google-site-verification: googleabbfd1327a3af7a3.html

Badili maisha yako sasa kwa kuwa na fikra sahihi.

Kujifunza zaidi juu ya maisha na mafanikio, nakualika kwenye kundi la whats app kujifunza kwa kina. Tututumie ujumbe kwa njia ya whats app kwenda 0687449428 kupata utaratibu wa kujiunga.

May 12, 2015

Kanuni 12 Za Kukuongoza Kwenye Njia Sahihi Ya Kuufikia UTAJIRI.

1 comment :
Wataalamu mbalimbali wa mambo ya mafanikio wameweza kuthibitisha kuwa iko sayansi  ya kuwa tajiri na ni sayansi hasa , kama ilivyo hisabati za aina mbalimbali. Sayansi hii ambayo wataalamu hawa wanaizungumzia ni rahisi kuifuta na  ambayo mwanadamu yeyote  anaweza kuitumia kuweza kufikia mafanikio makubwa anayotaka kama tu ataamua kufanya hivyo.
 
Kwa mujibu wa sayansi hii inadai kuwa katika maisha yetu tuwe tunajua ama hatujui lakini zipo sheria au kanuni fulani zinazotawala mchakato mzima wa kupata utajiri, na mara nyingi sheria hizi zinapoeleweka kwa mtu ama kufuatwa, mtu huyo atakuwa na kila uwezekano wa kuwa tajiri katika maisha yake, bila kizuizi chochote kile.

Ni kweli. Wale waliofanikiwa na kuwa matajiri, hujua namna wanavyoupata  kwa kufuata misingi, sheria na taratibu ndogondogo tu. Wale wasiofanikiwa kuwa matajiri huwa hawajui sheria hizi ndogondogo na hivyo huishia kudhani kwamba utajiri ni matokeo ya bahati au matokeo yasiyotarajiwa ama kitu fulani cha ajabu ama cha kijinga.

Anthony Robbins ni mmoja wa watu waliofanikiwa sana katika kuwafundisha watu mbinu za kufanikiwa, akiwa pia anawafundisha wanamichezo kadhaa maarufu duniani, watu matajiri wakubwa na wakuu wa makampuni zaidi ya 500. Kupitia yeye ameweza kutengeneza matajiri wengi sana duniani kutokana na sayansi  ya mafanikio anayofundisha.

Katika taratibu yake anayoiita  FIKA HADI UKINGONI , Anthony Robbins anaorodhesha kanuni ama sheria 12 za msingi anazosema ndizo zinazowaongoza watu wengi kuweza kuufikia utajiri. Kiu na matamanio yake nikuona kila mtu kufikia mafanikio makubwa sana. Kanuni  hizo anazoziorodhesha ni hizi zifuatazo:-

1. Kuwa na maamuzi sahihi ya kuwa tajiri.
Mara nyingi watu wanaokwama huwa hawaamui ama kuwa na mwelekeo wa moja kwa moja wa utajiri wanaoutafuta. Hili ni wazi kabisa. Ili uweze kufanikiwa ni lazima kuwa na maamuzi sahihi na kuweza kujua umbali wa kule unakoelekea kabla ya kuanza kuufukuzia utajiri unaoutaka. Kaa chini, kisha chukua maamuzi ya kuwa tajiri. Kama hujafanya uamuzi, huwezi kuwa tajiri. 



2.Tambua kuwa utajiri ni kitu kinachowezekana.
Kwa kawaida mtu ana uwezo wa kufanikisha kile anachokiona katika mawazo yake na siyo zaidi ya hapo. Kama wewe ni mtu wa fikra hasi na kuona kuwa utajiri ni kitu ambacho hakiwezekani, huo ndio ukweli hautaweza kuwa tajiri katika maisha yako yote hata ufanyaje. Kitakachokufanya usifanikiwa si kingine ni mtazamo wako tu. Badili mtazamo wako na amini kuwa unao uwezo wa kuwa tajiri, utafanikiwa.


3. Anza kufanyia kazi ndoto zako mara moja.
Siri kubwa ya mafanikio ni kuanza kufanyia kazi ndoto zako mara moja na kuachana na hali ya kusitasita. Watu wasiofanikiwa mara nyingi huwa hawaanzi kabisa. Ikiwa utaendelea kufikiria unalofikiria litaendelea kubaki hivyo milele. Ili uweze kuwa tajiri ni lazima uanze , popote, si lazima iwe mahala maalum kama unavyofikiri, wewe anza tu, mambo mengine yatajipanga mbele ya safari.


4. Kuwa na mipango ya uhakika.
Kama unataka kufanikiwa zaidi kwa kitu unachokifanya sasa, tafuta njia ya kufikia mafanikio yako kutoka kwa mtu mwingine aliyewahi kufanikisha hilo. Weka mipango ya uhakika na inayowezekana kwako kutekelezeka. Jifunze haya kwa waliofanikiwa kabla yako. Lakini usiachane na uwezo wako wa kufikiria na kuangalia mambo mengine ya ziada yatakayo kuwa msaada kwako pia katika kukufanikisha.


5. Jiwekee utaratibu wa kufuatilia mipango yako.
Kuwa na mipango ya uhakika peke yake haitoshi. Ili uweze kufanikiwa na kuwa tajiri ni muhimu kwako pia kujijengea utaratibu wa kuifatilia mipango yako kwa karibu sana. Kama hutoweza kufanya hivyo, itakuwa ni ngumu kufanikiwa kwa sababu mambo yako mengine hayatafanyika kwa uhakika. Jaribu kujiuliza, ikiwa hufuatilii mipango yako nani ataifatilia? Kazi yako inakuwa ni kupanga tu, unaanza, halafu kufuatilia hakuna.

