google-site-verification: googleabbfd1327a3af7a3.html

DIRA YA MAFANIKIO

Badili maisha yako sasa kwa kuwa na fikra sahihi.

Kujifunza zaidi juu ya maisha na mafanikio, nakualika kwenye kundi la whats app kujifunza kwa kina. Tututumie ujumbe kwa njia ya whats app kwenda 0687449428 kupata utaratibu wa kujiunga.

Sep 30, 2015

Mambo 12 Yakujifunza Kutoka Kwa Watu Waliofanikiwa.

No comments :
Ipo haja kubwa sana ya kujifunza kupitia watu waliofanikiwa ili kuweza kufikia mafanikio mkubwa. Kupitia maisha yao kuna mambo mengi ya msingi tunakuwa tunajifunza na kuachana na makosa ambayo wao waliyafanya bila kujua.
Na kiuhalisia yapo mambo mengi ya kujifunza kutoka kwa watu waliofanikiwa ambayo yanaweza kuwa msingi mkubwa wa mafanikio yetu. Kuyajua mambo hayo itakusaidia kujiamini na kuendelea mbele. Mambo hayo ya kujifunza kutoka kwa watu waliofanikiwa ni kama haya yafuatayo:-
1. Watu waliofaniwa ni watu wa kutegemea mafanikio makubwa kutoka ndani mwao na siyo kinyume cha hapo. Ni watu wa kuamini ule uwezo walionao ndani mwao kuwa ndiyo utakao wafanikisha.
2. Watu waliofanikiwa ni watu wa kuishi kwa bajeti. Mara nyingi hujikuta wakikata au kupunguza kile ambacho siyo cha muhimu katika bajeti yao na kutengeneza bajeti upya itakayowafanikisha. Kwa kifupi, matumizi yao kwa sehemu kubwa yanaongozwa na bajeti.
3. Watu waliofanikiwa ni watu wa vitendo. Mara nyingi siyo waongeaji sana. Ni watu wa kuchukua hatua ambazo zinaleta matokeo halisi na chanya yatakayojitokeza kwenye maisha yao.

4. Watu waliofanikiwa wako makini na suala zima la uwekezaji. Kila wakati wanafungua macho yao kuangalia ni wapi ambapo wanaweza kufanya uwekezaji ambao utawaletea matunda na mafanikio makubwa badala ya kukaa na kutumia pesa hizo tu.
5. Watu wenye mafanikio wanatumia muda wao mwingi kujifunza. Kwa kifupi hawa ni watu wa kujifunza kupitia vitabu mbalimbali wanavyovisoma hata pia kuhudhuria semina au warsha za mafanikio.
6. Watu wenye mafanikio ni watu kuendelea mbele hata pale inapotokea wameshindwa katika jambo fulani. Huwa hawasimami kusikilizia sana maumivu hayo. Hujifunza pale walipokosea na kisha safari ya mafanikio kuendelea kama kawaida.
7. Watu wenye mafanikio mara nyingi wanazungukwa na watu wenye mitazamo chanya kama ya kwao. Watu hawa wanaowazunguka huwasaidia zaidi kimtazamo na kuwafanya wawe na mafanikio muda wote.
8. Watu wenye mafanikio hawana kauli za kushindwa kwenye maisha yao. Muda mwingi wamebeba kauli za mafanikio. Hutaweza kuja kuwasikia wakisema ‘siwezi hili, au lile’ badala yake hukaa na kusema ‘nitaweza vipi kufanya jambo hili nakufanikiwa’ hizo ndizo kauli za watu wenye mafanikio siku zote.
9. Watu wenye mafanikio ni watu wa kujitoa mhanga. Siku zote wako tayari kufanya na kutoa chochote ili mradi tu mipango na malengo yao yaweze kutumia na kufika kule wanakotaka kufika.
10. Watu wenye mafanikio ni watu wa kufanya mambo yako kwa kuweka nguvu nyingi za uzingativu katika eneo moja. Kama kuna jambo wameamua kulifanya wanaling’ang’ania hilohilo mpaka liwape matokeo kamili.
11. Watu wenye mafanikio ni watu wa kutunza muda siku zote. Hawako tayari kupoteza muda wao kwa kufatilia mambo ambayo wanaona hayana msaada kwao.
12. Watu wenye mafanikio ni watu wenye uvumilivu wa kutosha. Kuna wakati huwa wanashindwa katika mambo yao, lakini huvumilia mpaka kuweza kufanikiwa.
Yapo mambo mengi sana ambayo unaweza kujifunza kupitia watu waliofanikiwa, lakini unaweza ukayafanyia kazi mambo  hayo kwanza ili yawe msingi bora katika safari yako ya kuelekea kwenye mafanikio makubwa.
Nakutakia kila la kheri katika safari yako ya mafanikio na endelea kutembelea DIRA YAMAFANIKIO kujifunza na kuhamasika.
Ni wako rafiki katika mafanikio,
Imani Ngwangwalu,

Kama una maoni, ushauri au changamoto yoyote inayokuzuia kufikia mafanikio yako wasiliana nami kwa email dirayamafanikio@gmail.com au simu 0713 048035 kwa ushauri na msaada wa haraka. 

Sep 29, 2015

Sababu 8 Kwanini Unatakiwa Kumiliki Biashara Yako Sasa?

No comments :
Inawezekana mara kwa mara umekuwa ukiwaza namna unavyoweza kuanzisha biashara yako na kujenga uhuru wa kifedha. Mawazo hayo umekuwa ukiyapata hasa kutokana na kila ukiangalia unaona kama vile kipato chako hakitoshi kutokana na kazi unayoifanya sasa. Kama hayo ndiyo mawazo yako upo kwenye njia sahihi.
Nikiwa na maana kuwa upo umuhimu mkubwa wa kuanzisha biashara yako mwenyewe kuliko hata unavyofikiri. Kwani mbali na faida ya kifedha yapo mambo mengine mengi utakayojifunza kutokana na kumiliki biashara yako mwenyewe. Je, unajua ni kwa sababu gani unatakiwa kumiliki biashara yako mwenyewe na kuacha kutegemea kuajiriwa kwa asilimia zote ?
Hizi Ndizo  Sababu 8 Kwanini Unatakiwa Kumiliki Biashara Yako Sasa?
1. …Ni njia bora ya kukufikisha kwenye uhuru wa fedha.
Inawezekana ukawa umechoka na kazi unayoifanya na unaoina haifai kwa namna moja au nyingine. Lakini njia bora ya kuweza kuondokana na utumwa huo ambao unakukabili ni kuanzisha biashara yako mwenyewe ambayo utaisimamia mpaka ikuletee mafanikio unayoyahitaji.
2. …Ni Njia bora ya kujifunza.
Hakuna njia bora ya kujifunza kuhusu kutunza na kumiliki pesa kama biashara. Hili ndilo eneo  ambalo utajifunza mengi kuhusu masoko, namna ya kukuza mtaji na jinsi ambavyo unaweza ukaufikia uhuru wa kipesa. Kwa hiyo kama una biashara yako inakusaidia kujifunza yote hayo hatua kwa hatua.

