao wananunua magari, wanajenga majumba, wanasomesha watoto wao katika shule nzuri na wanaishi maisha mazuri kuliko wewe. Je wewe utawazaje? Utajisikiaje? Utawaonea kijicho ama?
 
Ni kweli kabisa kwamba, kuna wakati ambapo huwa tunataka kuwa na kila kitu, ili kuoekana kuwa na maisha bora pengine hata zaidi ya hao wengine tunaowaona. Lakini swali la msingi hapa tunalopaswa kujiuliza ni kwamba, je, katika hali halisi jambo hili linawezekana?

Kulingana na maoni ya Jo Anne White ambaye ni profesa wa elimu katika chuo kikuu cha Temple nchini marekani, ni kwamba kijicho huonesha ile hali ya mtu kujitazama na kujijali yeye mwenyewe. Ni suala linalohusu namna watu wanavyojihisi kujielekea wao wenyewe na iwapo kweli wanajiamini kuhusu namna walivyo.

Kijicho na wivi ni kama ndugu mapacha. Kwa mfano, unaweza kuona wivu iwapo mwenzi wako wa ndoa hakujali. Vilevile wivu unaweza ukachochewa endapo mwenzako wa karibu atakufanya usijisikie vizuri kwa kutumia maneno ya kuumiza na vitendo pia.


Ikumbukwe pia katika uhusiano wowote ule, kuaminia, kutamaniana na kuheshimiana kwa dhati ni mambo muhimu katika kufanya uhusiano huo ustawi na kuimarisha mawasiliano yenye nguvu.


Vilevile kama mtu ana picha mbaya na isiyo na nguvu kujihusu, mara nyingi anaweza kuhisi kutishiwa na kuamini kwamba, hana lolote atakaloweza kuchangia katika kumfanya mtu yeyote yule avutiwe naye.

Kwa kawaida, mwanzoni tabia ya wivu inaweza ikaonekana kuwa ni hali fulani ya urafiki, hasa iwapo mtu wako wa karibu atahitaji muda wako mwingi wa kumjali na inaweza pia kuwa ni dalili ya kukosa ukaribu kwenye hisia.

Ni ukweli ulio wazi kwamba, suala la wivu huweza kuibuka pale mtu anapohisi kukosa usalama na kutishiwa, ama kwa kuhofia kupoteza uhusiano wake au kwamba mtu mwingine badala yake anathaminiwa kama yeye ambvyo alikuwa akithaminiwa.

Hata hivyo wivu hauko kwenye uhusiano wa kimapenzi tu, pia upo kwenye mafanikio ndio kitu ninachotaka kuzungumzia hapa kama nilivyoanza makala hii. Kwani, mtu ambaye hana picha kubwa na yenye kujielekea yeye mwenyewe atakuwa ni rahisi kwake kuhisi kwamba watu wengine wanamuonea wivu na kijicho kwa mafanikio yake.


Kulingana na maoni ya Debbie ambaye ni mwandishi wa kitabu kiitwacho Turn off your inner light: Fitness of of body, mind and soul, ni kwamba, wanaume wengi hupatwa na hali ya kijicho kinachohusiana na kujipatia mali, kama vile kazi nzuri, heshima au hadhi fulani,nyumba nzuri, ambapo kwa upande mwingine, wanawake wao huwa ni mwenye kijicho kuhusiana na mwonekano wao ikiwemo sura, watoto na marafiki zao.

Ili kuweza kukabiliana na kijicho katika maisha yetu, mtu anapaswa kutambua uwezo na nguvu zake, kwa maana kwamba anamudu kufanikisha nini, nini malengo yake aliyojiwekea katika maisha yake. Usijilinganishe na mtu au watu wengine, kwa sababu kwa kufanya hivyo ni sawasawa na kuhujumu uwezo wako pekee.

Wahakikishie  watu wengine na wewe mwenyewe kwamba, leo ni siku yako na zamu yako kufanikiwa, na siyo kesho ila fanya hivyo kwa vitendo. Tumia kijicho hicho hicho ulichonacho na kukuchochea uweze kukamilika na kukua. Hapa tunasema kuwa na kijicho cha maendeleo. Jiambie, kuwa kama fulani ameweza , ni wazi kwamba, inawezekana hata kwangu na nitafanya hivyo.

Kama kuna mtu ambaye anapenyeza sumu ili kufanya uone wivu au kijicho katika jambo fulani, basi unalazimika kubadili mada kwenye mazungumzo yenu au kama ni lazima jiondoe machoni pa mtu huyo. Acha kuwa na kijicho ama wivu sana unaokuumiza wa mafanikio yaw engine. Jipange na tafuta mafanikio yako, vinginevyo hayo ndiyo mambo mawili usipokuwa nayo makini yatakutesa na kukusumbua sana katika maisha yako.  

Tunakutakia kila la kheri katika safari yako ya mafanikio, endelea kutembelea DIRA YA MAFANIKIO kujifunza zaidi kila siku.

DAIMA TUPO PAMOJA MPAKA MAISHA YAKO YAIMARIKE,

IMANI NGWANGWALU,
0713 048035,

May 29, 2015

Hivi Ndivyo Unavyoweza Kuishi Na Watu Wasumbufu Ulionao Kazini Kwako.

No comments :
Ajira au kazi katika ujumla wake huwakusanya pamoja watu wa tabia, haiba na mikabala mbalimbali ya kimaisha. Tabia na haiba hizi tofauti wakati mwingine huweza kusababisha misuguano , majuto na hata sononi. Kuna wakati bosi ni mkorofi na watumishi wengine wanakuwa wamekaa kisharishari tu.

Hali kama hizi ndizo huwafanya baadhi ya watumishi kusubiri likizo kwa hamu kubwa sana.  Kwa kwenda likizo hujisahaulisha na vurugu hizi. Lakini wengine huamua kubadili ama kuacha kazi kabisa. Hatua hizo mbili zinaweza kuwa ni za muda mfupi tu. likizo hatimaye huisha na mtu hurejea kazini au kule anakoenda baada ya kuacha sehemu ya awali, anaweza kupambana na kero kubwa na nyingi zaidi.

Nijuavyo mimi, kuna mambo ambayo mtu akiyafanya, vurugu na tafrani hizi za makazini haziwezi kumdhuru, bila kuhama au kwenda likizo.

Mambo haya akiyafanya atahisi amani ya nafsi, utulivu wa mawazo na kufurahia kazi au kufurahia maisha hata nje ya eneo la kazi. Haya ni mambo ambayo katika hatua za awali, mtu anaweza asifanikiwe, hata baada ya kufanya. Lakini kwa kujizoeza tena na tena atapatwa na mshangao kugundua yanafanya kazi.


Kama watu wa kazini kwako au pengine popote wanazungumza kwa kufoka au mkabala wa kukosa adabu na upendo, unaweza kujikuta unawaiga. Kama ni kufoka nawe utafoka, kama ni kutukana nawe utatukana na kama ni ubishi utabishana pia. Hii husaidia kuongeza tatizo na kuchokoza na kuchochea hisia.



