google-site-verification: googleabbfd1327a3af7a3.html

Badili maisha yako sasa kwa kuwa na fikra sahihi.

Kujifunza zaidi juu ya maisha na mafanikio, nakualika kwenye kundi la whats app kujifunza kwa kina. Tututumie ujumbe kwa njia ya whats app kwenda 0687449428 kupata utaratibu wa kujiunga.

Jul 21, 2015

Kipaji Chako Ni Ajira Namba Moja.

No comments :
Tunu muhimu za mafanikio ambazo Mungu amewekeza ndani ya kila mtu ni vipawa/talanta. Kwa bahati mbaya sana na pengine kutokujua umuhimu wa vipawa, watu wengi hawatilii maanani vipaji walivyonavyo. Wengi wanaishi kwa kuiga maisha ya watu wengine kana kwamba wao ni nakala ya wengine. Kipaji chako ni mtaji mkubwa kama utaamua kukitumia vizuri ipasavyo. Kipaji chako ni fursa ya kufanikiwa maishani. Ni daraja la maendeleo kwa binadamu yeyote yule.
Kipaji ni umahiri wa kipekee aliouweka Mungu ndani ya akili ya mtu unaongoza usadifu wa viungo na fikra zake kufanya jambo Fulani kwa upekee kabisa. Ni talanta ambazo mtu anazo siyo kwa sababu kasomea bali ni ujuzi wa kuzaliwa nao, elimu inakusaidia tu katika kumfanya atumie kipaji chake kwa ufanisi na kwa manufaa zaidi. Kwa mfano, michezo mbalimbali, sanaa kama mziki, kuchora, kucheza mpira, kuimba, kusanifu, kubuni program za kompyuta, mitandao, na wakati mwingine kuchonga. Wapo watu ambao wana vipaji katika eneo mojawapo wanachotakiwa kufanya ni kuvitumia vipaji vyao.
Watu mashuhuri na wale waliofanikiwa sana ni wale waliotumia vipaji vyao vizuri. Kuna mifano hai mingi kama Filbert Bayi wa Tanzania alitumia talanta yake ya kukimbia mbio, wanamuziki kama vile Michael Jackson, Rose Muhando walitumia sauti zao kufanikiwa. Na hata wachezaji maarufu wanatumia vipaji vyao kucheza mipira na wanafanikiwa kuliko hata wasomi wenye shahada lukuki.
Wasanii na wana michezo wengi ni miongoni mwa watu maarufu na matajri sana duniani, japokuwa walio wengi hawana elimu kubwa kiasi cha kushangaza , walichofanya ni kutumia vipawa vyao kama ipasavyo. Maana hata sukari iliyo katika chai bila kukorogwa chai inaonekana haina sukari. Vivyo hivyo vipaji tunavyo, ili vifanye kazi vizuri inabidi tuvikoroge.