3. …Ni njia bora yakujifunza kujitegemea.
Unapokuwa kwenye ajira kwa kawaida unakuwa unamtegemea mtu fulani ambaye ndiye akuamulie juu ya maisha yako. Lakini kwenye biashara mambo hayako hivyo. Wewe ndiye unakuwa mwamuzi mkubwa wa maisha yako. Na unakuwa unakikisha unafanya kila linalowezeka mpaka biashara yako ifanikiwe.
4. …Inakuwa inakupa hamasa ya mafanikio zaidi.
Huo ndiyo ukweli unaotakiwa ujue kuwa, unapokuwa na biashara inakuwa inakupa hamasa ya kuweza kufanikiwa na kusonga mbele zaidi. Tofauti na ajira ni rahisi kusema kuwa ‘aaah kazi yenyewe siyo yangu kwanza’ kwa hiyo unakuwa unafanya kwa jinsi unavyojisikia. Lakini kwenye biashara mambo hayako hivyo ni lazima kujituma ili kufanikiwa.
5. …Inakuongezea ujasiri.
Unapokuwa mfanyabishara ni hatua nzuri sana kwako ya kukupelekea kuwa na ujasiri wa hali ya juu. Hiyo yote ni kwa sababu unapofanikiwa katika biashara moja unakuwa ndani yako una hamasa kubwa ya kutaka kufanya biashara nyingine tena kwa mafanikio. Kwa hali hiyo unakuwa una maamuzi mengi ya kijasiri ambayo ni rahisi kukusaidia kukusonga mbele.
6. …Ni njia rahisi ya kufuata mipango na malengo yako.
Mara unapoanzisha biashara yako unakuwa upo kwenye njia sahihi ya kufuata ndoto za maisha yako. Hii yote ni kwa sababu unakuwa unakifanya kile kitu ambacho unakipenda kwa dhati toka moyoni mwako. Wakati unapokuwa kwenye ajira unakuwa unafanya tu ilimradi mkono uende kinywani. Hiyo ndiyo faida kubwa mojawapo ya kuwa kwenye biashara.
7. …Inakufanya unakuwa ni mtu wa vitendo.
Watu wengi mara nyingi ni waongeaji bila ya kuwa watu wa vitendo. Lakini kitendo cha kuwa na biashara yako mwenyewe inakupelekea unakuwa ni mtu wa vitendo. Utaelewa vizuri umuhimu wa kuchukua hatua katika biashara tofauti na ambavyo ungekuwa hufanyi biashara ingekupelekea wewe kuwa na maneno mengi bila utekelezaji.
8. …Ni njia bora ya kufanya mambo mengine zaidi.
Unapokuwa kwenye biashara inakuwa ni njia bora ya kufanya mambo mengine bora zaidi. Kama ulikuwa una lengo moja na umelikamilisha inakuwa ni rahisi kuweza kulifatilia lengo lingine mpaka tena kulifanikisha. Na hiyo nguvu yote ya kufanya mambo mengine inakuja kutokana na ujasiri ambao tayari unakuwa umeshajijengea kwenye biashara yako.
Kama ulikuwa ni mtu wa kusubiri subiri, achana na hiyo habari. Wakati wa kumiliki biashara yako ni sasa, ili iweze kukupa mafanikio mkubwa na endelevu.
Nakutakia kila la kheri maendeleo ya biashara yako na endelea kutembelea DIRA YA MAFANIKIO kujifunza na kuhamasika.
Ni wako rafiki katika mafanikio,
Imani Ngwangwalu,
dirayamafanikio@gmail.com

Sep 28, 2015

Kama Unataka Kuwa Na Furaha Ya Kweli, Zingatia Mambo Haya.

No comments :
Kila mmoja kati yetu anatamani sana kuwa na furaha ya kweli maishani mwake. Nina uhakika kama furaha ingekuwa inauzwa, mfanyabishara wake ndiye mtu ambaye angekuwa tajiri zaidi duniani. Asingekuwa tajiri tu, bali angekuwa tajiri wa kufuru.
Kwa nini? kwa sababu, kila binadamu anatamani kuwa na furaha ya kweli kwenye maisha yake. Kila mmoja wetu, awe anajua au awe hajui, anachotafuta hapa duniani ni furaha tu. Kuhangaika kwetu kote, ni kutafuta furaha ya kweli.
Lakini kwa bahati mbaya wengi wetu hatujui namna ya kuipata furaha ya kweli. Wengi tumekuwa tukifanya mambo ambayo tunafikiri yanaweza kutupa furaha, lakini baada ya muda tunagundua mambo hayo hayatupi furaha ya kweli tunayoihitaji kama tulivyokuwa tukifikiri.
Kwa mujibu wa wataalamu wa masuala ya utambuzi wanadai kuwa kutafuta furaha ya kweli maishani, kunahitaji juhudi na kila mmoja anaweza kuipata furaha hiyo kama kweli ataamua. Wanasema, kimsingi furaha ni ujuzi ambao inabidi mtu ajifunze kuupata.
Na ili kuliweka jambo hili wazi, na kueleweka kwa kila mtu hadi kumudu kupata furaha ya kweli, wataalamu hawa wautambuzi wameweka mambo au vigezo vya kuzingatia ili kuweza kujijengea furaha ya kweli. Kwa kuyajua mambo hayo yanauwezesha ubongo wako kufanya mabadiliko ya kukupa furaha ya kweli.