Badala ya kufanya hivyo, unashauriwa kuwa mtulivu, uzungumze na kutenda kwa amani na upendo. Kwa kufanya hivyo, bila ya wao kujua, watajikuta wakiiga tabia zako. Bila kujali nafasi yako kazini, utaona wengine wakikutazama kama dira, kwa mfano na kama mwanga.

Kila siku kabla hujafika au kuingia kwenye eneo lako la kazi, jitahidi kusema kwa kurudia maneno haya ‘mawazo ni yenye utulivu mkubwa kwa siku nzima ya leo. Namwaga utulivu ambao umenizunguka. Nazungumza kwa amani, utiifu na tabasamu. Nachagua kutenda kwa amani na upendo.’ Yaseme haya ukiwa umedhamiria na hisia zako zikiamini hivyo.

Jaribu kusalimia kila unayekutana naye hapo kazini. Kila unapojihisi kuwa umekerwa, vuta pumzi kwa upole na kwa kina kiasi mara tatu hivi, kabla hujaamua au kusema lolote.


Unapaswa kutambua pia maneno unayoyasema au kuyaandika. Hii ina maana kwamba, kabla hujaandika au kusema jambo, uwe unajiuliza kwanza. Kila linalotoka mdomoni mwako au mkononi mwako(Kuandika) liwe limepata kibali chako baada ya kulitafakari na kuona halitasababisha madhara kwako au kwa wengine.

Usizungumze kwa sauti ya juu sana au ya chini sana wala usikubai kuchotwa na mtu anayefoka, nawe ukaanza kufoka. Wacha anayefoka afoke huku ukijua wazi kwamba, anajiumiza bure, huku wewe ukiwa huna haja ya kujiumiza. Kumbuka kwamba, kufoka ni kujitetea kwa sauti kuliko mantiki. Usikubali kuwa dhaifu wa kiwango hicho.

Jaribu kutafuta muda, tuseme wakati wa mapumziko la mchana. Tafuta mahali palipotulia, kaa hapo na kujaribu kupeleka mawazo yako kwenye eneo lenye mandhari inayopendeza. Yapeleke hapo, yakae kwa muda wa kutosha. Kama siyo mandhari, basi kumbuka tukio lolote huko nyuma ambalo liliwahi kukufurahisha sana. Liweke mawazoni mwako kwa muda wa kutosha.

Jaribu kuweka mawazo yako yote kwenye kile unachokifanya kwa wakati huo. Hii itakuwezesha kutokuingiza mawazo yenye kukera kwenye mfumo wako wa kufikiri.

Badala ya kupoteza muda na nguvu kwa kujiuliza sababu za watu kufanya mambo fulani dhidi yako au kuhusu tabia usizozipenda kwa baadhi ya watu, ni botra kuweka nguvu na mawazo yako kwenye namna utakavyoweza kuboresha vitendo vyako.

Kabla hujazungumza na mtu anayekukera au unayemwogopa ama pengine usiyempenda, pumua polepole kwa kina, ukivuta pumzi ndani na kuzitoa nje, kiasi cha mara tatu na tengeneza picha kwenye mawazo yako, ukijiona kuwa mnazungumza kwa amani na upendo na mtu huyo.

Kwa kufanya haya na baadhi yake utamudu kukabiliana na watu na mazingira ambayo hayakuridhishi kazini kwako au hata nyumbani na kwenye mkusanyiko wa watu ambao unapaswa kuwa nao.

Tunakutakia kila la kheri katika safari yako ya mafanikio, endelea kutembelea DIRA YA MAFANIKIO kujifunza zaidi kila siku.

DAIMA TUPO PAMOJA MPAKA MAISHA YAKO YAIMARIKE,

IMANI NGWANGWALU,
0713 048035,





May 28, 2015

Badili Maisha Yako Kwa Kuwekeza Kwenye Kilimo Hiki Cha Vitunguu Saumu.

No comments :
Kitunguu saumu ni moja kati ya zao bora lenye manufaa mengi kwa matumizi ya kila siku kwa maisha ya mwanadamu, kiafya, Kitabibu na kwa ajili ya kutengeneza au kuchanganyia katika dawa tofauti. Pia ni kiungo mahusui katika mambo ya mapishi.

Zipo aina tisa za vitunguu swaumu ambazo hulimwa hapa
duniani katika maeneo mbalimbali.

Aina za vitunguu saumu maalufu kwa matumizi ya kawaida ni tatu,

1. SOFT NECK - ni nyeupe huzaa kwa muda mfupi.

2. SILVER SKIN - vina rangi ya silver vikikaushwa vinaweza kukaa hadi mwaka mmoja.

3. ANTICHOKE - vina rangi nyekundu kwa mbali.

katika nchi yetu ya tanzania vinapatikana vitunguu swaumu ya aina tatu

 1. Kitunguu saumu chenye mafuta makali.

2. Kitunguu saumu chenye madini ya protini

3. kitunguu saumu chenye madini, protini na mafuta mepesi.
Hiki ndicho tulacho kila siku hapa kwetu na wengi hutumia kama dawa wakati hakina sifa za kuwa dawa.


NAMNA YA KULIMA
Kitunguu hiki hulimwa katika maeneo yenye baridi uwanda wa jua hafifu, mvua za wastani na joto hafifu, aridhi iwe nyeusi yenye rutuba na mfinyanzi, kusiwe na upepo mkali au ukungu mwingi.

Hulimwa kwa kuandaa kitaluna kupandikizwa baada ya miche kufikia urefu wa inchi 6-14, hupandwa kwa mstari na mche hadi mche ni nchi 3-4 na mstari kwa mstari ni nchi 12.

Kwa kifupi kitunguu swaumu ni kati ya zao gumu sana kulilima kwani hustawi katika maeneo machache sana hapa duniani. Kwa hapa tanzania hustawi katika mkoa wa manyara wilaya ya Mbulu, Hanang na babati kidogo, pia kidogo mkoa wa kilimanjaro na kwa eneo lolote ambalo hali inaendana na maeneo tajwa hapo juu.
kwa morogoro vinalimwa maeneo ya mgeta.

UANDAAJI WA SHAMBA

Tifua udongo kidogo kisha ufanye hallowing ili kurahisisha upandaji na ukaaji wa mimea tu. Tengeneza tuta za mita 1 hadi 1.5, upana mita 10 urefu. Kwa upande wa mbolea Inashauliwa utumie WINNER

UPANDIKIZAJI

Vibanguliwe vipandwe kwa kuelekezea mizizi chini na kina cha wastani 2.5 inchi, mbolea ya samadi hushauriwa zaidi kutumika, Huvunwa baada ya miezi 4 -6 kulingana na hali ya hewa na aina ya mbegu iliyotumika.

