google-site-verification: googleabbfd1327a3af7a3.html

Badili maisha yako sasa kwa kuwa na fikra sahihi.

Kujifunza zaidi juu ya maisha na mafanikio, nakualika kwenye kundi la whats app kujifunza kwa kina. Tututumie ujumbe kwa njia ya whats app kwenda 0687449428 kupata utaratibu wa kujiunga.

Jan 1, 2015

Kama Unataka Mafanikio Makubwa Mwaka 2015, Acha Kukata Tamaa Tena Katika Mambo Haya.

No comments :
Mara nyingi wengi wetu huwa ni watu wa kufikiria kukata tamaa hasa pale tunapokutana na magumu katika maisha yetu. Kukata tamaa  huwa kuna kuja pale ambapo mambo huwa hayajaenda sawa kama tulivyopanga, na wakati mwingine huwa tunakatishwa tamaa na mazingira ambayo huwa tuna uhakika nayo hayawezi kutufanikisha katika kile tunachokitaka katika maisha yetu.

Kabla hujakata tamaa kwa kile unachokifanya, elewa kabisa kukata tamaa ni moja ya sababu inayowafanya watu wengi sana washindwe kufikia malengo yao waliyojiwekea. Katika maisha yako acha kufikiria kwanza kukata tamaa pale unapokumbana na magumu. Hakuna utakalopanga kulipata ukalipata kirahisi rahisi kama wengi wetu tunavyotamani iwe. Maisha ni changamoto.

Inawezekana ni kweli malengo na mipango yako mikubwa uliyojiwekea mwaka huu unaoisha leo, hayajakuendea vizuri kama ulivyokuwa ukitaka. Hilo lisikutishe unayonafasi ya kujipanga upya kwa mwaka 2015 na kufanya mambo makubwa. Hata kama kuna mambo yalikukatisha tamaa sana na ukajiona umeshindwa, ninachotaka kukuwambia huo sio mwisho wa safari yako ya mafanikio.

Kumbuka, tunaishi katika dunia ambayo ina njia nyingi za kutufanikisha kwa yale tunayofanya. Acha kujidanganya na kuamini kuwa umeshindwa na huwezi tena kusonga mbele kutokana na mambo yaliyokukatisha tamaa. wewe sio mtu wa kushindwa kama unavyofikiri, unayo nafasi kubwa ya kufanya mabadiliko na kuufanya mwaka 2015 uwe wa historia kwako kama ukiamua.

Kama Unataka Mafanikio Makubwa Mwaka 2015, Acha Kukata Tamaa Tena Katika Mambo Haya:-

1. Acha kukata tamaa kujiwekea  mipango na malengo yako upya.

Ni kweli mambo yako yanaweza yakawa yameharibika kiasi cha kwamba kwako unaona kama inakuwa ngumu kusonga mbele. Huo sasa ndio wakati wako wa kutulia na kuweka malengo yako upya. Acha kukaa chini na kusikilizia maumivu ya kushindwa huku ukiwa upo hapo hufanyi kitu. Chukua hatua ya kuendelea mbele kwa kuweka malengo yako upya. Usikatishwe tamaa wewe ndio mwamuzi wa mwisho wa maisha yako, weka mikakati upya ya kufanikiwa.


2. Acha kukata tamaa kushughulikia matatizo yako.

Kuna wakati katika maisha yetu mambo yanaweza kuwa magumu kiasi cha kwamba unaweza ukaanza kukata tamaa. Na ugumu huu huwa wakati mwingine unakuja pale ambapo unajikuta wewe binafsi unapokuwa unakabiliana na tatizo zaidi ya moja. Usipokuwa makini hapa, huwa ni rahisi kwako kukata tamaa na kuacha kabisa kushughulikia hayo matatizo yako. Ili ufanikiwe hutakiwi kukata tamaa, matatizo hayawezi kuondoka mpaka wewe mwenyewe uyakabili. Fanya jitihada zako zote pale unapoweza halafu jipongeze kwa hatua utakayopiga.

3Acha kukata tamaa kuweka wazi wazo na ndoto zako.

Utaweza kuweka wazi wazo na ndoto zako kama utajijengea utaratibu wa kuwa na kijitabu kidogo ambacho utakuwa unaweka malengo yako, hiyo itakupa nguvu ya kufatilia malengo yako kwa ukaribu kabisa. Ukifanya hivyo hapo utakuwa unaweka wazi wazo na ndoto zako kutekelezwa, hata kama ulifanya hivi mambo hayakukaa sawa, acha kukata tamaa hii ni muhimu sana kwako. Ukifanya hivi katika maisha yako hii itakuwa na sawa na kuzifuata fursa huko ziliko nazo zitakupokea kwa mikono miwili.