6. Jifunze kutekeleza majukumu yako kwanza.
Ili kufanikiwa ni vyema, kufanya kitu mwenyewe kwanza. Hiyo itakusaidia kukielewa wewe mwenyewe, hata ukitoa jukumu la utekelezaji wake kwa mwingine ni sawa. Acha kutoa majukumu kwa wengine sana na hata kujisahau wewe mwenyewe. Unapotoa majukumu sana kwa wengine kinachokutokea, unakuwa hujifunzi namna ya kutekeleza mambo kwa ufanisi na hata ikitokea kushindwa unakua hujui kwa nini ulishindwa.

7. Fanya utajiri kuwa ni kitu cha lazima.
Katika maisha yako ili uweze kufanikiwa na kuwa tajiri, weka utaratibu wa kufanya utajiri kuwa ni kitu cha lazima na siyo jambo la hiari tu. Kwa kufafanua hili namaanisha kwamba, ni kuelekeza matakwa yako yote, nia yako yote. mwelekeo wako wote, kwenye mtiririko mmoja wa kuelekea kwenye lango kuu la utajiri. Ukiweza kuitumia kanuni hii ndogo katika maisha yako ni lazima ufike ukingoni na kuwa tajiri.

8. Kuwa king’ang’anizi katika maisha yako yote. 
Kitu kitakachokufanya kuwa tajiri katika maisha yako ni kuwa na uwezo wa kupambana na vikwazo mpaka mwisho na sio kukata tamaa na kuacha. Tambua kwamba, katika safari ya mafanikio kukutana na vikwazo ni kitu ambacho hakikwepeki na  vikwazo vyote ni nafasi ya kufanikiwa vilivyo vaa nguo za kazi, kumbuka hilo. Hivyo, zoea jambo hilo na kuwa king’ang’azi bila kuchoka mpaka uufikie utajiri.Utaweza tu kufika kule unakotaka, ikiwa uko tayari kupambana na vikwazo vinavyotekea njiani. 

9. Andaa bajeti maalumu itakayokuongoza.
Kitu ambacho unakihitaji sasa, ili uweze kuelekea vizuri kwenye utajiri ni bajeti. Ni kweli, unahitaji kuwa na bajeti na taarifa nyingi za matumizi na mapato ya fedha zako binafsi na za biashara zako. Ikiwa hutaweza kuweka kumbukumbu za fedha zako, itakuwa ni rahisi kwako kutokujua wakati unapopoteza fedha zako bila sababu hadi hali itakapokuwa mbaya kabisa. Hii ni kanuni bora kwako ambayo unaweza kuanza kuitumia sasa.

10. Simamia maamuzi yako.
Ni lazima ufahamu kwamba siku zote watakuwepo watu wasiokubaliana na jinsi unavyofanya mambo yako, walio na wasiwasi na wanaojaribu kukurudisha chini kwa kila njia. Watu hawa wanaweza kuwa marafiki zako wa karibu wakati mwingine, ama hata ndugu zako. Huwezi kulizuia wala kulibadili hilo, wanayo haki ya kuwa kama walivyo. Katika hili usifanye kosa la kuruhusu mawazo ya watu wengine kuathiri maamuzi yako bila sababu ya maana. Simamia maamuzi yako unayoyaamini mpaka ufanikiwe.

11. Jifunze kutokana na makosa.
Watu waliofanikiwa ni watu wenye tabia ya kujifunza kutokana na makosa waliyoyafanya. Ikiwa kuna kushindwa wanakuwa wanataka kujua ni kwanini walishindwa. Hivyo kama kuna uwezekano wanakuwa wanatafuta njia nyingine mbadala ya kuweza kuepuka hayo makosa na kufanya mambo yao kwa ufanisi zaidi mpaka kuweza kufikia lengo. Hii ni moja kati ya kanuni rahisi ambayo unaweza kuitumia na kufanikiwa sana.

12. Endelea kujifunza zaidi.
Hiki ni kitu muhimu sana kwako leo na katika maisha yako yote. Unatakiwa kuendelea kujifunza kila siku bila kuchoka. Watu waliofanikiwa sana huhudhuria semina, husoma vitabu, magazeti, hujiunga na vikundi na warsha mbalimbali zinazohusika katika maeneo hayo. Pia kuna wakati hutafuta watu wa kuwashauri na hata kuajiri washauri binafsi katika maisha yao ili tu kuhakikisha ni lazima wanafanikiwa,. Hii ni sheria ya msingi sana kwako kuijua na kuitumia ili kuufikia utajiri.

Tunakutakia mafanikio mema, endelea kutembelea DIRA YA MAFANIKIO kujifunza kila siku.

DAIMA TUPO PAMOJA MPAKA MAISHA YAKO YAIMARIKE,

IMANI NGWANGWALU,
0713 048035,
dirayamafanikio@gmail.com

1 comment :

  1. Nashukuru Sana kwa waandishi.mambo mengi nimeweza kujifunza ambayo natakiwa kuyafanya ili kufanikiwa na nitaendelea kufatilia na kuyatendea kazi asanteni Sana.

    ReplyDelete

Note: Only a member of this blog may post a comment.