SPACING/ MUACHANO WA MBEGU NA MBEGU


Mstari hadi mstari ni inchi 8 na mmea hadi mmea ni inchi 6 yaani  (8*6)inchi

KIWANGO CHA MBEGU
Kiwango cha mbegu ni kilo 200 - 300 kwa heka moja

MAVUNO
 Ni tani 5 -6 kwa heka moja

UANDAAJI WA MBEGU
Kitunguu swaumu hupandwa "BULB" na  sio mbegu kama vitunguu maji. Ni ile Punje ambayo Imekuwa na kukomaa vizuri na isyoathiliwa na magonjwa

MAGONJWA
1. Vitunguu saumu havishambuliwi na magonjwa kama ilivyo mazao mengine.
2. Mimea ikianza kutoa maua, yaache yawe marefu hadi yajikunje kisha utayakata ili kuongeza uzalishaji.
Wadudu wasumbufu ni THRIPS na ukungu upande wa magojwa.
Kwa upande wa ukungu anza na  RIDOMILL GOLD upulizie mara nne kisha malizia na score kwa ajili ya Thrips tumia ACTARA au MATCH.

Hushambuliwa na magonjwa kuanzia wiki ya Tatu hadi ya saba, Tumia madwa ya kupuliza yatumikayo kwa nyanya na vitunguu vya kawaida.

SOKO
Kwa kariakoo kilo moja ni kati ya TSH 4000 hadi 6000. Ila kwa ujumla ni bidhaa ambayo inahitajika kwa wingi ndani na nje ya nchi.

Tunakutakia kila la kheri katika safari yako ya kilimo bora.
MAKALA HII IMEANDALIWA NA SAID MALOGO, MTAALAMU WA MASUALA YA KILIMO.


MAWASILIANO 0782 396 729

May 27, 2015

Huu Ndiyo Uamuzi Unaotakiwa Kuufanya, Ili Kubadilisha Maisha Yako Kabisa.

No comments :
Ni kitu ambacho huwa kinanitokea mara kwa mara  hasa pale ninapokuwa katika mazungumzo na baadhi ya jamaa zangu wakijaribu kuzungumzia jinsi hali ya maisha ilivyokuwa ngumu. Ni maelezo hayo hayo ambayo huwa ninakutana nayo nikiwa mtaani na maeneo mengine mengi, ambayo yamekuwa kama wimbo na kusababisha wengi kuamini kuwa hali zao ni ngumu na hawana uwezo wa kubadilisha maisha yao tena.

Na hivi karibuni niliweza kupokea ujumbe kwa njia ya barua pepe kutoka kwa moja ya wasomaji wetu wa mtandao huu wa DIRA YA MAFANIKIO, akijaribu kunieleza kitu kama hicho ambacho wengi wanacho na kinawapa changamoto kubwa katika maisha yao kwa ujumla.

Ni maisha hayo hayo ambayo wamekuwa nayo Watanzania wenzangu wengi wakiamini hali zao ni ngumu sana  na haziwezi kubadilishwa kwa namna yeyote ile. Wengi wamekuwa wakiamini zaidi vitu vingi ambavyo viko nje ya wao kama mfumo mbaya ama uchumi mbovu ndiyo umewakwamisha na kuwafikisha hapo walipo.


Kama umekuwa ukiishi katika fikra hizo na kuamini kabisa kuwa upo katika hali ngumu sana, unachotakiwa kufanya sasa ni kubadilisha mawazo yako hayo mara moja. Kila kitu kinawezekana kwako, hakuna kisichowezekana hata iweje. Unachotakiwa kufanya wewe ni  kuamka pengine kwenye usingizi uliolala wa kutokutambua kuwa hata wewe unaweza kufanikiwa tena kwa viwango vya juu.



Huna haja tena ya kuamini kuwa huwezi ama kulaumu sana. Uwezo na nguvu kubwa ya kubadilisha maisha yako unayo. Wewe ndiye mwenye uwezo wa kubadilisha matokeo ya  maisha yako kulingana na maamuzi unayofanya kila siku na kila mara katika maisha yako. Acha kujiaminisha sana vitu unavyoweza kuvibadilisha. Unao uwezo wa kugeuza matokeo ya maisha yako bila ubishi.

Hata kama imesemwa sana na ikafika mahali na wewe ukaamini kuwa wewe  ni maskini, huo sio mwisho wa mafanikio yako eti tu kwa sababu ya kauli hizo, nasema tena huo sio mwisho wa mafanikio yako. hata kama una hali ngumu sana na familia uliyotoka haijiwezi kabisa, lakini hata hivyo bado ninayo sababu ya kukwambia unaweza kutoka huko na kuwa tajiri wa kesho na unayeheshimika.

Utaweza kutoka huko, ikiwa wewe leo hii utaamua kubadili jambo moja  tu.  Kwa kubadili jambo hilo utakuwa umemudu kuweza kubadilisha maisha yote kabisa. Na jambo ambalo unatakiwa ulibadili kwa haraka sana ili kuweza kuishi maisha ya mafanikio ni namna wewe unavyowaza juu ya umaskini ulionao. Huu ndiyo uamuzi unaotakiwa kuufanya ili kubadilisha maisha yako kabisa.

Mabadiliko makubwa ya maisha yako yanategemea jinsi unavyowaza. Kama utaendelea kuwaza kuwa huwezi na ni maskini wa kutupwa ndivyo itakavyokuwa. Leo hii upo hapo ulivyo kutokana na matokeo ya mawazo uliyokuwa nayo hapo awali. Kwa kufanya uuamuzi wa kubadilisha fikra zako utakuwa umefanya uamuzi ambao utabadilisha maisha yako kwa sehemu kubwa sana.


Kumbuka kuwa, fikra ulizonazo  zinakuwa zinakupa mtazamo wa aina fulani iwe hasi ama chanya. Kama mtazamo ulionao unakuwa ni hasi na ukabaki nao kwa muda mrefu, hatimaye hujitokeza katika maneno na matendo. Kwa mtu mwenye mtazamo chanya na anayewaza mafanikio katika maisha yake, ni kawaida kumkuta akizungumzia mafanikio na hata matendo yake yatadhihirisha hilo pia.

Kwa hiyo, mawazo aliyonayo mtu juu ya maisha yake huweza kudhihirika kwa urahisi katika maneno yake. Unapoona mtu amekata tamaa juu ya maisha yake na kuamua kuishi maisha ya kimaskini, chanzo au asili yake ni mawazo yake. Msaada mkubwa anaotakiwa kupata mtu huyu ni kuweza kufanya uamuzi wa kubadili mawazo yake jinsi anavyo uwazia huo umaskini.  

Hivyo ninaweza kusema kuwa, umaskini na utajiri ni suala linalohusisha mawazo zaidi kuliko kuwa au kutokuwa nacho. Kama ukitaka kubadilisha hali ngumu ya maisha uliyonayo, kitu cha kwanza unachotakiwa kushughulika nacho ni mawazo uliyonayo. Na utakuwa na mawazo chanya ikiwa utachukua jukumu la kujifunza kila siku na kukaa na watu wenye mtazamo chanya juu ya maisha. Huu ndio uamuzi utakaoweza kubadilisha maisha yako kabisa.