Moja ya sababu au nguzo ya kukupa furaha ya kweli ni kufanya tahajudi (Meditation) au sala za uzingativu kwa muda mrefu. Watu wengi  wanaofanya aina fulani za tahajudi au meditation huweza kumudu kuongeza furaha katika maisha yao kwa kiwango fulani.
Hiyo huweza kutokea hivyo kwa sababu, kwa kadri mtu anavyofanya sala au tahajudi hupelekea kwa nguvu nyingi hasi kukandamizwa katika ubongo wake na matokeo yake nguvu chanya kuongezeka na kupelekea kumudu kujenga furaha ya kweli anayoitaka kwake. Hivyo tahajudi ni jambo la muhimu sana katika kujenga furaha halisi.
Pili, furaha ya kweli inakuja kwa kutambua kuwa inatoka ndani mwako na siyo vinginevyo. Hii ina maana kwamba, haiwezekani kwa mtu kupata furaha ya kweli kama ndani yake mtu huyo hajikubali na haioni furaha hiyo kwake.
Wengi wanategemea mambo ya nje kama fedha, elimu au umaarufu  kupata furaha. Lakini kitu cha kushangaza hawaipati furaha hiyo, hata kama wakiipata inakuwa ni ya muda mfupi sana na kutoweka.
Wakati mwingine hata furaha ya muda mfupi hawawezi kuipata , kwani kwa mfano, mara wanapopata fedha nyingi, sekunde hiyohiyo mawazo yenye kukera na hofu kuhusu fedha hizo huanza kujitokeza kwao na mwisho hujikuta furaha yao ikiyeyuka.
Kwa kulitambua hilo usiwe mtumwa kwa mambo hayo ya nje ambayo yanaweza yakatoweka muda wowote na kukupotezea furaha yako. Kitu cha msingi tambua wewe ndiye chanzo cha huzuni au furaha katika maisha yako.
Tatu, jifunze kuyachukulia mambo kama yanavyokuja ili kujijengea furaha ya kweli. Acha kushindana sana  baadhi ya hali zinazokuja kwako, kwani utashindwa kuzimudu hali hizo na mwisho wa siku utajikuta unakosa ile furaha halisi. Usiwe mtu wa kubadilika asubuhi na jioni kwa kutegemea kitu gani kinaendelea nje.
Mtu mwenye furaha ya kweli anakubaliana na maisha kama yalivyo bila kujali kama kuna mvua au jua, kama mambo yameenda vizuri au vibaya, kama kuna fedha au hakuna, kama kuna kusifiwa au hakuna. Tunasema ni watu ambao ndani zao hazitegemei sana ni kati gani kinaendelea nje.
Nne, unaweza upata furaha ya kweli kama utaamua kuwapenda wengine pia.  Kuwapenda wengine ina maana kuwapokea na kuwakubali watu wengine kama walivyo na mapungufu yao. Hili huwa ni jambo gumu kwa wengi kuwapenda watu wengine.
Kama nilivyosema awali, kila binadamu anataka kupata furaha maishani. Katika kutafuta furaha binadamu hujikuta akitafuta kazi nzuri, gari nzuri ya kutembelea, kujenga nyumba nzuri, kuoa au kuolewa na mke au mume mzuri na mengine mengi, yote hayo hufanywa kwa ajili ya kutafuta furaha.
Kwa sababu, furaha haiko kwenye mambo hayo tu, watu hujikuta wanapata vitu hivyo, lakini bado hawana furaha. Kwa sasa itakuwa ni rahisi sana kwa binadamu kupata furaha ya kweli kama ataamua na kuzingatia mambo hayo tuliyojadili, badala tu ya kuhangaika kutafuta mara hiki mara kile.
Nakutakia kila la kheri katika safari yako ya mafanikio na endelea kutembelea DIRA YAMAFANIKIO kujifunza na kuhamasika.
Ni wako rafiki katika mafanikio,
Imani Ngwangwalu,
Kama una maoni, ushauri au changamoto yoyote inayokuzuia kufikia mafanikio yako wasiliana nami kwa email dirayamafanikio@gmail.com au simu 0713 048035 kwa ushauri na msaada wa haraka.


Sep 25, 2015

Jinsi Ambavyo Unavyoweza Kuitumia Dakika Moja Kubadili Maisha Yako.

No comments :
Inaweza ikawa ni kitu cha kushangaza kidogo kwako, lakini huu ndiyo ukweli, unao uwezo wa kutumia dakika moja tu kubadili maisha yako. Kama wewe ni mtu wa visingizio kila wakati mara ‘oooh mimi sina muda’ utachelewa na utaacha mipango yako mingi ipotee bure.  Dakika moja ni ya thamani kubwa kwako na inakutosha kufanya uamuzi wa msingi utakao kuletea mabadiliko kwenye maisha yako.
Ni rahisi kusema haiwezekani, lakini inawezekana. Unawezaje kufanya mabadiliko hayo kwa kutumia dakika moja ili kubadili maisha yako na wengine pia? Kumbuka tu kwamba:-
1. Inakuchukua dakika moja tu, kuchukua uamuzi wa kutafakari kile unachokwenda kukifanya katika siku yako ya leo.
2. Inachukua dakika moja tu, kuchukua uamuzi wa kufanikiwa au kushindwa katika maisha yako.
3. Inachukua dakika moja tu, kuamua kujenga hofu ama kujimini katika maisha yako katika kila jambo unalotaka kulifanya katika maisha yako.
4. Inachukua dakika moja tu, kumwambia mtu aliyekata tamaa kuwa ni lazima atafanikiwa.

5. Inachukua dakika moja tu, kusema mwenyewe kuwa basi nimeshindwa kwa kile ninachokifanya au nitaendelea kung’ang’ania mpaka nipate matokeo ninayoyahitaji.
6. Inachukua dakika moja tu, kumwonyesha upendo mtu yule ambaye anajihisi mpweke.
7. Inachukua dakika moja tu, kuamua kuwa wewe ndiye kiongozi pekee wa maisha yako.
8. Inachukua dakika moja tu,  kuamua kuishi maisha ya kuwaumiza wengine au kuwa msaada kwao.
9. Inachukua dakika moja tu, kuamua kuwa utabadilika na kuwa na tabia za mafanikio au utaendelea na maisha yako uliyonayo sasa.
10. Inachukua dakika moja tu, kujikubali kuwa wewe ni mshindi na hakuna kitu kinachoshindikana kwako na kwa uamuzi huo ni lazima ufanikiwe.
Kitu cha kujiuliza hapa, je unaitumia vipi dakika uliyonayo ili uweze kukufanikisha kufikia mafanikio makubwa unayoyahitaji? Kumbuka dakika moja tu inaweza kukufanikisha au kukufanya ukashindwa kwenye maisha yako kutokana na kile unachokiamua ndani ya dakika hiyo.
Watu wengi wameharibu maisha yao kutokana na maamuzi madogo madogo wanayoyafanya kwa dakika hiyo moja. Kwa mfano kama umefanya maamuzi mabaya kwa dakika sitini, tafsiri yake ni kwamba umeharibu maisha yako mara sitini. Kuwa makini na dakika yako moja na itumie vizuri ikufanikishe.
Nakutakia kila la kheri katika safari yako ya mafanikio na endelea kutembelea DIRA YAMAFANIKIO kujifunza na kuhamasika.
Ni wako rafiki katika mafanikio,
 Imani Ngwangwalu,
Kama una maoni, ushauri au changamoto yoyote inayokuzuia kufikia mafanikio yako wasiliana nami kwa email dirayamafanikio@gmail.com au simu 0713 048035 kwa ushauri na msaada wa haraka.



