google-site-verification: googleabbfd1327a3af7a3.html

Badili maisha yako sasa kwa kuwa na fikra sahihi.

Kujifunza zaidi juu ya maisha na mafanikio, nakualika kwenye kundi la whats app kujifunza kwa kina. Tututumie ujumbe kwa njia ya whats app kwenda 0687449428 kupata utaratibu wa kujiunga.

May 29, 2015

Hivi Ndivyo Unavyoweza Kuishi Na Watu Wasumbufu Ulionao Kazini Kwako.

No comments :
Ajira au kazi katika ujumla wake huwakusanya pamoja watu wa tabia, haiba na mikabala mbalimbali ya kimaisha. Tabia na haiba hizi tofauti wakati mwingine huweza kusababisha misuguano , majuto na hata sononi. Kuna wakati bosi ni mkorofi na watumishi wengine wanakuwa wamekaa kisharishari tu.

Hali kama hizi ndizo huwafanya baadhi ya watumishi kusubiri likizo kwa hamu kubwa sana.  Kwa kwenda likizo hujisahaulisha na vurugu hizi. Lakini wengine huamua kubadili ama kuacha kazi kabisa. Hatua hizo mbili zinaweza kuwa ni za muda mfupi tu. likizo hatimaye huisha na mtu hurejea kazini au kule anakoenda baada ya kuacha sehemu ya awali, anaweza kupambana na kero kubwa na nyingi zaidi.

Nijuavyo mimi, kuna mambo ambayo mtu akiyafanya, vurugu na tafrani hizi za makazini haziwezi kumdhuru, bila kuhama au kwenda likizo.

Mambo haya akiyafanya atahisi amani ya nafsi, utulivu wa mawazo na kufurahia kazi au kufurahia maisha hata nje ya eneo la kazi. Haya ni mambo ambayo katika hatua za awali, mtu anaweza asifanikiwe, hata baada ya kufanya. Lakini kwa kujizoeza tena na tena atapatwa na mshangao kugundua yanafanya kazi.


Kama watu wa kazini kwako au pengine popote wanazungumza kwa kufoka au mkabala wa kukosa adabu na upendo, unaweza kujikuta unawaiga. Kama ni kufoka nawe utafoka, kama ni kutukana nawe utatukana na kama ni ubishi utabishana pia. Hii husaidia kuongeza tatizo na kuchokoza na kuchochea hisia.



Badala ya kufanya hivyo, unashauriwa kuwa mtulivu, uzungumze na kutenda kwa amani na upendo. Kwa kufanya hivyo, bila ya wao kujua, watajikuta wakiiga tabia zako. Bila kujali nafasi yako kazini, utaona wengine wakikutazama kama dira, kwa mfano na kama mwanga.

Kila siku kabla hujafika au kuingia kwenye eneo lako la kazi, jitahidi kusema kwa kurudia maneno haya ‘mawazo ni yenye utulivu mkubwa kwa siku nzima ya leo. Namwaga utulivu ambao umenizunguka. Nazungumza kwa amani, utiifu na tabasamu. Nachagua kutenda kwa amani na upendo.’ Yaseme haya ukiwa umedhamiria na hisia zako zikiamini hivyo.

Jaribu kusalimia kila unayekutana naye hapo kazini. Kila unapojihisi kuwa umekerwa, vuta pumzi kwa upole na kwa kina kiasi mara tatu hivi, kabla hujaamua au kusema lolote.


Unapaswa kutambua pia maneno unayoyasema au kuyaandika. Hii ina maana kwamba, kabla hujaandika au kusema jambo, uwe unajiuliza kwanza. Kila linalotoka mdomoni mwako au mkononi mwako(Kuandika) liwe limepata kibali chako baada ya kulitafakari na kuona halitasababisha madhara kwako au kwa wengine.

Usizungumze kwa sauti ya juu sana au ya chini sana wala usikubai kuchotwa na mtu anayefoka, nawe ukaanza kufoka. Wacha anayefoka afoke huku ukijua wazi kwamba, anajiumiza bure, huku wewe ukiwa huna haja ya kujiumiza. Kumbuka kwamba, kufoka ni kujitetea kwa sauti kuliko mantiki. Usikubali kuwa dhaifu wa kiwango hicho.

Jaribu kutafuta muda, tuseme wakati wa mapumziko la mchana. Tafuta mahali palipotulia, kaa hapo na kujaribu kupeleka mawazo yako kwenye eneo lenye mandhari inayopendeza. Yapeleke hapo, yakae kwa muda wa kutosha. Kama siyo mandhari, basi kumbuka tukio lolote huko nyuma ambalo liliwahi kukufurahisha sana. Liweke mawazoni mwako kwa muda wa kutosha.

Jaribu kuweka mawazo yako yote kwenye kile unachokifanya kwa wakati huo. Hii itakuwezesha kutokuingiza mawazo yenye kukera kwenye mfumo wako wa kufikiri.

Badala ya kupoteza muda na nguvu kwa kujiuliza sababu za watu kufanya mambo fulani dhidi yako au kuhusu tabia usizozipenda kwa baadhi ya watu, ni botra kuweka nguvu na mawazo yako kwenye namna utakavyoweza kuboresha vitendo vyako.

Kabla hujazungumza na mtu anayekukera au unayemwogopa ama pengine usiyempenda, pumua polepole kwa kina, ukivuta pumzi ndani na kuzitoa nje, kiasi cha mara tatu na tengeneza picha kwenye mawazo yako, ukijiona kuwa mnazungumza kwa amani na upendo na mtu huyo.

Kwa kufanya haya na baadhi yake utamudu kukabiliana na watu na mazingira ambayo hayakuridhishi kazini kwako au hata nyumbani na kwenye mkusanyiko wa watu ambao unapaswa kuwa nao.

Tunakutakia kila la kheri katika safari yako ya mafanikio, endelea kutembelea DIRA YA MAFANIKIO kujifunza zaidi kila siku.

DAIMA TUPO PAMOJA MPAKA MAISHA YAKO YAIMARIKE,

IMANI NGWANGWALU,
0713 048035,





No comments :

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.