Tunakutakia kila la kheri katika safari yako ya mafanikio, endelea kutembelea DIRA YA MAFANIKIO kujifunza zaidi kila siku.

DAIMA TUPO PAMOJA MPAKA MAISHA YAKO YAIMARIKE,
IMANI NGWANGWALU,
0713 048035,



  

May 26, 2015

Mambo 6 Ya Kukusaidia Kutengeneza Biashara Itakayokupa Faida Kubwa.

1 comment :
Ili uweze kufanikiwa vizuri katika biashara yako, kwenye kipindi hiki chenye ushindani wa kila namna,  unahitaji kuwa mipango imara na utaratibu mzuri utakaoweza kufanya biashara yako ikasimama kwa muda mrefu bila kuteteleka. Watu wengi huwa wana mawazo ya kufikiri kuwa wana uwezo wa kutengeneza pesa na faida kubwa mara moja katika biashara zao  kwa kuwa wana mtaji na uwezo wa kufungua biashara wanao.

Kwa mawazo hayo, huwa yakiwapoteza wengi kutokana na ukweli kwamba mambo mengi yamebadilika kwenye biashara kwa sasa tofauti na siku za nyuma. Kitendo cha wewe kuwa na mtaji mkubwa siyo kipimo cha mwisho cha kukuhakikishia ni lazima biashara yako itatoa faida kubwa kama unavyofikiri. Yapo mabadiliko na mambo ya lazima ambayo unatakiwa uyafanye ili kuweza kutengeneza pesa za kutosha na si mtaji pekee tu.

Wapo watu ambao walianza na mitaji mikubwa katika biashara zao lakini hawakuweza kuona matokeo makubwa kama walivyofikiri. Na pia wapo watu walianza na mitaji midogo waliweza kufanya vizuri na kupata faida kubwa sana. Ninachotaka kukuonyesha hapa ni ujue  kuwa yapo mambo ya ziada unayotakiwa uyajue mbali na mataji ili ufanikiwe.  Lakini, sio nia yangu kukuonyesha uzuri ama ubaya wa mtaji mdogo au mkubwa katika biashara yako.

Kwa kuweza kujua mambo hayo itakusaidia hatua kwa hatua, kujenga biashara itakayoweza kukupa faida. Watu wenye mafanikio makubwa kibiashara,  moja ya siri kubwa wanayoitumia katika biasha zao ni kufanyia kazi mambo hayo kila siku. Hiki ndicho kitu tunachotaka ujue leo hapa kupitia makala hii. Ni mambo gani yatakayoweza kukusaidia kutengeneza biashara itakayokupa faida kubwa na endelevu?

Haya Ndiyo Mambo 6 Ya Kukusaidia Kutengeneza Biashara Itakayokupa Faida Kubwa.

1. Kuwa mbunifu.
Ipo nguvu kubwa sana ya kimafanikio ikiwa utakuwa mbunifu katika biashara yako. Bila kuwa na ubunifu wowote ule muhimu katika bishara yako, elewa utaachwa nyuma sana. Kwa kuwa mbunifu itakusaidia kujua ni wapi ulipo na uboreshe biashara yako eneo lipi ili uweze kushinda nguvu ya ushindani.

Kwa kadri unavyozidi kuwa mbinifu ndivyo mafanikio makubwa yanazidi kuwa upande wako. Biashara yoyote ile yenye mafanikio makubwa, ndani yake huwa ina ubunifu. Hili ni jambo mojawapo muhimu sana litakalokuwezesha kukusaidia kutengeneza biashara itakayokupa faida kubwa, ikiwa utalizingatia.



2. Kuwa tayari kwa ushindani.
Hiki ndicho kitu ambacho hutakiwi kukiogopa hasa linapokuja suala ushindani katika biashara. Kikubwa unachotakiwa kujua hapa ni hao washindani wako wanafanya nini cha ziada tofauti na wewe, ili nawe uweze kujifunza na ikiwezekana ufanye kama wao na pengine kuzidi zaidi ya hapo walipo. Kwa kufanya hivyo itakusidia kukabiliana na ushindani na kufikia malengo yako.

3. Kuwa na utaratibu wa kuweka kumbukumbu.
Karibu wafanyabishara wote wenye mafanikio makubwa huwa wana utaratibu wa kuweka kumbukumbu katika biashara zao. Kwa kuweka kumbukumbu muhimu itakusaidia sana kujua ni wapi ambapo unakumbana na changamoto na pia kujua ni eneo lipi unalopaswa kuliboresha zaidi. Hii ndiyo siri mojawapo unayoweza kuitumia kutengeneza faida katika biashara yako.


4. Kuwa tayari kujitoa mhanga.
Katika kipindi ambacho ndio kwanza biashara yako inaanza, ili kufanya biashara yako ikue kwa kasi unalazimika kujitoa mhanga ama kuchua ‘Risk’. Hii ndio njia muhimu itakayoweza kukuza biashara yako. Kuna wakati utalazimika kufanya kazi zaidi kuweza kujifunza hata kwa wengine ili kuona matokeo unayoyataka yawe kwako. Bila kujitoa mhanga juu ya biashara yako utachelewa kufika kule unakotaka kufika.

5. Kuwa mvumilivu.
Kuna wakati  mambo yanaweza yakawa mabaya na yakakuendea kinyume na ulivyotarajia, lakini kuwa mvumilivu. Hii ni nguzo muhimu kwako ambayo unatakiwa kujishikilia bila kuachia mpaka ufanikiwe. Matatizo yoyote yatakayo kupata kwenye biashara yako siyo mwisho wa mafanikio. Jifunze juu ya changamoto hizo na kisha chukua hatua ya kuendelea mbele zaidi. Vinginevyo, ukikata tamaa, utakuwa umejikwamisha wewe mwenyewe.

6. Kuwa tayari kutoa huduma bora.
Hii naweza kusema ndio funga kazi. Ukiweza kutoa huduma bora itakayoweza kukidhi matakwa ya mteja ujue tayari umefanikiwa katika biashara yako. Nasema hivyo kwa sababu, suala la kutoa huduma bora kwa wengi ni tatizo kubwa sana. Unaweza ukafanya uchunguzi mdogo tu, utaelewa ukweli zaidi wa hili ninalosema. Acha kufanya biashara ilimradi ufanye tu, jifunze kutoa huduma nzuri itakayomvuta mteja aje tena kwako kesho.


Tambua  kuwa, kuanzisha na kuendesha biashara itakayokupa mafanikio makubwa unahitaji kujua mambo hayo muhimu, lakini zaidi kuwa na nidhamu binafsi na king’ang’azi mpaka upate matokeo chanya. Kinyume cha hapo, hakuna mafanikio yanayokuja kama ndoto ni muhimu na lazima sana kujitoa.

Tunakutakia kila la kheri katika safari yako ya mafanikio, endelea kutembelea DIRA YA MAFANIKIO kujifunza zaidi kila siku.

DAIMA TUPO PAMOJA MPAKA MAISHA YAKO YAIMARIKE,

IMANI NGWANGWALU,
0713 048035,

May 23, 2015

Hivi Ndivyo Tunavyowaalika Watu Wabaya Katika Maisha Yetu.