Sep 24, 2015

Faida 7 Za kufanya Mazoezi Ya mwili.

No comments :
Kuwa na afya bora ni msingi wa mafanikio yote. Hata uwe na mipango na malengo mazuri vipi lakini kama afya yako ni mbovu huwezi kuyafikia mafanikio hayo unayoyataka. Unapokuwa na afya bora inakuwa inakupa nguvu ya kuishi maisha bora wakati wote na kufanya mambo mengi bila kuteteleka.
Kama ambavyo waswahili wanasema ‘mwili haujengwi kwa matofali’ ndivyo hivyo afya hii tunayaoizungumzia haiji kwa bahati mbaya tu. Mara nyingi vyakula tunavyokula na aina ya maisha tunayoyaishi karibu kila siku ndiyo inayotuamulia afya zetu ziweje kwa sasa na baadae
Kama unaishi maisha ya kulakula hovyo tu bila utaratibu kamwe usitegemee ikawa rahisi kujenga afya bora ni lazima itakusumbua. Vilevile hata kama hujihusishi na mazoezi nayo pia itakuwa ni tatizo kwa afya yako. Ili ufanikiwe ni muhimu kutambua kitu cha kwanza kukilinda ni afya kuliko kitu chochote kile.
Kwa hiyo utakuja kuona kuwa chakula bora chenye virutubisho vyote muhimu, ni kitu cha lazima na msingi sana kwa afya zetu. Lakini mbali vyakula hivyo pia tunaona hata mazoezi yanahusika pia katika kutupa afya zetu kwa kiasi kikubwa kuliko wengi tunavyofikiri.
Wengi huwa tunaona mazoezi ya mwili yanafanyika lakini huwa hatujui yanafanya kazi gani hasa kwenye hii miili yetu. Mara nyingi zipo faida nyingi za kufanya mazoezi ambazo siyo rahisi kuzitambua ikiwa hujafanya uchunguzi hata kidogo. Faida hizo ni kama hizi zifuatazo:-

1. Mazoezi ya mwili husaidia kulirekebisha shinikizo la damu.
2. Mazoezi ya mwili huiruhusu damu nyingi zaidi kuzifikia sehemu zote za mwili na kuifanya mikono na miguu ipate joto.
3. Mazoezi ya mwili yanaondoa mambo yote mawili. Yaani mkazo wa mwili na mfadhaiko wa moyo, na kukusiadia wewe kujisikia vizuri zaidi katika maisha yako. Mazoezi ya mwili kwa kawaida ni tiba bora kabisa ya wasiwasi na msongo (stress).
4. Mazoezi ya mwili hutupatia nguvu ya umeme kwa ajili ya ubongo wetu pamoja na seli za neva. Yanaongeza afya kwa kuuamsha mfumo wa kinga mwilini (immune system). Mwili unapowekwa katika hali ya afya kwa kufanya mazoezi yanayofaa. Ubongo unakuwa na uwezo wa kufikiri kwa ubunifu na ufanisi zaidi.
5. Yanaweza kukusaidia kuiweka vizuri rangi ya uso wako na kukuweka katika hali nzuri kabisa kimwili. 
6. Mazoezi ya mwili hukufanya uwe na nguvu nyingi zaidi, hivyo kuchelewesha kupatwa na uchovu kimwili na kimawazo 
7. Yanausaidia ubongo wako kutengeneza dawa inayokupa wewe hali ya kujisikia vizuri na kukuongezea uwezo wa kustahimili maumivu.
Endapo wewe ulikuwa hufanyi mazoezi, basi anza taratibu (polepole) na kuongeza nguvu yake hatua kwa hatua upatapo uwezo wa kustahimili.
Nakutakia kila la kheri katika maendeleo ya afya na endelea kutembelea DIRA YA MAFANIKIO kujifunza na kuhamasika.
Ni wako rafiki katika mafanikio,
 Imani Ngwangwalu,
Kama una maoni, ushauri au changamoto yoyote inayokuzuia kufikia mafanikio yako wasiliana nami kwa email dirayamafanikio@gmail.com au simu 0713 048035 kwa ushauri na msaada wa haraka.



Sep 23, 2015

Kama Unakimbia Kitu Hiki, Huwezi Kufanikiwa.

No comments :
Kwa hakika ‘Hakuna kisichowezekana chini ya jua’ ikiwa nia hiyo ya kufanikiwa unayo kweli kutoka moyoni mwako. Kila kitu unachokihitaji katika maisha yako kinapatikana ikiwa utaamua kufanya kwa kazi kwa bidii. Haijalishi hali au rasilimali ulizonazo lakini kama wewe ni mtu wa kufanya kazi kwa bidii zote huku ukiwa na mipango na malengo imara  ni lazima ufanikiwe.
Watu  wote wenye mafanikio makubwa duniani kote ni wachapakazi. Mafanikio yao yote ni matokeo ya kile walichokifanyia kazi kwa muda mrefu bila kuchoka. Na pengine kazi hizo walizokuwa wakizifanya ziliwachosha, kuwakatisha tamaa lakini kutokana na uvumilivu wao walivumilia na kuendelea kujishughulisha mpaka malengo yao yakatimia.
Nakumbuka katika maisha yake Daktari Ronald Rose kama ambavyo tuliwahi kuandika wakati fulani katika mtandao huu, alifanya kazi kwa bidii sana ili kukamilisha ugunduzi wake wa dawa ya malaria. Mbaya zaidi mazingira aliyokuwa akifanyia kazi hayakumpa ushirikiano wowote lakini aliweka  juhudi mpaka dawa ya malaria ilipatikana bila kuchoka.
Hiyo yote inatuonyesha uvumilivu na kufanya kazi kwa bidii ni vitu ambavyo havikwepeki ili kufikia mafanikio makubwa. Ikiwa nia yako ni kutafuta mafanikio ya kweli ni lazima ujue kazi inahitajika tena ya ubora wa juu  na wala sio ‘hadithi’  za hapa na pale. Achana na habari za sterehe zisizo na msingi kwako.  Jitume ili kufikia uhuru wa kifedha, vinginevyo utaendelea kuwa na maisha magumu mpaka mwisho wako.