4Acha kukata tamaa kujifunza kutokana na makosa.

Kama ulikuwa ukifanya hivi na umesahau na kukumbusha anza kujifunza tena kutokana na makosa uliyoyafanya. Kama uliwahi kukosea na ukapata funzo fulani anza kulithamini hilo funzo kwa kuchukua mafundisho yake na kuyafanyia kazi. Na ukiweza kufanya hilo, utaona kumbe kukosea ni hatua moja wapo katika kupata mafanikio. Kwani kuna uwezekano mkubwa kabisa kama usipotaka kujifunza kutokana na hilo basi utakuwa unalikwepa daraja ambalo lingekuunganisha na mafanikio.

5. Acha kukata tamaa kuwekeza kwako mwenyewe.

Mara nyingi tumekuwa tukitumia pesa kuwekeza katika miradi yetu, lakini tumekuwa tukisahasahau kujiwekeza sisi wenyewe katika maisha yetu. Ili uwe na mafanikio makubwa ni muhimu kwako kujiwekeza wewe kwa kujisomea kila siku. Unapochukua jukumu la kujifunza kila siku kwa kujisomea vitabu na vitu vya mafanikio hapo unakuwa unafanya uwekezaji mkubwa kwako mwenyewe. Pengine mwaka huu ilikuwa tabu kidogo kwako kijisomea, mwaka 2015 fanya mabadiliko makubwa sana kwa kujisomea vitu vingi vitakavyobadili maisha yako.

6. Acha kukata tamaa kuwa na watu sahihi.

Hawa ni watu ambao wewe unapokuwa nao unafurahia, wanaokupenda, kukuthamini, na wanaokutia moyo wa kutokata tamaa katika mambo yako. Hawa ni wale watu ambao ukikaa nao wanakufanya ujihisi uko hai, ambao wanaokukumbatia wewe wa sasa hivi na wanaotamani kumkumbatia yule unayetamani kuwa, bila masharti yoyote. Ni watu ambao wanapenda kuona ndoto zako zikitimia, hivyo ni muhimu kuwa nao ili kutimiza malengo yako.

7. Acha kukataa kuomba msaada wa kimawazo.

Kuna uwezekano mkubwa ukawa umekatishwa tamaa na watu ambao umekuwa ukiwaomba msaada wa kimawazo, pengine pale mambo yako yalipokuwa yakikwama. Na inawezekana walikushauri vibaya na kukatisha tamaa na wewe ukafikiri kuwa kuomba ushauri kwa mtu kama ni aina fulani ya udhaifu. Acha kukata tamaa kwa hili, kwa kawaida binadamu huwa hatujui kila kitu, tafuta watu sahihi watakaokushauri katika mambo yako na hii itakusaidia wewe kukupa nguvu  kusonga mbele hata kama kuna sehemu ulikuwa unahisi umekata tamaa.

8. Acha kukata tamaa kusamehe.
Migongano katika maisha ya kila siku ni kitu ambacho mara nyingi huwa hakikwepeki. Na kila mmoja wetu kwa sehemu amewahi kukosewa na mtu kwa namna yoyote ile. Kama hili limekutokea katika maisha yako, jifunze kusamehe. Acha kujenga chuki, kisirani moyoni na kuona kuwa haiwezekani kumsamehe. Hata kama mtu kakukosea mara ngapi acha kukata tamaa kwake, msamehe na kisha chukua jukumu la kufanya mambo mengine. Unaposamehe hii inakusaidia wewe kuishi maisha ya amani na utulivu ndani mwako.

Kwa kuchukua jukumu hilo la kutokukata tamaa kwa mambo hayo, mwaka 2015 utakuwa na mafanikio makubwa kwako na wala hutajuta. Chukua hatua muhimu kwa kutafakari haya unapoenda kuanza mwaka mpya kwa siku ya kesho.

DIRA YA MAFANIKIO inakutakia mafanikio mema na kheri ya mwaka mpya uwe wa Baraka na mafanikio makubwa kwako, ansante kwa kuwa pamoja nasi.

DAIMA TUPO PAMOJA MPAKA MAISHA YAKO YAIMARIKE,

IMANI NGWANGWALU,




No comments :

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.