google-site-verification: googleabbfd1327a3af7a3.html

Badili maisha yako sasa kwa kuwa na fikra sahihi.

Kujifunza zaidi juu ya maisha na mafanikio, nakualika kwenye kundi la whats app kujifunza kwa kina. Tututumie ujumbe kwa njia ya whats app kwenda 0687449428 kupata utaratibu wa kujiunga.

Mar 24, 2015

Hatua 8 Za Kufuata Ili Kuwa Mjasiriamali Mwenye Mafanikio Makubwa.

No comments :
Ni jambo ambalo mara nyingi huwa linafahamika na liko wazi kuwa, ili kuweza kufanikiwa na kuwa mjasiriamali mwenye mafanikio makubwa ni lazima suala la kufanya kazi kwa ubunifu, juhudi kubwa na maarifa pamoja na kuwa king’ang’anizi kwenye mipango na malengo yako huwa linahusika kwa sehemu kubwa sana. Hutaweza na huwezi kuwa mjasiriamali mkubwa na kufikia mafanikio makubwa kama utakuwa huzingatii mambo hayo.

Pamoja na kufanya kazi kwa ubunifu, juhudi kubwa na maarifa, kuwa ni nguzo muhimu sana kwako wewe mjasiriamali ili kuweza kufikia mafanikio makubwa, lakini pia huwa kuna kitu cha ziada ambacho ni lazima ukifanye na kukifuata ili kuweza kuona mafanikio hayo unayoyataka. Kitu hiki ni wewe kuweza kujua hatua muhimu za kufuata ili kuweza kuwa mjasiriamali mwenye mafanikio makubwa.

kwa kadri unavyozidi kujua hatua hizi zinakuwa zinakupa nguvu na hamasa kubwa ya kuendelea kung’ang’ania na kushikilia ndoto zako mapaka kuona zinatimia. Hizi ni hatua muhimu sana kwako na kwa kila mjasiriamali mwenye nia na kiu ya kutaka kufanikiwa na kufika mbali hasa katika safari ya kibiashara na maisha kwa ujumla. Je, unajua ni hatua zipi unazotakiwa kuzifuata ili kuwa majsiriamali mwenye mafanikio?

Hizi Hatua 8 Za Kufuata Ili Kuwa Mjasiriamali Mwenye Mafanikio Makubwa.

1. Fanya kile unachokipenda kwa moyo wote.
Watu wengi huwa wana kawaida ya kufanya mambo yale ambayo hawayapendi sana katika maisha yao. Hii huwa inatokea au wanafanya hivyo kwa lengo hasa la kuingiza kipato.  Kutokana na kufanya mambo kwa kutopenda iwe kazi au biashara  hii  mara nyingi husababisha kutokuwa na mafanikio makubwa kwa kile wanachofanya.

Mafanikio huwa hayawezi kupatikana kwa sababu unapokuwa unafanya kazi ambayo huipendi kikubwa kinachokutokea utajikuta unakuwa ni mtu wa kulalamika sana na pia unakuwa unakosa ubunifu kitu ambacho ni hatari na  kitakufanya ushindwe moja kwa moja kwa kile unachokifanya. Kama unataka kuwa mjasiriamali mwenye mafanikio makubwa, chagua kitu kimoja unachokipenda na kifanye kwa moyo wote, mafanikio makubwa utayaona.


 

2. Anza kwa kidogo.
Ni ushauri ambao pengine umewahi kuusikia mara nyingi  kwa namna moja ama nyingine, lakini na mimi napenda kukumbushia leo kwa kile unachotaka kukifanya kwenye biashara yako hiyo anza kwa hatua ndogo kwanza. Unapokuwa unaanza kwa kidogo inakuwa inakusaidia wewe kuweza kupima kama utaweza kwenda kwa hatua nyingine zaidi.

Acha kuogopa wala kukatishwa tamaa na kitu chochote katika maisha yako kwa kuhofu kuwa pengine hayo malengo yako hayawezi kutimia. Kila kitu kinawezekana na hakuna kitu kinachoshindikana kwako hata kidogo. Anza kutekeleza malengo yako kidogo kidogo hata kama ni makubwa vipi, lakini tambua kuwa ni lazima uyafikie.

3. Jifunze kutoka kwa wengine.
Hautaweza kufanikiwa kama utakuwa tu unaendesha biashara yako wewe mwenyewe na kushindwa kujifunza kutoka kwa wengine. Unapojifunza kutoka kwa wengine inakuwa inakusaidia kukupa wewe kuweza kutambua mapungufu uliyonayo ambayo yanaweza kukukwamisha na kukusaidia kuweza kusonga mbele zaidi.

Hata hivyo unaweza pia ukajifunza mikakati na mbinu za ujasiriamali zaidi kwa kujisomea kutoka kwa wajasiriamali wengine wakubwa kupitia vitabu ambapo nako huko utapata maarifa  bora yatakayokutoa hapo ulipo. Kama una nia na shauku kubwa kweli ya kutaka kufanikiwa na kuwa mjasiriamali mwenye mafanikio makubwa ni lazima ukubali kujifunza kutoka kwa wengine kila siku.

