google-site-verification: googleabbfd1327a3af7a3.html

Badili maisha yako sasa kwa kuwa na fikra sahihi.

Kujifunza zaidi juu ya maisha na mafanikio, nakualika kwenye kundi la whats app kujifunza kwa kina. Tututumie ujumbe kwa njia ya whats app kwenda 0687449428 kupata utaratibu wa kujiunga.

Apr 25, 2015

Hii Ndiyo Kanuni Rahisi Kwako Unayoweza Kuitumia Kukupa Mafanikio Makubwa.

No comments :
Ni hivi. Ili uweze kufanikiwa na kufikia mafanikio makubwa unayotaka iwe katika masomo, kupata kazi, kuvuna sana mazao shambani, kupata faida katika biashara au kuwa na uhusiano mzuri na ndoa nzuri, ni lazima kwanza ujue kwamba hayo yote yanawezekana na yanakuhusu wewe moja kwa moja kwa asilimia zote na siyo bahati.
 
Unapotaka mafanikio ambayo huamini kwamba unastahili kuyapata, huwezi kamwe kuyapata hata kama ungefanya nini. Unapotaka kupata ajira, lakini ukajiambia kwamba kuna watu wengi wenye sifa kuliko wewe, ambao watapata kazi hiyo na siyo wewe, ni wazi pia hutapata kazi hiyo unayoitafuta.

Unapoamini kwamba utapata kazi hiyo kwa juujuu, lakini ndani kabisa mawazoni mwako unajua ni jambo gumu litakuwa gumu kweli. Unapoingia kwenye biashara kwa kuamini kwamba hutaweza kufanikiwa kwa sababu haijawahi kutokea ukafanikiwa au kwa sababu wewe una mtaji mdogo, hufahamiki na pengine hukusoma sana kama wengine, ni wazi hutafanikiwa.


Unaposema na kuamini kwamba una mkosi, utaendelea kuwa na mkosi hadi unaingia kaburini. Sisi binadamu ni kile tunachoamini. Kwa nini inakuwa hivyo, kwamba tunapoamini kuwa hatuwezi au tuna mkosi, mambo yanakuwa kama tunavyoamini?

Siyo kuamini tu kwamba mambo yatakwenda vibaya au tuna mkosi, lakini hata tunapoamini kwamba tunaweza, tutamudu, tutashinda, tutafurahi na tutatekeleza, basi ni wazi itakuwa hivyo. Hii ni kanuni ya kimaumbile, na ndiyo kanuni pekee ambayo ukiitumia ni lazima ikupe mafanikio unayoyataka. Kwa mujibu wa kanuni hii kwa vyovyote vile, tunavyofikiri na kuamini ndicho kinachokuwa chetu, iwe ni katika mafanikio au maanguko.

Kwa hiyo, ili kuweza kupata kile unachokihitaji katika maisha na kuenda sawa na kanuni hii ambayo ni rahisi kwako kuitumia na kukupa mafanikio, ni lazima kuweza kutambua umuhimu wa kufikiri vizuri. Kwa kufikiri kwetu vizuri itatusaidia kuweza kumudu na kutenda kwa mkabala wa kimafanikio na kuweza kuvuta mafanikio makubwa kwa upande wetu zaidi.


Kwa kufikiri kwamba hatuwezi au hatustahili, bila wenyewe kujua, tutafanya kwa mkabala wa kutoweza na kutostahili. Kumbuka kuwa upo uhusiano mkubwa sana kati ya fikra zetu, hisia zetu na tabia au matendo yetu. Tunapofikiri kwamba hatuwezi, bila kujua, tutakuwa na tabia zitakazotupeleka mahali ambapo hatutaweza kweli. 

Mwandishi na mwanafalsafa maarufu duniani Shakespeare aliwahi kusema: ‘Hakuna jambo baya au zuri, bali kufikiri kwetu ndiko kunakolifanya jambo kuwa hivyo’. Huu ndiyo ukweli , kwamba, kufikiri vibaya hutudhuru sana , tuwe tunajua au hatujui. Ubaya au uzuri wa mawazo yetu, hasa yale ya kina ni kwamba, kile tunachokifikiri  na kukiamini ndicho kinachotokea au kufanyiwa kazi, hayachagui au kutuhurumia ati kwa sababu hatujui juu ya ukweli huo.

