google-site-verification: googleabbfd1327a3af7a3.html

Badili maisha yako sasa kwa kuwa na fikra sahihi.

Kujifunza zaidi juu ya maisha na mafanikio, nakualika kwenye kundi la whats app kujifunza kwa kina. Tututumie ujumbe kwa njia ya whats app kwenda 0687449428 kupata utaratibu wa kujiunga.

May 14, 2015

Kama Utazingatia Kitu Hiki katika Biashara Yako, Ni Lazima Uwe Tajiri.

No comments :
Mara nyingi huwa tunaona na kushudia kwa wenzetu wakiwa ni watu wa kufanya biashara ambazo kwa macho ya nje huwa zinaonekana ni kubwa na zinawalipa sana. Wengi wetu kwa kutokuja hubaki tukijiuliza maswali ya kutaka kujua nini hasa siri ya mafanikio yao.  Kwa bahati mbaya wengi kwa kutojua huishia kusema wale ni wezi ama ni ma freemason ili mradi tu kujitetea na kutosumbua akili zetu kujua ukweli wa mambo ulivyo.
 
Hivi karibuni nilipata nafasi ya kumtembelea rafiki yangu ambaye kwa kipindi hicho nilisoma naye chuo. Tulipokutana naye katika eneo la Muheza(Tanga) tuliweza kuongea mambo mengi ikiwa pamoja na mambo ya kibiashara. Lakini pia aliweza kunieleza biashara ambayo anafanya katika eneo alipo. Sikutaka kuishia hapo nilimuuliza ni biashara gani? Aliniambia na nilishikwa na mshangao jinsi ambavyo ilikuwa ikimlipa na amepiga hatua.

Bwana huyu kwa kifupi, alikuwa akifanya biashara ya ‘saluni’ ambayo ni ya kawaida kabisa, ninaposema ni ya kawaida nikiwa na maana haijafikia kiwango cha kuwa Barber shop. Kilichonishangaza kwenye ofisi yake ni idadi kubwa ya wateja aliyonayo  kwa siku, ambao niliwaona wakipishana wakihitaji huduma yake na wengine kusubiri kwenye viti vya ziada ili kunyolewa, ingawa mle ndani alikuwa na viti sita vyote vyenye wateja.

Kwa harakaharaka sikutaka tu kuishia kupata mshangao ambao naamini usingenisaidia kitu, bali nilitaka kujua nini siri aliyonayo na inayofanya wateja wengi wamkimbilie yeye na kuacha saluni nyingi ambazo zipo mjini? Nilikuja kugundua kitu muhimu na cha ziada alichokuwa akikifanya tofauti na wengine. Kitu hiki ni huduma bora  aliyokuwa akiitoa na ndicho kitu hata wewe, kama utazingitia kitu hiki katika biashara yako ni lazima ufanikiwe sana.


Kwa muda mchache tu niliokuwa nae niliweza kushuhudia akiwajali wateja hasa anapowakaribisha na kuagana nao, lakini hata pia wasaidizi wake ni watu ambao nyuso zao  zilionekana zenye tabasamu. Na kwa hali hiyo hakuna mteja ambaye angeweza kujisikia vibaya ama kero kwa kupewa huduma kama hiyo. Hicho ndicho kitu ambacho mimi na wewe tunatakiwa tukifanye na kukitilia mkazo zaidi kwenye biashara zetu, ili kufanikiwa kwa viwango vya juu.


 Kwa wengi wetu suala la kuwa na huduma nzuri zaidi inayoendana na mteja wako ni kitu kigumu kidogo. Wengi huwa ni watu wa kufanya biashara zao kwa kujisikia tu. Huwa ni watu wa kutokujali sana ama kusikiliza hasa mteja anataka nini. Kutokana na hili, naweza kusema moja kwa moja hii ndio sababu mojawapo inakufanya ukose wateja zaidi katika biashara yako kuliko unavyodhani.
Kabla hujajilaumu kuwa wateja hakuna ama siku hizi biashara ni ngumu kama ulivyo wimbo wa wengi, jaribu kukaa chini na kukagua kama kweli huduma zako ni bora. Haiwezekani ukawa ni mtu wa kununa, usiyeweza hata kuchangamkia wateja halafu kesho ukategemea uwe una wateja wengi katika biashara yako. Hakuna muujiza kama huo ambao unaweza ukakutokea, vinginevyo uchukue hatua ya kubadilika.

Watu wengi wenye mafanikio makubwa katika biashara zao pia huwa ni watu wa kuboresha sana huduma zao kila mara. Jaribu kuangalia kampuni kubwa  kama vile za simu jinsi zinavyofanya vizuri, bila shaka utathibitisha hili ninalosema. Ukiweza kutoa huduma bora katika biashara yako hiyo ni dalili tosha ya kuweza kufikia mafanikio makubwa katika biashara yako.


Mimi mwenyewe mara nyingi nimekuwa shahidi kwa jambo hili. Kuna wakati huwa ninalazimika kusafiri umbali mrefu wa mji kwenda kona ya pili kwa ajili ya kununua bidhaa ambayo hata ningeweza kuipata tu jirani na ninapoishi. Ninao marafiki ambao mara nyingi hawawezi kula katika hotel yoyote mjini, wanapendelea hotel fulani hata kama iko mbali. Ukija kuangalia yote hiyo inasababishwa na huduma bora wanayopewa.

Kumbuka huduma unayotoa ingawa unaweza ukaona ni kitu kidogo sana katika biashara yako, lakini ndiyo inayoamua ama kukupa wateja wa kiwango gani. Kama huduma yako mbovu sahau kuwa na wateja wengi na hiyo itakusumbua sana kama hutabadilika. Acha kujali ‘pesa, pesa, pesa’ tu, zingatia kwanza huduma yako, mambo ya pesa yatafuata baadae. Wafanye wateja wako wajisikie vizuri kuhudumiwa na wewe kesho na kesho kutwa watakuja tena.

Ieleweke kuwa pia ukiweza kumshawishi mteja mmoja katika biashara yako utakuwa umewapata marafiki zake hata na jirani zake. Hivyo ni muhimu sana kwako na wasaidizi wako ambao mnafanya kazi pamoja kuweza kuijua vizuri lugha ya kibiashara. Kwa kujua lugha hii itasaidia kumvutia mteja kitu ambacho kitakuwa ni faida kwako na maendeleo ya biashara kwa ujumla.

Kwa kumalizia makala hii, tutambue kuwa tunatakiwa kubadilika sisi wenyewe kwanza, hasa katika suala zima la kutoa huduma ili kuweza kufikia mafanikio makubwa. Kinyume cha hapo itakuwa ngumu sana kwetu kuweza kupiga hatua tunazozihitaji katika maisha yetu. Ni vizuri tukajifunza hata kwa wenzetu waliofanikiwa katika hili.
Tunakutakia kila la kheri katika safari yako ya mafanikio, endelea kuwashirikisha wengine kutembelea mtandao huu wa DIRA YA MAFANIKIO kwa ajili ya kujifunza zaidi kila siku.
DAIMA TUPO PAMOJA MPAKA MAISHA YAKO YAIMARIKE,
 
IMANI NGWANGWALU,
0713 048035,

No comments :

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.