4. Chukua hatua mapema.
Kusoma sana hakutakusaidia kitu hata kama utasoma vipi hiyo itakuwa ni sawa na kazi bure kama tu utakuwa huchukui hatua kwa vitendo kufanyia kazi kile kidogo unachojifunza. Kuwa mtu wa vitendo ni hatua muhimu sana kwako wewe ya kukuwezesha kufikia mafanikio makubwa katika safari yako ya ujasiriamali na biashara.

Watu wengi wenye mafanikio makubwa siku zote huwa ni watu wa vitendo tu. Ndani ya maisha yao huwa yametawaliwa na vitendo na huwa ni watu ambao hawajui kitu kinachoitwa kuahirisha mipango waliyojiwekea. Jifunze kuchukua mapema katika kila kitu unachokifanya katika maisha yako, hiyo itakusaidia kufika mbali sana katika maisha yako. 

5. Kuwa na mipango imara.
Kila kitu unachokijua wewe chenye mafanikio makubwa hapa duniani, huwa kinaanza na mipango tena mipango iliyoimara. Hata biashara yako inahitaji kuwa na mipango mathubuti na imara ili iweze kufanikiwa zaidi na kukuletea matunda unayoyataka. Kinyume cha hapo utabaki ukilaumu tu kuwa mambo magumu kama wengine wanavyofanya.

Jifunze kujiwekea mikakati na mipango endelevu kwa biashara yako. Hakikisha mipango utakayojiwekea iweze kukusaidia kuisimamisha biashara yako na kuwa imara zaidi kwa miaka mingi zaidi. Chukua muda wa kutafakari na kujiuliza baada ya miaka miwili, mitatu au mitano kuanzia leo utakuwa umefika wapi kibiashara? Kuwa na mipango imara ni nguzo muhimu ya kukufikisha kwenye mafanikio makubwa unayoyahitaji.

6. Tengeneza ‘timu’ imara itakayokusaidia.
Mara nyingi huwa hakuna jeshi la mtu mmoja au mafanikio makubwa yatakayoonekana kwa mtu mmoja pekee. Kuna wakati katika maisha yetu huwa tunalazimika kutafuta watu watakaotusaidia katika biashara zetu hilo ni lazima. Hii huwa ni muhimu sana kwa sababu sio kila kitu tutaweza kukifanya sisi wenyewe tunahitaji wasaidizi ambayo ndiyo timu yenyewe.

Katika zoezi zima la zima la kujenga timu hakikisha unatafuta watu ambao watakusaidia kupigania kile unachotaka kitimie katika maisha yako. Nikiwa na maana kuwa timu yako inatakiwa kuwa msaada na kuweza kufanya kazi na wewe bega kwa bega mpaka malengo yako uliyojiwekea yanatimia yanatimia. Kuwa na timu imara ni kitu muhimu sana katika safari yako ya ujasiriamali.

7. Acha kufikiria kuwa umechelewa.
Unaweza ukawa unakwama au kushindwa kuendelea mbele kama inavyotakiwa iwe katika biashara yako, kutokana na mawazo ambayo unayo ya kuhisi kwamba pengine umechelewa kwa kile unachotaka kukifanya. Kwa mawazo haya yamekuwa yakikupelekea wewe kushindwa kufanya mabadiliko makubwa  yako katika biashara.

Kitu usichokijua hakuna kitu kinachoitwa kuchelewa katika maisha yako. Wapo watu ambao mwanzoni walijihisi na kujiona wamechelewa katika maisha yao, lakini walipokuja kugundua ukweli huu walikuja kufanya mabadiliko makubwa sana. Kisikuzuie kitu chochote kufikia ndoto zako. Unaweza ukawa na maisha yoyote unayotaka ukiamua.

8. Kuwa na mitazamo chanya.
Hiki ni kitu muhimu sana kukufikisha katika ngazi ya juu ya mafanikio na hatimaye kuwa tajiri kama utaamua kuwa na mitazamo chanya. Unapokuwa na mitazamo chanya inakuwa inakusaidia kukupa hamasa na nguvu ya kuona mambo yako yanawezekana hata katika maeneo ambayo kweli yanakuwa yanachangamoto.

Ikumbukwe kuwa watu wengi huwa wanakosa kufikia mafanikio makubwa kibiashara kutokana na kuwa watu wa hasi sana katika maisha yao. Hali hii huwa inawapelekea wao kushindwa kukabiliana na changamoto hata zile ndogo ambazo walikuwa wanauwezo wa kuzivuka. Kuwa na mawazo chanya ni muhimu sana kwa mafanikio yako.

Kwa kumalizia, ukumbuke kuwa kiu ya mafanikio yako unayoitaka uitimize itafanikiwa tu endapo, utakuwa mtu wa kujifunza na kuchukua hatua muhimu zitakazoweza kubadili maisha yako. Chukua hatua leo na acha kusubiri kesho au kesho kutwa utakuwa umechelewa sana na hautabadili kitu. Hizo ndizo hatua muhimu za kufuata ili kuwa mjasiriamali mwenye mafanikio.

Nakutakia mafanikio mema, endelea kutembelea DIRA YA MAFANIKIO kwa kujifunza na kuhamasika zaidi.

DAIMA TUPO PAMOJA MPAKA MAISHA YAKO YAIMARIKE,

IMANI NGWANGWALU,




  

No comments :

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.