Tatizo kubwa la watanzania tulio wengi ni kukwepa majukumu ya kufanya kazi kwa bidii. Kama unafikiri natania jaribu kuangalia  hata wale wote waliokaribu na wewe,  utagundua ni wengi wenye uvivu fulani fulani hivi hata kwenye kazi zao. Kazi zinakuwa zinafanyika ila kwa kujivuta sana hali ambayo hupelekea majukumu mengi kukwama.
Ili uweze kufanikiwa na kufikia viwango vya juu vya mafanikio kitu kikubwa ambacho hutakiwi kukwepa ni kufanya kazi kwa bidii.  Kama kwenye maisha yako hufanyi kazi kwa bidii, sahau kuhusu mafanikio. Jaribu kuchunguza wale wote wanaofanikiwa sana katika jamii yako ni watu wa aina gani? Utakuja kugundua ni wale wote wanaojituma kila siku bila kuchoka katika kazi zao.
Kama kanuni au maisha yako hivi kwa nini unataka kujidanganya na kuamua kutafuta urahisi unaojua wewe? Kumbuka, kama unakimbia kitu hiki kwa namna moja au nyingine huwezi kufanikiwa. Kila kitu ili uweze kukipata kina gharama yake. Na gharama mojawapo ya mafanikio hadi uweze kuyafikia ni kujitoa na kufanya kazi kwa bidii.
Najua kila mmoja wetu ana nia ya kufanikiwa katika mambo yake iwe katika biashara au maeneo mengine. Lakini mafanikio hayo hayawezi kuja kama ndoto tu. Yatapatikana kwa kufanya kitu kimoja tu ambacho ni kufanya kazi kwa bidii. Hapo ndipo ilipo siri ya kufikia mafanikio makubwa na hakuna muujiza katika hilo.
Kama wahenga walivyosema ‘kazi ni msingi wa maendeleo’ hakuna ubishi katika hilo. Penda kile unachokifanya, weka juhudi na nguvu zako zote bila kuchoka na mafanikio yatakuja upande wako. Haijalishi mazingira uliyopo ni magumu kiasi gani lakini kitu cha muhimu kwako ni kujituma tu mpaka uone hatma ya mafanikio yako.
Kwa makala nyingine nzuri hakikisha unaendelea kutembelea DIRA YA MAFANIKIO kujifunza zaidi.
Ni wako rafiki katika mafanikio,
 Imani Ngwangwalu,
Kama una maoni, ushauri au changamoto yoyote inayokuzuia kufikia mafanikio yako wasiliana nami kwa email dirayamafanikio@gmail.com au simu 0713 048035 kwa ushauri na msaada wa haraka.  





Sep 22, 2015

Jinsi Unavyoweza Kuwavuta Watu Unaokutana Nao.

No comments :
Kwa nguvu zake Mungu naamini umzima wa afya na unaendelea kujifunza kupitia DIRA YAMAFANIKIO ili kuboresha maisha yako. Leo napenda nianze makala hii kwa kukuuliza swali hili, ni kwa nini baadhi ya watu, wakikutana na mtu kwa mara ya kwanza tu, mtu huyo waliyekutana naye ‘anaboreka’ haraka? Na ni kwa nini wengine, wanapokelewa kirahisi na watu wapya wanaokutana nao maishani?
Najua, unajua kuna sababu nyingi. Lakini ningependa nikutajie moja tu, ili iweze kukusaidia kukabiliana na ‘kuwaboa’ watu wengine. Na tumia neno ‘kuboa’ kwa sababu ni neno ambalo limezoeleka kimatumizi kwa sasa, likiwa na maana ya kumfanya mtu asiwe na haja ya kukusikiliza au kuwepo kwako hukera, wewe ukiwa ndiyo chanzo.
Kama umekutana na mtu kwa mara ya kwanza, usizungumze sana kuhusu wewe, usijizungumzie kwa kujisifu na kujipandisha sana. Ingawa haina maana kwamba usijishushe. Usitake kuonesha kwamba wewe ndiye wewe.
Watu wasiojitosha, huwa wanakawaida ya kujisifu sana, wanataka kuwavuta wanaozungumza nao wawaone wa maana sana, huzungumza kwa muda mwingi wao tu, hujisifu na kujikweza. Ni mara chache sana huwaacha wengine waseme.
Hebe fikiria, hujamjua mtu, unasema kama kinanda kuhusu mambo yako, unadhani atakuchukulia vipi? Ni lazima utamkera tu, badala ya kumfurahisha, kama unavyofikiria. Ni lazima utaanza kuwa na wasiwasi nawe.

