google-site-verification: googleabbfd1327a3af7a3.html

Badili maisha yako sasa kwa kuwa na fikra sahihi.

Kujifunza zaidi juu ya maisha na mafanikio, nakualika kwenye kundi la whats app kujifunza kwa kina. Tututumie ujumbe kwa njia ya whats app kwenda 0687449428 kupata utaratibu wa kujiunga.

Dec 18, 2014

Kanuni Muhimu Katika Kuendesha Biashara Yako, Ili Iwe Na Mafanikio Makubwa Unayoyataka.

No comments :
Wengi wetu tumekuwa tukibuni, tukiiga na hata kuanzisha biashara mbalimbali ambazo, zimekuwa hazidumu wala kuendelea kwa muda mrefu kwa sababu ya kufilisika. Kukwama na kufilisika au kutokuendelea kwa biashara zetu hizi, limekuwa ndilo tatizo sugu au kikwazo kigumu kwa wafanyabiashara walio wengi, wakubwa kwa wadogo.

Wengi wetu tumekuwa tukilitafutia dawa au suluhisho la kudumu tatizo hili bila mafanikio. Kuendelea kudumu kwa tatizo hili, kumesababisha baadhi ya watu kukata tamaa kabisa ya kuendelea kufanya biashara. Hata hivyo maelezo na mifano halisi nitakayoitoa hapa, inaweza kutusaidia kutupatia majibu ya uhakika au suluhisho la kudumu nini kifanyike.

Ni muhimu kwetu kufata maelezo haya au kanuni hizi ikiwa endapo tumedhamiria kutimiza wajibu wetu wa kufanya biashara tuzipendazo, ili kuboresha maisha yetu na jamii kwa ujumla. Kanuni hizi ni muhimu hasa kwa watu walioamua kuanzisha biashara ndogondogo na wanazomiliki wenyewe, pengine baada ya kuchoshwa na kazi za kuajiriwa au kwa sababu nyingine.

Ukiweza kuzitumia kanuni hizi ndogondogo vizuri katika biashara yako, itakuletea mafanikio makubwa unayoyataka na hutajuta tena. Huna haja ya kulalamika tena wala kulaumu kwa sababu ya biashara zako kwenda hovyo, ni wajibu wako sasa kuzitumia kanuni hizi ili uone manufaa yake katika biashara yako. Unajua kanuni hizi ni zipi?

Hizi ndizo kanuni muhimu katika kuendesha biashara yako, ili iwe na mafanikio makubwa.

1. Ifanye biashara yako iwe ya thamani na ubunifu kila siku.

Kushindwa kutambua thamani ya ubunifu, ni jambo ambalo hupaswi kulifanya. Ni rahisi kuangukia kwenye mtego wa dhana kwamba lengo la biashara ni kutengeneza fedha tu. Lakini lengo sahihi la biashara ni kutengeneza thamani. Wakati si rahisi kutengeneza fedha katika kipindi kifupi bila kutengeneza thamani, kutengeneza fedha bila thamani si kitu cha kudumu.

Ni lazima biashara yako iweze kujenga thamani kwa ajili yako na wateja wako. Kwa jinsi utakavyotambua thamani ya kile unachotoa, ndivyo utakavyoweza kuelekeza nguvu zako zaidi. Kama biashara yako ni ya michezo kama ya kompyuta ama mingine, basi ujue thamani unayotengeneza hapo ni kuburudisha akili.

Ni kwa kutambua hivyo tu, ndipo utakapoweza kujitahidi kufanya huduma yako iwe bora zaidi na kuthamini wateja wako. Imetokea mara nyingi wamiliki wa biashara wameshindwa kutambua thamani wanayojaribu kutoa. Hawa hubaki tu wakitarajia makubwa bila ya kujua watayafanya vipi, kwani hawajui hata lengo la biashara yao. Ukitoa thamani kwa huduma unayotoa, wateja utapata tu.