Mungu alituumba na vipaji na talanta nyingi tofauti ili tuvitumie kufanikiwa maishani. Kila mtu ana talanta yake imejificha ndani ya umaizi wa akili yake. Tunahitaji kuweza kuziibua talanta hizo  kule ziliko fichika, na kuzitumia huku tukibadili mitazamo na kasumba. Huwa nasikitika sana kumsikia mtanzania anasimama kwenye chombo cha habari akisema yeye ni maskini anahitaji msaada. Wakati huo kafunika talanta zake kibindoni, na nyuma kaacha ardhi kubwa, misitu mingi na hata watoto wengi ambao ni nguvu kazi muhimu katika kuchangia maendeleo.
Wapo watanzania wanadiriki kusema kuwa “sisi tutaendelea kubaki maskini hivihivi” na wengine wanadai umaskini wao ni mpango wa Mungu. Huu ni uongo na ni dhambi. Mungu angetaka sisi tuwe maskini asingeweza kutupa ardhi kubwa, asingetupa mvua nyingi na maji mengi, asingetupa samaki wengi, asingetupa ndege na wanyama wengi wa mwituni. Asingutupa afya njema na nguvu. Mungu alitupatia vyote hivi ili tuwe matajiri tuwasaidie na wale wanaoishi nchi zisizo na ardhi (mawe tu), nchi zisizo na bahari, nchi zisizo na msitu, mto wala bwawa. Sisi siyo maskini kamwe.
Na kiongozi au mwanasiasa anayetamka Tanzania ni maskini(wakati yeye ni tajiri) huyo ni mpotoshaji. Tusiwafundishe watoto wetu mtazamo hasi hata kama tunachangamoto. Kuwa na matatizo ni sehemu ya changamoto za maisha, tunazipaswa kuzikabili. Maana hakuna mtu au nchi inayojitosheleza. Ndio maana hata wao walioendelea huko ulaya bado wanakuja kwetu kununua malighafi ili wakutumie huko kwao.
Tena nadhani hata walioita mkakati wa kukuza uchumi na kupunguza umaskini(MKUKUTA) walikosea sana. Ingefaa ukaitwa “mkakati wa kukuza uchumi na ustawi wa maisha ya watu”. Kuutaja umaskini wakati tupo ndani ya utajiri mkubwa ni kujitafutia laana ya kudumu .Maana kama tunakubali sisi ni maskini kamwe hatuwezi kuweka mikakati ya maendeleo. Tunabaki na mikakati ya kimaskini.
Nafadhaishwa na mtazamo unaotaka kuzoeleka hapa Tanzania miongoni mwa vijana kuwa mtu yeyote akifanikiwa: kumiliki nyumba nzuri, shamba zuri lenye mavuno mengi, gari zuri, kiwanda na hata kuwa na elimu nzuri anaitwa fisadi, yaani mwizi. Unakuta vijana wenye nguvu wanapita makazi ya watu wenye nyumba nzuri wanasema “unayaona mahekalu ya mafisadi” wakimaanisha kuwa kila nyumba nzuri, kiwanda kikubwa, shamba kubwa ni la fisadi au mwizi. Kwao maendeleo ni wizi na siyo jitihada za kazi. Hawa wamepotoka sana.
Umaskini siyo mpango wa Mungu wala siyo ngozi ya kuzaliwa nayo isiyobadilika. Hata vitabu vitakatifu kama vile bibilia na msahafa vimesema wazi kwamba umaskini siyo mpango wa Mungu. Mungu anataka kila mtu aishi maisha mazuri yenye ustawi huku akimpenda na kutii mwongozo wake. Kila binadamu anahitaji maisha bora. Kila binadamu anahitaji kulala pazuri, kula vizuri, kusafri vizuri, afya bora, kupata elimu bora, mazingira safi, kucheza pazuri na kufurahia maisha kwa ujumla.
Watu wanakuwa kwenye shida kama vile kuishi katika nyumba mbovu, na kula chakula kibaya au kisichotosheleza siyo kwa sababu wao wanapenda, au kudhani kuwa maskini ndiyo sifa ya uadilifu. La hasha ni kwa sababu hawana. Fikra za kuyaona maendeleo yoyote ya mtu au kikundi cha watu ni ufisadi ni dalili kupoteza dira na kukosa matumaini kuelekea ufukara wa kudumu na dhiki kuu.
Na ukiona kijana mwenye nguvu anatamka kuwa hayo majumba ni ya mafisadi, fahamu kuwa familia yake na jamii inayomzunguka iko msibani. Si tetei wizi ama ufisadi na si sahihi kuwa mwizi au fisadi. Na ni dhambi hata kwa mungu wezi waadhibiwe tena vikali.
Lakini, pia sikubaliani na mtazamo kwamba kila anayefanikiwa ni mwizi au fisadi. Kuna watanzania wengi tu ambao wanakesha, wanafikiri na kubuni mbinu za kufanikiwa huku wakiongozwa na jitihada kubwa ya kufanya kazi na kuchangamkia fursa ndani na nje ya nchi na kutumia pesa kwa kwa makini katka uwekezaji binafsi bila ufujaji.
Hawatapanyi mapato kwa starehe na kuulimbukia utandawazi. Kila senti yao inatumika kwa tija na manufaa. Hawa wanastahili pongezi siyo kuitwa wezi. Kazi kubwa tliyonayo hasa vijana ni kutambua vipaji vyetu na kuvitumia ipasavyo.Tpunguze kulalamika tuongoze juhudi zetu katika ufanya kazi zaidi. Tutafanikiwa sana maishani.
§  MAKALA HII IMEANDIKWA NA MTEMI ZOMBWE, DAR ES SALAAM.

§  MAWASILIANO 0713 000027 

No comments :

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.