Jambo la awali unalotakiwa kulifanya unapokutana na mtu mgeni, ambaye hujawahi kukutana naye, iwe kibiashara, kimapenzi au kwa nasibu tu, inabidi uwe msikilizaji tu kuliko kuwa msemaji.
Kuna watu ambao wanatatizo la kutaka kusikilizwa wao tu, amablo chimbuko lake ni kushindwa kwao kupata watu waliowajali walipokuwa wadogo.
Kama nawe ni mmojawapo, inabidi uwe mwepesi kujikumbusha kwamba, una tatizo la kutaka kusikilizwa wewe tu. Kujikumbusha au kukumbuka, kutakusaidia kuamua kumsikiliza mwingine badala ya wewe kusema.
Siku zote wanaopenda kusikiliza badala ya kusema, hao ndiyo mara nyingi huwa wanawavutia watu, siyo wale wanaopenda kusema sana. Wengi hawalijui sana jambo hili.
Ni vizuri unapokutana na mtu mgeni, ukasema kidogo uhusu wewe, yaani yale mambo ya msingi tu yanayokuhusu. Sema tu yale ambayo ni ya lazima au muhimu. Usiwe kasuku kwanza.
Halafu, soma kama huyo mtu ambaye humjui, ndiyo kwanza mnakutana, anavutwa na mazungumzo gani? Unaweza ukaanza kubwata siasa wakati hataki kusikia kabisa mambo yanayohusiana na siasa zako hizo. Unaweza ukaanza kubwata kuhusu vifo, wakati pengine wiki iliyopita tu kapoteza mkewe au mumewe ama mtu wake wa karibu kabisa.
Ukijua mtu au watu wa fulani ambao ndiyo kwanza unakutana nao wanafurahia kuungumzia mambo gani, hutawakera. Kwako itakuwa rahisi pia kuwasikiliza, kwani huenda watakuwa na mengi, kwani wanazungumza yale wanayoyapenda na pengine wanajua zaidi.
Unapokutana na mtu mgeni popote na mazingira yakakulazimisha muwasiliane, siyo vibaya ukaanza kwa kujitambuisha kwa kujitaja jina.
Hii humjengea mtu huyo mwingine kukuamini na kuhisi ukaribu na urafiki.  Onesha kwamba, mtu huyo mgeni anapozungumza unafurahia mazungumzo yake. Unaweza kutabasamu, kumtazama bila kukodolea macho na kutikisa kichwa mara kwa mara.
Hata kama ikitokea mtu huyo anaongea upuuzi, ni vema kujenga uhusiano wa karibu na mtu huyo. Wacha mgeni aseme zaidi ili umjue zaidi kuliko wewe anavyokujua.
Kumjua kwako zaidi kutakusaidia kujua uzungumze vipi naye na kwa sababu zipi. Lakini, usijaribu kuwa mtu ambaye siyo wewe. Kuwa wewe kwa kujikubali, bila kujipandisha wala kujishusha.
Nakutakia kila la kheri katika safari ya mafanikio yako na endelea kutembelea DIRA YA MAFANIKIO kujifunza na kuhamasika.
DAIMA TUPO PAMOJA MPAKA MAISHA YAKO YAIMARIKE,
Ni wako rafiki katika mafanikio,
 Imani Ngwangwalu,
Kama una maoni, ushauri au changamoto yoyote inayokuzuia kufikia mafanikio yako wasiliana nami kwa email dirayamafanikio@gmail.com au simu 0713 048035 kwa ushauri na msaada wa haraka. 

Sep 21, 2015

Siri Nzito Katika Kufikia Mafanikio Makubwa.

No comments :
Katika maisha kila mtu hupenda kufanikiwa na kufikia mafanikio makubwa. Lakini pamoja na umuhimu huo ni wapo ambao hujikuta wakifanya yale yasiyotakiwa kufanywa ili kufikia mafanikio hayo. Mafanikio mazuri ni lazima yaanze na malengo. Bila kujiwekea malengo yatakayokuongoza kwenye mafanikio inakuwa ni kama kazi bure.
Katika mfano mzuri wakukueleza hili na ukanielewa vizuri ningependa leo nikusimulie kisa kimoja cha ndege Tai. Ndege huyu ni moja kati ya ndege aliyefanikiwa kuwa na uwezo mkubwa wa kuruka juu zaidi kuliko ndege wengine wote.  Siku moja mfugaji mmoja katika pitipita zake alibahatika kupata yai la Tai.  Alipofika nyumbani aliamua kuliweka yai lile kwenye mayai ya kuku ili litotolewe.
Ulipita muda wa siku ishirini na moja malengo ya mkulima yule yaliweza kufanikiwa pale yai lile lilipototolewa pamoja na mayai mengine ya kuku. Siku zote utambulisho wa kitu au mtu ni jamii aishiyo. Kuku wale pamoja na tai yule waliweza kuishi pamoja na hata kujita wote wana tabia za aina moja zinazofanana.
Siku moja sasa kuku alikuwa akitafuta chakula kwa ajili ya vifaranga wake.  Tai yule ambaye alikuwa  pamoja na kuku alimuona tai mkubwa akiwa angani na akamuuliza kuku yule ni ndege gani mbona yuko juu sana kuliko sisi? Kuku alimjibu na kusema yule ni tai ndege aliyebarikiwa sana kuliko ndege mwingine.
Tai mdogo hakushia hapo aliendelea kumhoji kuku kwa hiyo sisi hatuwezi kuruka na kuwa kama yeye?  Kuku alimjibu ni kweli hatuwezi sisi ni kuku hatuna uwezo huo. Kwa kuwa tai mdogo alishindwa kujitambua yeye ni nani aliweza kukata tamaa na kuamini kabisa ni kweli hawezi kufanana naye.

Tai yule aliendelea kuishi maisha yaleyale akiwa na kuku hadi siku ya mwisho alijikuta akiwa amekufa bila kutimiza malengo yake. Kitu kikubwa kilichomfanya hadi afe na hali hiyo ya kutokuweza kuruka ni kutokana na yeye kuamini asingeweza kuleta mabadiliko ya kuruka kumbe uwezo huo alikuwa nao tena mkubwa wa kufanya hivyo ingawa yeye hakujua.
Ni mambo gani ya kuweza kujifunza kupitia simulizi hii?
1. Kama unataka kufanya mambo makubwa katika maisha yako, jifunze kuamini fikra zako na kuwa wewe kama wewe. Ukisikiliza sauti nyingi za nje zitakuzuia kufika kule unakotaka kufika. Kwa mfano kama tai yule mdogo angejiamini angeweza kuruka lakini kwa bahati mbaya alikufa huku na uwezo wote akiwa nao. Kilichomkwamisha ni sauti ya kuku. Angalia hata hapo ulipo usije ukakwamishwa na kuku, wewe ni tai.
2. Kila wakati ni lazima kujiandaa na kujifunza kwa ajili ya mafanikio yako. Kama usipojiandaa na kujifunza utakufa na mambo mengi bila ya kuyatumia.
3. Upo umuhimu wa kuachana na mambo ya zamani yanayotushikilia na kutukwamisha. Acha kuaminishwa tena na mtu eti kuwa huwezi wakati uwezo huo unao tena mkubwa sana.
4. Watu wengi wanajikuta wakifa na kwenda makuburini bila kutimiza malengo yao makubwa waliyojiwekea kutokana na kutokuelewa uwezo ulio ndani mwao. Wapo waliokufa wakiwa na vipaji vikubwa vya mziki ndani yao, wengine walikufa wakiwa na vipaji vya mpira na wengine hata vya uandishi lakini kwa bahati mbaya hawakuweza kuvitumia vyote hivyo, kama tu ilivyokuwa kwa tai.
5. Tulizaliwe ili tushinde katika maisha na siyo tushindwe. Acha kujiona mnyonge katika dunia hii, kumbuka wewe ni mshindi na siyo mtu wa kushuindwa kama unavyojiona.
Yapo mengi ya kujifunza kupitia simulizi hiyo, lakini nimekushirikisha kwa sehemu ili kujifunza pamoja. Tafakari juu ya maisha yako na chukua hatua kubwa ya kutumia vipaji ulivyonavyo ndani mwako na kukufanikisha.
Nakutakia kila la kheri katika safari ya mafanikio yako na endelea kutembelea DIRA YA MAFANIKIO kujifunza na kuhamasika.
DAIMA TUPO PAMOJA MPAKA MAISHA YAKO YAIMARIKE,
Ni wako rafiki katika mafanikio,
Imani Ngwangwalu,
Kama una maoni, ushauri au changamoto yoyote inayokuzuia kufikia mafanikio yako wasiliana nami kwa email dirayamafanikio@gmail.com au simu 0713 048035 kwa ushauri na msaada wa haraka.  