No comments :
Nikupe siri moja? Kwamba, wataalamu hivi sasa wamegundua kwamba, asilimia 95 ya muda wote, ambapo sisi binadamu hutendewa ubaya na wengine, ni sisi ambao tunakuwa tumewaalika watu hao kututendea hivyo bila kujua.

Kila kitu tunachofanya, hasa vile vitendo ambavyo havihusishi kuzungumza, ni mwaliko kwa watu wanaotuzunguka . Kutabasamu kwa mfano ni mwaliko. Hii ni kama ilivyo kuweka ndita, kuonesha huzuni usoni, kuonesha hasira usoni au kuwa na uso wenye kuonesha dhati ya mambo muda wote. Hii yote ni mialiko pia.

Mtu anasimama vipi, anatembea na kukaa vipi, na yenyewe pia ni mialiko tosha, tofauti na tunavyofahamu sisi. Hebu siku moja ukiwa kwenye mkusanyiko wa watu, jaribu kuwatazama watu hao mmoja mmoja na kujiuliza, kila mmoja kati yao anawaalika watu wengine kumtendea vipi. Halafu jiulize, watu hao wanatendewa kwa namna wanavyowaalika watu kuwatendea?Jibu kwa asililmia 95 litakuwa, ‘ndiyo’ kubwa kabisa.


Ukitaka kumwalika mtu akutendee ubaya, fanya kwa njia yenye kuvuta ubaya huo. Kukunja ndita kunafanya watu wengine kuogopa kuwa karibu nawe, hata kama huna nia mbaya nao. Kutabasamu huwakaribisha watu wenye kupenda urafiki kuwa karibu nawe. Lakini kwa kufanya kinyume na hapo, hivyo ndivyo utakavyozidi kuwaalika watu wabaya katika maisha yako.


Kubinua midomo kwa dharau huweza kuwaleta kwako watu ambao mtakwaruzana nao kwa sababu, tayari wamekuhukumu hata kabla hawajakufahamu. Aliyesaidia kuwafanya wakuhukumu ni wewe mwenyewe. Kwa hiyo, kama ni kuwaalika ni wewe mwenyewe unayefanya hivyo. Waalike wale ambao ni wema basi, badala ya kuwaalika watakaokuumiza kihisia.

Hebu tazama namna watu wanaotembea wakiwa wamejiinamia na wamejipinda wanavyoishi. Mara nyingi ukichunguza maisha yao utagundua kwamba, yana kuonewa na hofu, kutokujiamini na mashaka. Kutembea kwao kinaaonyesha kile kinachokwenda kwenye ma
wazo yao. Ni rahisi watu wa namna hii kuweza kuonewa tena na tena.


Kama hutaki kuishi kwa mashaka, ni lazima uwakimbie watu wanaoweza kukufanya uingie kwenye maisha ya mashaka. Huwezi kukimbia kama wewe mwenyewe unaishi kimashaka. Kama unataka maisha yasiyo na ushirikina ndani, ni lazima uwakimbie watu wanaohusudu ushirikina. Kwa kukimbia, ni wewe kutokuwa sehemu ya ushirikina wowote.

Kwa kuwa sasa unajua kwamba, mara nyingi kama siyo zote, sisi wenyewe ndiyo ambao tunaowaalika watu na kutufanyia ubaya au wema, ni uchaguzi wetu. Tunatakiwa kujiweka kwenye mazingira ambayo yatawavuta watu wema kwetu, kama tunataka amani. Kama tunataka shari, tunaweza kujiweka kwenye njia ambayo tutawavuta wakorofi kuwa karibu nasi zaidi.

Tunakutakia kila la kheri katika safari yako ya mafanikio, endelea kutembelea DIRA YA MAFANIKIO kwa elimu na maarifa bora yatakayoboresha maisha yako.

DAIMA TUPO PAMOJA MPAKA MAISHA YAKO YAIMARIKE.

IMANI NGWANGWALU,
0713 048035,


May 22, 2015

Unahitaji Kitu Hiki Cha Ziada Ili Uwe Na Mafanikio Makubwa Unayohitaji.

No comments :
Daktari mmoja maarufu sana duniani na hasa kwa nchi za joto kama kwetu, anaitwa Ronald Rose. Daktari huyu alifanya utafiti mkubwa na wa miaka mingi kule nchini India kuhusiana na malaria. Wakati anafanya utafiti huu mgumu, bila shaka kulikuwa hakujagunduliwa hasa chanzo cha malaria. Kwa hiyo, unaweza kufikiria kuhusu mtu, ambaye anaanza kutafuta chanzo cha tatizo akiwa hana msaada wa tafiti za kutosha za kabla. Bila shaka ilikuwa ni kazi ngumu sana kwake.

Daktari huyu alifanyia utafiti huu kwenye mazingira magumu sana ya kimaskini. Alikuwa akifanyia kazi yake kwenye maabara ambayo mchana ilimlazimu lazima atumia pangaboi ili kujinga na joto kali sana la India. Lakini pangaboi hilohilo likawa linapeperusha mbu ambao alikuwa akiwatafiti. Basi, ikawa ni shida kubwa sana ya afanye kipi na aache kipi. Hiyo haitoshi usiku kulikuwa na baridi sana na usumbufu mkubwa wa mbu.

Najua utasema, angejikinga kwa mbu kwa kufanya hivi au vile ni sawa. Utakuwa unasema hivyo kwa kuzingatia zaidi mazingira ya siku hizi. Kwa wakati ule, mbu alikuwa hajabainika kuwa adui wa maradhi na hivyo hakukuwa na njia rasmi za kujikinga naye. Akiwa na matumaini ya kugundua na kuthibitisha kwamba, mbu ndiye anayeeneza malaria, alifanya kazi kwa nguvu zake zote. Lakini hata baaada ya kuwafanyia utafiti mbu kwa maelfu, alikuwa hajahisi hata kwamba, angeweza kupata jibu.
  
Kila mbu alikuwa anachukua zaidi ya saa mbili kufanyiwa utafiti. Kwa maelfu ya mbu, ilikuwa na maana ya siku nyingi za kazi ngumu isiyolipa. Bado, alikuwa na haja ya kujaribu tena na tena na siyo kwa sababu analipwa chochote, hapana. Alikuwa anafanya kwa sababu, alitaka kufanya kilichomleta duniani, kugundua kitu kitakachosaidia wengine. Kumbuka muda wowote kwake ungeonekana mrefu sana , kwa sababu ya shida mbalimbali kama zilizotajwa.


Pamoja na shida zote hizo, mbaya zaidi wahindi ambao ndiyo waliokuwa wanaathiriwa sana na mbu kuliko watu wengine wowote duniani wakati ule, hawakuwa wema kwake. Walikuwa wakijazana kumwangalia wakati akiwanyia utafiti mbu hao na walimbeza sana. Walikuwa wanamcheka, wanamwita kichaa na wengine walisema ni mchawi. Hivyo, hata maisha yake yalikuwa hatarini pia kutokana na mazingira ya kigeni aliyokuwa akifanyia kazi hayakuwa rafiki kwake.