2. Acha kujaribu kuuzia watu wasio sahihi.

Wakati mauzo ni kitu muhimu ili biashara iweze kudumu, huna haja ya kuhamanika kwa hilo na kudhani unalazimika kumlazimisha kila mtu unayekutana naye kufanya nawe biashara, ikiwa ni pamoja na marafiki zako na watu wa familia yako. Ni kupoteza wakati kujaribu kuwauzia watu ambao unajua wazi hawahitaji kile unachouza.

Kuuzia watu wasio sahihi ni pamoja na kujaribu kumuuzia kila mtu unayemwona mbele yako. Wapo wateja ambao ni rahisi kuwauzia kile ulichonacho kuliko wengine. Kwa mfano unafanya kazi ya kutengeneza tovuti halafu unakutana na mtu asiyejua chochote kuhusu intaneti na unaanza kumtangazia biashara yako ya tovuti, ni wazi utapoteza wakati wako kwani huyu si mteja wako sahihi.

Unatakiwa uwe na uwezo wa kukataa kuwapatia maelezo wateja wanaoonekana wazi kuwa na uwezekano wa kukuletea matatizo kuliko faida katika biashara yako. Waache wapinzani wako wafanye kazi ya kuwauzia badala yake. Kwa kufanya hivyo utajiokoa na matatizo ya kuumia kichwa kwa kuongea na watu ambao sio sahihi katika biashara yako.

3. Acha kutumia pesa nyingi kupita kiasi.

Kama biashara yao bado ni changa, acha kutumia pesa nyingi kupita kiasi mpaka utakapokuwa na mtiririko wa uhakika wa fedha zinazoingia. Usitumie fedha za kufanyia biashara hadi pale itakapokuwa muhimu sana na kwa manufaa yaliyo wazi kwa biashara yako. Hapa itabidi ujifunze kutokufanya matumizi yasiyo ya lazima katika biashara yako.

Ili kufanikiwa katika suala hili la kutokutumia pesa nyingi kupita kiasi, ni muhimu kujua utumie nini, kwa sababu ya nini, na kwa nini. Ikumbukwe pia katika malengo ya kawaida ya biashara, biashara inatakiwa kuingiza fedha mfukoni mwako, hivyo kabla ya kuwekeza unatakiwa ujue namna ya fedha ulizotoa mifukoni mwako kuwekeza zitakavyorudi.

4. Acha ugumu (ubahili) katika kutumia fedha.

Wakati kutumia pesa nyingi bila umuhimu ni kosa katika biashara, ni kosa pia kufanya biashara yako huku ukiweka mbele matumizi yaliyotawaliwa na ugumu katika matumizi ya fedha zako hata pale inapokuwa muhimu. Usiruhusu ugumu au ubahili ukwamishe ufanisi wa kazi yako.

Kama itatakiwa kuwatumia wataalamu wazuri wenye uwezo wa kufanya kazi Fulani vizuri kuliko utakavyofanya mwenyewe ama watakavyoweza kufanya watu wasio na uhakika, wa bei rahisi ni vizuri ukawatumia hao. Nunua vifaa imara na vinavyofanya kazi vizuri ikiwa una hakika fedha zako zitarudi.

Na mwisho kabisa, ukumbuke pia biashara ya kudumu na endelevu, huhitaji mtu awe amejiandaa na kujidhatiti kifikra, kimtazamo na awe tayari kubadilika kulingana na hali au mazingira ya kibiashara yanayomzunguka, kwani bila ya mambo au kanuni hizo kuzizingatia suala la kufilisika halitakuwa geni kwetu.

Nakutakia kila la kheri katika mafanikio ya biashara yako na endelea kutembelea mtandao huu wa DIRA YA MAFANIKIO kila siku kujifunza zaidi, karibu sana.

MAISHA YAKO YAIMARIKE,

IMANI NGWANGWALU,


No comments :

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.