Sep 18, 2015

Siri 6 Za Kuishi Maisha Yenye Afya Bora.

No comments :
Habari za siku rafiki  na mpenzi msomaji wa mtandao huu wa DIRA YA MAFANIKIO. Nimatumaini yangu umzima wa afya na unaendelea kujifunza ili kuboresha maisha yako. Karibu tena katika siku nyingine ambapo tunapata fursa ya kujadili mambo ya kimafanikio kama ilivyo kawaida yetu.
Katika makala yetu ya leo tutaangalia kuhusu afya kama sehemu muhimu sana kwa mafanikio yoyote yale. Bila shaka utakubaliana nami kuwa kama afya yako ni mbovu huwezi kufanikiwa hata iweje. Mafanikio yote unayoyatafuta yanahitaji uwe na afya njema ili kuyafikia, vinginevyo utakwama.
Ikumbukwe kuwa hakuna mtu anayependa kuumwa au afya yake kuwa mbovu hata kidogo. Kila mtu anahitaji afya yake iwe bora tena hata siku zote ikiwezekana ili kuishi maisha ya furaha. Lakini ubora huo wa afya tunaoutaka hauji hivihivi tu huwa zipo kanuni au siri za kufanya ili kuweza kujijengea afya bora zaidi.
Hapa zipo siri sita za kufuata endapo wewe kweli unataka kuishi maisha yenye afya na yenye manufaa mengi zaidi.
1. Fanya Mazoezi ya mwili kila siku.
Mazoezi ya mwili ni ya muhimu sana kwa afya yetu na yanafaida nyingi kwetu. Unapofanya mazoezi hiyo inakuwa inakusaidia kuupa mwili afya kutokana na ukweli kwamba yanapunguza magonjwa mengi kama ya msongo wa mawazo na shinikizo la damu. Hivyo unapofanya mazoezi hata kama ni kidogo unakuwa upo katika hali nzuri kiafya tofauti na yule ambaye hafanyi kabisa.

2. Pata muda wa kupumzika
Baada ya kazi zetu tunazozifanya, mwili huu ni lazima upumzike ili upate kujitengeneza upya wenyewe. Yatupasa kuwa na muda wa burudani na wa kupumzika ili kupunguza msongo utokanao na kazi pamoja na majukumu ya kifamilia. Bila kuwa na muda wa kutosha kupumzika mara nyingi watu wanakuwa na wasiwasi, mfadhaiko na hasira kali.  Hivyo ni lazima kutenga muda huu ili kujijengea afya bora.
3. Kula chakula bora.
Ili kujihakikishia usalama wa hili epuka kula vyakula vyenye mafuta mengi. Kama unazidisha vyakula hivi vyenye mafuta hali hiyo inaweza ikawa hatari kwa afya yako. Vyakula hivi vinaweza vikawa nyama au vinginevyo. Hakikiha unajipatia vyakula vyenye virutubisho muhimu vya mwili, lakini siyo lazima viwe vya mafuta. Kwa kujijengea tabia hiyo mwili wako kwa namna yoyote ile ni lazima utakuwa na afya bora.
4. Epuka Vitu Vinavyokuletea Madhara.
Vitu hivi inaweza ikawa ni pamoja na matumizi mbaya ya pombe hususani pombe kali au uvutaji wa sigara wa kupitiliza. Unapokuwa unafanya mambo kama hayo tambua tu moja kwa moja yatakuharibia afya yako. Kitu cha msingi hapo ni kuhakikisha unaachana na tabia hiyo ili kujijengea afya bora na endelevu kwako.
5. Kunywa maji safi na ya kutosha.
Tunapozungumzia afya safi huwezi kulikwepa hili la kunywa maji safi. Unalazimika kunywa maji safi na ya kutosha ili kuipa akili yako nguvu ya kufanya kazi kwa ufanisi. Unapokunywa maji mengi yanakuwa yanasaidia ubongo wako kufanya kazi vizuri kwa sababu yanakuwa yanaiongezea akili yako oksijeni kwa hali ya juu kabisa.
6. Dumisha usafi.
Usafi ni suala la muhimu sana katika kuboresha afya zetu. Usafi huu unaweza ukaanzia kwenye miili yetu, mavazi na hata pia katika mazingira yetu. Tunapoimarisha usafi katika maeneo yote hayo inakuwa ni rahisi kuweza kukabiliana na magonjwa mbalimbali ambayo yangeweza kutushambulia.
Kumbuka,  kuwa na afya bora ni msingi mkubwa wa mafanikio kwa binadamu. Hivyo ni lazima kwetu kudumisha afya bora siku zetu ili kujihakikishia hata usalama wa maisha yetu kwa kiasi kikubwa.
Nakutakia kila la kheri katika maendeleo ya afya yako na endelea kutembelea DIRA YA MAFANIKIO kujifunza na kuhamasika.
DAIMA TUPO PAMOJA MPAKA MAISHA YAKO YAIMARIKE,
Ni wako rafiki katika mafanikio,
 Imani Ngwangwalu,
Kama una maoni, ushauri au changamoto yoyote inayokuzuia kufikia mafanikio yako wasiliana nami kwa email dirayamafanikio@gmail.com au simu 0713 048035 kwa ushauri na msaada wa haraka.  

Sep 17, 2015

Mambo 7 Yakukusaidia Kutunza Muda Wako Vizuri.