Hapa angeweza kusema, ‘nimtoka kwetu kuja kuchunguza kinachouwa watu hawa, halafu wao wananibeza,’ halafu angenawa mikono nakurudi kwao ulaya. Hakufanya hivyo, badala yake, aliwapuuza na kuendelea na utafiti wake. Lengo lake halikuwa sifa, bali kuchangia kwenye maisha ya binadamu wengine. Aliendelea na hatimaye alihisi kuanza kukata tamaa. Alifikia hatua hiyo, baada ya siku moja kukamata aina mpya ya mbu nakujiambia, ‘huyu atatoa jibu.’ Lakini kwa bahati mbaya, wala hakutoa kitu hata kinachokaribia jibu.

Alipokosa kupata kile alichotarajia kwenye mbu huyu, alijiinamia na kujiuliza, ni kwa nini imeshindikana? Wakati anajiuliza hivyo, msaidizi wake alikuja na aina nyingine ya mbu wapya. Dk. Ronald alitaka kumwambia msaidizi wake Yule awaachie mbu hao waende zao, kwa sababu alijua mbu wote wapya wasingempa jibu, hakukuwa na jibu. Lakini alibadili mawazo yake ghafla na kumwambia msaidizi wake ampe mbu wale.

Akiwa amechoka na kazi nzito ya siku nyingi isiyo na majibu anayoyataka alianza kuwafanyia utafiti mbu wale mmoja baada ya mwingine. Akiwa amebaki mbu mmoja, alikuwa hajapata jibu na alijua angelazimika kufunga virago kurudi kwao, baada ya miaka mingi ya ‘kusota’. Alimchukua mbu wa mwisho na kuanza kumfanyia utafiti. Halafu alishindwa kuamini, mbu yule alitoa jibu alilokuwa amelitafuta kwa miaka mingi kwa shida na mateso.  Aligundua chanzo cha ugonjwa wa malaria. Alimgundua maikrobu, aliye mwenezi wa malaria.

Ni kitu gani kinachotokea tunapokuwa watu wanaoweza kwa vitendo kuvuta subira na kuwa na imani kubwa kwa yale tunayoyatenda? Bila shaka ni mafanikio mwishoni kabisa. Kupitia maisha aliyoishi Dk. Ronald tunajifunza mengi kuhusu maisha yetu ya mafanikio. Tunaonyeshwa kuwa mafanikio yanahitaji uvumilivu, subira ya kutosha lakini zaidi ili uweze kufanikiwa unahitaji unapofanya jambo lolote uwe na uhakika unalipenda jambo hilo kwanza, hiki ndicho kitu cha ziada unachohitaji ili kuwa na mafannikio makubwa.

Kupenda tunachofanya ni sifa muhimu sana kwetu, kuliko ujuzi wetu au fedha zetu tulizonazo.  Dk. Ronald alidhamiria na akasema, kuna siku nitagundua, kuna siku nitapata jibu ninalotafuta. Alifanikiwa kupata jibu kweli. Ndani ya kero, shida, kebehi na dharau, hatimaye ikawezekana. Lakini kubwa la kujifunza ni hili. Mtu anapofika mahali anajikuta anaanza kukata tamaa kwenye kile anachokifanya, inabidi ujue kwamba, huenda upo karibu kufikia mafanikio unayoyataka.

Ni kama Dk. Ronald alipokuwa amefikia mahali ambapo alikuwa amejiandaa kusema, ‘sasa kinachofuata ni kufunga virago.’ Lakini kabla hajaweka chini vifaa jibu likaja. Hii yote inaonyesha ni kwa jinsi gani hatutakiwi kukata tamaa hata mambo yawe magumu vipi kwetu, tunatakiwa kuwa wavumilivu. Unaweza ukajikuta biashara uliyokuwa ukiitegemea kuwa italipa sana haikupi faida uliyokuwa ukitaka hicho nacho ni kipindi cha kutokata tama kama ambavyo Dk. Ronald hakuweza kukata tamaa.

Kwa kuwa umeamua kuwa mjasiriamali kuwa na roho ya paka usikubali kufa au kushindwa kiurahisi, hata watu wakutukane ama wakupigie kelele vipi, wewe ziba masikio kisha songa mbele na amini kile unachofanya ndio kipo sahihi. Acha kuyumbishwa na kitu chochote katika maisha yako kuwa na msimamo wako utakaousimamia. Kumbuka, usipokuwa na msimamo juu ya maisha yako huwezi kufanikisha kitu utakuwa unayumbishwa tu kama bendera.

Uwezo wa kutoka hapo ulipo unao, jipe moyo, kuwa na subira na mvumilivu katika kipindi unachotafuta mafanikio, zaidi penda kile unachokifanya hapo utakuwa upo kwenye mstari sahihi wa mafanikio.

Nakutakia mafanikio mema, karibu katika mtandao huu wa DIRA YA MAFANIKIO uendelee kupata maarifa bora yatakayokutoa kwenye umaskini, kwa pamoja tunaweza.

DAIMA TUPO PAMOJA MPAKA MAISHA YAKO YAIMARIKE,

IMANI NGWANGWALU,




May 21, 2015

Tabia 4 Muhimu Za Kimafanikio Unazotakiwa Kuzijua.

No comments :
Mara nyingi watu wenye mafanikio huwa wana tabia za aina fulani ambazo huwa wanazifuata kila siku na hatimaye kuweza kutimiza ndoto na malengo yao waliyojiwekea. Kwa kuzifuata na kung’ang’ania tabia hizi, hujikuta ni watu wa mafanikio zaidi katika mambo wanayoyafanya na maisha kwa ujumla.
 
Kwa kawaida, ili uweze kufikia viwango bora vya mafanikio unayoyahitaji, kitu cha muhimu kwako unachotakiwa kufanya ni kujenga tabia za kimafanikio. Unapokuwa na tabia za kimafanikio zinakuwa zinakusaidia kukufikisha kwenye viwango fulani vya mafanikio uliyojiwekea.

Kitu cha kujiuliza hapa ni wangapi wanaojua tabia hizi za kimafanikio zinaweza kuwa msaada kwao?. Ukweli ni kwamba wengi hawajui katika hili na kutokujua huko hupelekea kubeba tabia ambazo huwa ni kikwazo kikubwa sana cha mafanikio katika maisha yao.

Hivyo basi, ni muhimu kwako kuwa na tabia za kimafanikio zitakazo kusaidia kutimiza malengo yako. Acha kupoteza muda kwa kubeba tabia ambazo ni mzigo kwako na hazikusaidii sana, zaidi ya kupoteza muda. Je, ni tabia zipi za kimafanikio ambazo unatakiwa kuzijua ili kufanikiwa zaidi?

Hizi Ndizo Tabia 4 Za Kimafanikio Unazotakiwa Kuzijua.