Kwa hiyo, hatua ya awali kabisa ya mafanikio ya binadamu yako kichwani au mawazoni mwake. Kuna familia, koo, hata makabila ambayo yamekuwa na fikra kwamba hayawezi au hayastahili. Mtu kutoka familia, koo au makabila hayo anaweza kuwa na uwezo mkubwa sana katika kutenda, kipaji na ufahamu mkubwa ajabu, lakini akabaki kuwa mbumbumbu ambaye familia , ukoo au kabila lake limefanywa kuaminika kwamba ndilo linalostahili kuweza au kuwa nacho.

Bila kuanza kukagua namna tunavyofikiri, inaweza kuwa kazi bure kujaribu kutafuta au kuzungumzia mafanikio kwa ngazi yoyote, iwe mtu binafsi au taifa. Ni lazima tuanze kwa kujiuliza kile tunachoamini kuhusu mafanikio, yaani kupata kile tukitakacho maishani. Inawezekana kabisa, bila sisi wenyewe kujua tulishawekewa mipaka ya mafanikio tangu wakati tukiwa wadogo. Mipaka kama hii huwekwa vipi?


Inawezekana kabisa wazazi au jamii yote tulimokulia ilikuwa ikisema na kutenda kwa njia ambayo ilituonyesha kwamba tunachoweza sanasana ni kuhangaika na kupata ajira mahali, basi. Pengine ilisema na kutenda kwa njia ambayo ilituonyesha kwamba, ni vigumu kwetu kumiliki gari. Inawezekana kwamba ilisema na kutenda kwa njia ambayo ilituonyesha kwamba hatupaswi kuinuka sana kimaisha kwani sisi kwa ukoo au kabila fulani hatustahili.

Pia kuna wakati tunajikuta tukitamani kusonga mbele katika kutafuta kile tunachokitaka, lakini tunazuiwa na uvivu wa aina fulani tu tusioujua sababu yake, tunazuiwa na kuahirisha kufanya hivyo, bila kujua ni kwa nini. Inawezekana kabisa kwamba hiyo inatokana na malezi, mazingira tulimokulia au uzoefu wetu maishani. 

Kumbuka kuwa kuna vizuizi vingi vilivyowekwa kwenye mawazo yetu katika hatua hizo tulizopitia maishani. Lakini ili uweze kumudu kuondokana na vizuizi hivyo ni muhimu kwako kujua mambo mawili tu, ambayo ni  kuweza kutumia kanuni tuliyoongelea ya kuamini kuwa katika maisha yetu tutaweza, tutamudu, tutashinda na tutatekeleza na jambo la pili ni kubadili mtindo wako mzima wa kufikiri.

Unapoamua kubadili mtindo wako wa kufikiri sio kwamba tu unakuwa unajiondoa kwenye vizuizi vya kutofanikiwa, bali pia unakuwa unajiweka katika nafasi nzuri ya kupata kile unachokihitaji. Je, unawezaje kubadili mfumo wako mzima wa kufikiri na kukuwezesha kukupatia kile unachohitaji ama kufanikiwa kwa ujumla? Kujua hilo hakikisha unafuatilia makala ijayo katika DIRA YA MAFANIKIO bila kukosa, ili kujua mawazo yako jinsi yanavyoweza kufanya kazi na kukupa utajiri. 

Ansante sana kwa kuwa msomaji mzuri wa DIRA YA MAFANIKIO, endelea kuwashirikisha wengine kujifunza zaidi kupitia mtandao huu. Kwa pamoja tukishirikiana tunaweza kabisa kufika mbali kimafanikio na kuufuta umaskini.

DAIMA TUKO PAMOJA MPAKA MAISHA YAKO YAIMARIKE.

IMANI NGWANGWALU,
0713048035,

No comments :

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.