No comments :
Matumizi mazuri ya muda ni moja kati ya changamoto kubwa sana inayotukabili wengi wetu. Mara nyingi imekuwa ikitokea kwa wengi wetu karibu kila siku, kujikuta tuna mambo mengi ya kufanya ukilinganisha na muda tulionao. Kutokana na mambo hayo kuwa mengi, mipango yetu mingi pia hujikuta imekwama na kushindwa kuendelea kutokana na ukosefu wa muda.
Lakini hata hivyo, pamoja na changamoto zote hizo za ukosefu wa muda, kwa wengine bado hubaki kuwa ni watu wa kupoteza muda katika maisha yao. Nikiwa na maana kuwa, wanakuwa ni watu ambao hawajali sana kupoteza muda wao na pia hata wanakuwa wanawapotezea wengine muda hivyohivyo. Najua umeshawahi kuwaona watu wa namna hii katika maisha yako wasiojali thamani ya muda.
Hawa ni watu ambao huishi maisha yasiyo na mafanikio sana kutokana na kupoteza muda mwingi sana katika maisha yao. Kitu cha muhimu hapa kujua ni kuwa muda ni kitu cha  thamani sana kuliko kitu chochote duniani. Mafanikio yote yanategemea muda. Unapopoteza muda wako ni sawa na kupoteza mafanikio yako. Sasa jiulize kama wewe unapoteza muda unategemea nini katika maisha yako?
Ili uweze kufanikiwa na kuwa tajiri ni lazima kujifunza kutumia muda wako vizuri tena sana. Watu wote wenye mafanikio makubwa ni watumiaji wazuri wa muda wao kuliko unavyofikiri. Kinachowatofautisha wao na wewe ni matumizi ya muda tu na sio kitu kingine. Hiyo yote inaonyesha siri kubwa ya mafanikio ipo kwenye muda. Kitu kingine cha kujiuliza tena  je, unataka kutunza muda wako na kujijengea mafanikio ya kudumu? Kama jibu ni NDIYO.
Yafuatayo Ni Mambo 7 Yakukusaidia Kutunza Muda Wako Vizuri.
1. Weka vipaumbele vya kila siku.
Ili uweze kuepuka muingiliano wa mambo ni lazima kujifunza kuweka vipaumbele vya kila siku. Andika mambo ya lazima ambayo unatakiwa uyafanye kwa siku hiyo husika bila kuacha kitu. Hilo litakusaidia kutopoteza hovyo muda wako ulionao kwa sababu kila kitu kitakuwa kwenye ratiba yake na muda wa kukifanya.

2. Jiwekee malengo.
Kama utakuwa unajiwekea malengo hiyo itakuwa ni silaha ya kukuwezesha kutumia muda wako vizuri pia. Kwa sababu utakuwa unajua kabisa baada ya muda fulani unatakiwa uwe umetekeleza kitu hiki ama kile. Wengi wanaopoteza muda mara nyingi ni watu ambao hawana malengo hata yale ya siku moja tu. Na kwa sababu hiyo kwao muda kupotea ni kitu ambacho hakikwepeki.
3. Fanya mambo machache kwa uhakika.
Ni rahisi sana kwako kupoteza muda kama utajikuta unataka kafanya mambo mengi kwa wakati mmoja. Hii ni kwa sababu utashika hiki mara kile na kujikuta hakuna ulichokifanya zaidi ya kurukaruka. Ili kufanikiwa jifunze kufanya mambo machache kwanza ikiwezekana jambo moja tu. Hiyo itakupa ufanisi wa kutunza muda wako vizuri sana.
4. Weka kumbukumbu ya muda wako.
Ili uweze kujua muda wako unautumiaje, ni vizuri kujiwekea kumbukumbu ya muda wako jinsi unavyoutumia. Unaweza ukaona ni kitu kama cha kijinga lakini ikifika siku kitakusaidia kujua tathmini ya wapi hasa unapopoteza muda wako mwingi ili kama ikiwezekana ujirekebishe. Kwa kujiwekea kumbukumbu ya muda wako uwe na uhakika utaweza kumiliki na kuutawala muda wako vizuri sana kwa mafanikio.
5. Kuwa makini na mambo yanayokupotezea muda.
Kuna mambo ambayo wengi wetu huwa yanatupotezea muda bila sababu. Jiulize ni kitu gani ambacho kinakupotezea muda sana. Je, ni mitandao ya kijamii, simu, mpira au ni kitu gani? Ukishajua kitu kinachokupotezea muda sana, tafuta njia nzuri namna ya kupunguza matumizi hayo. Acha kupoteza muda wako hovyo kwa kitu ambacho hakikupi faida ya moja kwa moja, badala yake linda na tunza sana muda wako kwani hapo ndipo mafanikio yako yalipo.
6. Jifunze kusema HAPANA.
Wengi huwa wanajikuta ni watu wa kupoteza muda wao pengine kutokana na kukubali vitu vingi bila kujiuliza kwa nini walikubali. Kabla hujasema ndiyo kwa jambo lolote la makubaliano jiulize linawezekana? Kama hutajifunza kusemaHAPANA hii itakufanya uzidi kupoteza muda wako mwingi wa thamani siku hadi siku bila ya wewe kujua. Kama huelewi kitu ni bora ukasema HAPANA kuliko ukafanya na ukaacha, hiyo itakuwa ni kupoteza muda.
7. Wape wengine majukumu.
Kama pengine kuna jambo ambalo unataka kulifanya wewe, lakini ukagundua wapo watu ambao wanaweza wa kakusaidia katika jambo hilo ni vizuri ukawapa wakafanya. Hiyo itakusaidia kufanya majukumu mengine zaidi na isitoshe utakuwa umeokoa muda wako mwingi. Acha kung’ang’ania kufanya mambo yote wewe, wape na wengine wakusaidie majukumu hayo ili kuokoa muda wako. 
Kumbuka, muda ni kitu cha thamani sana ambapo ukijenga tabia ya kuutumia vizuri utakuwezesha kufikia mafanikio makubwa yanajitokeza katika maisha yako.
Nakutakia kila la kheri katika matumizi bora ya muda wako na endelea kutembelea DIRA YA MAFANIKIO kujifunza na kuhamasika.
DAIMA TUPO PAMOJA MPAKA MAISHA YAKO YAIMARIKE,
Ni wako rafiki katika mafanikio,
 Imani Ngwangwalu,
Kama una maoni, ushauri au changamoto yoyote inayokuzuia kufikia mafanikio yako wasiliana nami kwa email dirayamafanikio@gmail.com au simu 0713 048035 kwa ushauri na msaada wa haraka.