1. Tabia ya kuweka vipaumbele.
Watu wenye mafanikio, daima huwa ni watu wa kuweka vipaumbele katika maisha yao. Huwa ni watu ambao hawakosei na kwenda kinyume na suala zima la kuweka vipaumbele. Mara nyingi huwa ni watu wa kukaa chini na kufanya uchaguzi sahihi  kwa kitu muhimu kuliko vyote na kukifanyia kazi.

Kwa kuwa na tabia hii peke yake, ni nguzo muhimu kwako kukufikisha kwenye mafanikio. Ili kuweza kufanikiwa inabidi kujifunza juu ya kuweka vipaumbele katika maisha yako. Kama utakuwa unataka kufanya kila kitu na kukosa vipaumbele, elewa kabisa itakuwa ngumu kwako kuweza kufanikiwa.




2. Tabia ya kuwa na mitazamo chanya.
Ni muhimu sana kuwa na matazamo chanya kwa kila unachokifanya katika maisha yako ili uweze kufanikiwa. Unatakiwa kila mara kuulisha ubongo wako vitu chanya vitakavyokujenga siku hadi siku, na hatimaye kuwa bora zaidi. Hii ni tabia muhimu na ya lazima kwako kuwa nayo ili kujenga ,mafanikio makubwa.

Unapokuwa na mtazamo chanya hata pale inapotokea umekwama katika kile unachokifanya inakuwa ni rahisi kwako kuvuka. Watu wengi wenye mafanikio ni watu wenye mitazamo chanya na ndicho kitu kinachowasukuma zaidi kuweza kufanikiwa. Kama nia yako ni kujenga mafanikio ya kudumu, jifunze kuanzia sasa kuwa na mtazamo chanya.


3. Tabia ya kuweka nguvu za uzingativu pamoja.
Kati ya kitu kimojawapo muhimu unachotakiwa kujifunza katika maisha yako ni kuweka nguvu za uzingativu sana kwa jambo unalolifanya. Moja kati ya kosa kubwa ambalo watu wengi wanalifanya katika maisha yao ni kuzingatia ama kutilia mkazo katika mambo ambayo hayana umuhimu sana katika maisha yao.

Kama utaendelea kuweka makazo katika mambo ambayo hayakusaidii itakuwa ni vigumu kwako kufanikiwa. Zingatia zaidi mambo ambayo yanakusaidia, utapata matokeo chanya na ya haraka sana. Hii ni tabia mojawapo ya kimafanikio unayatakiwa kuijua na kuifanyia kazi katika maisha yako, ili kusonga mbele zaidi.


4. Tabia ya kuanza jambo na kulimaliza.
Kuwa na uwezo wa kuanza jambo na kulimaliza ni siri mojawapo muhimu ya mafanikio kwako. Wapo watu ambao huwa ni wepesi sana wa kuanza jambo lakini huwa hawamalizii. Unapokuwa unaanza jambo na kushindwa kumalizia, hicho ni kitu hatari sana katika safari yako ya mafanikio.

Ili uweze kufanikiwa, unatakiwa ujijengee tabia ya kuanza jambo na kuhakikisha umelimaliza mpaka mwisho. Watu wengi wenye mafanikio hichi ndicho kitu wanachokifanya. Ukija kuchunguza kidogo tu, utagundua wengi wanaoshindwa katika maisha huwa hawamalizi mambo yao.

Kiuhalisia, mafanikio yoyote huwa hayaji kwa bahati kama wengi wanavyofikiri. Mafanikio huwa yanajengwa kwa vitu vidogovidogo kama vile tabia na mienendo yetu ya kila siku. Kwa kulijua hilo tunatakiwa kuwa makini na tabia zetu na kujenga tabia za kimafanikio zaidi. Kwa kifupi, hizo ndizo tabia za kimafanikio unazotakiwa kuzijua ili kufanikiwa.

Tunakutakia kila la kheri katika safari yako ya mafanikio, endelea kutembelea DIRA YA MAFANIKIO kujifunza na kuboresha maisha yako.

DAIMA TUPO PAMOJA MPAKA MAISHA YAKO YAIMARIKE,

IMANI NGWANGWALU,
0713 048035,

May 20, 2015

Huu Ndiyo Ufugaji Rahisi Kwako, Unaoweza Kukutoa Kwenye Umaskini.

No comments :
Ufugaji ni kazi ambayo wengi huiona kama kazi ya watu wanaoshi mashambani,na kwamba haina faida. Lakini je wajua kuna ufugaji ambao huhitaji nafasi kubwa, ila mazao yake ni ya mapato ya juu. Si mwingine ila ufugaji wa kware. Fuatana nasi katika makala hii ya leo  katika matandao huu wa DIRA YA MAFANIKIO kuona faida muhimu za kiafya na kipato kama ukiamua kuanzisha ufugaji huu utakaokufanya uwe na kila sababu ya kutabasamu endapo utaujua vizuri.
 
Ufugaji wa kware ni njia bora na rahisi sana kwa mfugaji yeyote aliyetayari kukuza kipato chake kwa haraka sana na kwa kiwango cha juu.

Kware ni jamii ya ndege ambao kwa sasa wanafugwa majumbani na wanaotaga mayai kama kuku ama bata na kwa wingi sana. Ndege hawa ni wadogo 280gm - 300gm, Wanarangi ya brown, nyeusi au hata nyeupe yenye miraba na madoa ya rangi ya ugondo au kijivu. Manyoya yao pia yana rangi ya brown au nyeupe na yenye madoa yanayovutia. 

Kutaga na kuatamia

Kware dume humpanda jike kwa muda kidogo, Hapo jike anakuwa tayari kutaga na hutaga mayai 290 hadi 310 kwa mwaka (hii hulingana na lishe nzuri atakayopatiwa).
Mayai ya Kware huatamiwa kwa siku 18 na huanza kuanguliwa vifaranga kwa muda wa siku 2, kuanzia siku ya 18 na hadi 20.
Njia bora ya kutotolesha mayai ya Kware ni kwa kutumia incubator ambapo mayai huatamiwa kwa wingi ndani ya siku 18.

Utunzaji wa vifaranga na chakula

Siku 1 – 7
Vifaranga wapatiwe chakula “STARTER PELLET” na maji masafi ya kutosha. Siku ya 1 wawekee ‘GLUCOSE’ kwenye maji, Packet moja kwa lita 20 za maji, na siku ya pili hadi ya tano wawekee Amin Total kwenye maji, Wape maji pekee siku ya sita na siku ya saba wapatie chanjo ya Newcastle. Utawapatia joto kwa njia ya umeme kwa ‘BULB’ mbili (2) za 200watts kwa kila vifaranga 300, ama unaweza kuweka taa ya ‘Energy Server’ pamoja na jiko la mkaa uliofunikwa na majivu ambao utakidhi kuwapatia joto sawia kwa masaa 24 kwa siku 7. (Majivu yanasaidia moto kukaa kwa muda mrefu)




Banda/box lako liwe la ukubwa wa 1.5m x 1.5m (au eneo la ukubwa huo ndani mwa banda kubwa la kufugia kuku) lazima uzingatie usalama wa vifaranga dhidi ya panya, paka au vicheche. Unatakiwa kuweka ‘magazeti au mabox’ chini kwenye sakafu yatakayosaidia usafi. Kwa week ya kwanza chakula kitawekwa chini na tunashauri utumie chakula cha pellet ili kusaidia vifaranga wasiteleze na kuathiri miguu. 
NOTE: Weka goroli au mawe kwenye drinkers zako ili kuzuia vifaranga wasizame ndani ya (drinkers) maji na kufa.


Siku 8-14
Vifaranga wataendelea kupewa chakula “STARTER PELLET” na maji safi. Wataendelea kuhitaji ‘mwanga’ wa kutosha muda wote na joto la wastani bulb 2 za watts 100 au moja ya watts 200 

Siku 15-21
Uhitaji wa joto utapungua, ila ni kipindi ambacho wanakula chakula zaidi kwa ajili ya kukua. Ni vizuri waendelee kupata taa ili kupata mwangaza utakayowawezesha kula mchana na usiku.

Siku 21 na Kuendelea
Kware wako hawatahitaji joto tena wawekee taa tu za energy server kipindi cha usiku, wape chakula na maji ya kutosha zaidi kwa ajili ya kukua. 

UTAGAJI MAYAI
WEEK YA SITA
Wiki ya sita kuelekea ya saba Kware wako wataanza kutaga mayai kila siku, kwa wastani Kware mmoja hutaga mayai 300 kwa mwaka. 

Magonjwa

Kware ni ndege wenye kinga kubwa na ni vigumu sana kushambuliwa na magonjwa kama kuku na mara wanapougua ni rahisi sana kutibika. Magonjwa yanayoweza kuwapata Kware ni typhoid, mafua na kuharisha .

Tiba za asili
Waweza kuwatibu vifaranga au Kware wako kwa kutumia njia ya asili ambayo pia ni rahisi, gharama nafuu na bora zaidi kuliko kutumia madawa yaliyochanganywa na kemikali na yenye gharama.
Vifuatazo ni vitu vya asili vinavyotumika kutibu magonjwa mbali mbali kwa Kware na yanayopatikana kwa wingi katika maeneo ya mfugaji. Madawa haya hutumika kwa kiwango cha wastani na hayana kipimo maalum kwani hata ukiyazidisha hayana madhara.

 Mwarobaini na Aloe Vera: Madawa haya hutumika kutibu kuharisha damu pamoja na mafua kwa vifaranga vya Kware. Chukua kiasi kidogo cha mwarubaini kisha twanga vizuri kupata maji maji. Kamua maji yale, kisha weka katika maji uliyoandaa kuwanywesha vifaranga wako. Kata vipande vidogovidogo vya aloe vera (jani moja laweza kutosha) na tia katika maji yaliyochanganywa na mwarobaini, kisha wapatie vifaranga wanywe (Aloe Vera itaendelea kujikamua yenyewe ikiwa ndani ya maji huku vifaranga wakiendele kunywa).

Kitunguu swaumu: Hii hutumika kukinga na kutibu vifaranga vya Kware wanaosumbuliwa na kuharisha damu. Unachukua kitunguu swaumu na kuondoa maganda ya nje kisha kusafisha na kukata vipande vidogo sana, na kuwawekea kama chakula. Vifaranga wanapenda sana vitunguu hivyo na watakula kwa kasi kama chakula lakini ni tiba tayari. Unaweza kuwapatia kila siku hadi watakapo pona.

Maziwa:Maziwa yanayotokana na ng’ombe pia hutumika kutibu ugonjwa wa kuhara pamoja na kuwapa nguvu Kware waliolegea. Mnyweshwe maziwa hayo Kware anayeumwa bila kuyachemsha na umnyweshe maziwa ya kutosha kiasi cha kushiba. Unamnywesha mara tatu kwa siku. Hakikisha maziwa unayotumia yanatoka kwa ng’ombe wanaotibiwa kila mara.


Angalizo
Siyo lazima Kware waugue ndipo uwapatie tiba hizi. Hakikisha unawapa tiba kabla hata hawajaugua hivyo utawakinga na magonjwa hayo. Waweza kuchanganya madawa hayo yote kwa wakati mmoja kwani hayana madhara.

Endapo madawa ya asili hayapatikani katika eneo la mfugaji basi waweza kuwatibu Kware kwa madawa yafuatayo ambapo vipimo huelezwa moja kwa moja kwa maandishi katika madawa hayo au kuelezwa na muuzaji pale utakaponunulia; Amprolium kwa ugonjwa wa kuharisha damu (Coccidiosis), Fluban,Coridix au Doxyco kutibu mafua (Coryza) na Esb3,Trisulmycine au Trimazine hutumika kwa homa ya matumbo (Typhoid). 


Chanjo

Siku ya 7 lazima vifaranga wapatiwe chanjo ya “kideri/mdondo
(respiratory & digestive diseases) kwa dawa inayoitwa ‘newcastle’. Chanzo cha maambukizi ni maji na chakula kilichochafuliwa na kinyesi na pia husababishwa na virusi kwa njia ya hewa.

Siku ya 14 lazima wapewe chanjo ya “gumboro”. Chanzo cha
maambukizi ni maji na chakula kilichochafuliwa na kinyesi na pia husababishwa na virusi kwa njia ya hewa.

Siku ya 21 lazima warudie chanjo ya “Newcastle (aina ya IBDL)”. Chanzo cha maambukizi ni maji na chakula kilichochafuliwa na kinyesi na pia husababishwa na virusi kwa njia ya hewa.

Siku ya 35 lazima wapate chanjo ya “Ndui”.

Soko
Mayai ya Kware ni bidhaa adimu sana hapa nchini kwa kuwa ni wafugaji wachache waliojikita katika ufugaji huu, Ufuatao ni muhtasari wa wastani wa bei ya bidhaa za Kware sokoni 

1.   Trei ya (mayai 30) ya KWALE inauzwa shilingi 30,000 .
2.   Kifaranga wa Kware wa siku moja anauzwa shilingi 2500 – 3000
3.   Kware wa week 4 (mwezi mmoja) anauzwa kwa shilingi 10,000– 12,000
4.   Kware aliyeanza kutotoa (week 6) huuzwa shillingi 20,000 – 25,000
5.   Kware kwa aliyekomaa kwa ajili ya kitoweo huuzwa kwa shilingi 25,000
6.   DROPING za Kware huuzwa kwa shilingi 10,000 kwa 50kg kwa wafugaji wa samaki
Soko la KWALE liko juu sana kwa mayai na nyama. KWALE pia hutofautiana bei kwa jike na dume.
Mayai yake pia huuzwa kwa bei nzuri sana. Yai moja huuzwa kuanzia 8,000 hadi 12,000 kwa wakati wowote ule.

TUNAKUTAKIA KILA LA KHERI KATIKA UFUGAJI BORA,

KWA MAWASILIANO JUU YA UFUGAJI WA KWARE TEMBELEA