google-site-verification: googleabbfd1327a3af7a3.html

Badili maisha yako sasa kwa kuwa na fikra sahihi.

Kujifunza zaidi juu ya maisha na mafanikio, nakualika kwenye kundi la whats app kujifunza kwa kina. Tututumie ujumbe kwa njia ya whats app kwenda 0687449428 kupata utaratibu wa kujiunga.

Oct 27, 2016

Namna Ya Kutambua Shughuli Iliyokuleta Duniani.

No comments :
Watu wengi huwa ni watu wa kujiuliza na kutaka kujua hasa ni shughuli ipi iliyowaleta duniani.  Mara nyingi wengi huwaza ‘ Sasa nitajuaje kwamba, kazi hii ndiyo ambayo imenileta au nimekuja kuifanya hapa duniani’? Ni kweli kila mtu duniani ameletwa au amekuja kwa ajili ya shughuli ama kazi maalumu kwake ambayo ni lazima aitimize ili kuweza kufanikiwa kwa viwango vya juu zaidi.
Tatizo kubwa linalooonekana kwa wengi wetu ni kutokujua hasa shughuli iliyotuleta hapa duniani. Kwa kutokujua huko hupelekea wengi kuvamia kazi ambazo sio zao na matokeo yake kushusha kiwango cha ufanisi. Kama unataka kufikia kiwango kikubwa cha mafanikio ni muhimu kujua shughuli iliyokuleta duniani. Swali la kujiuliza hapa utajuaje hasa shughuli iliyokuleta hapa duniani?
 1.Tambua ni kipi kimeikalia akili yako sana.
Hatua ya awali itakayokuwezesha kujua shughuli au kazi uifanyayo ndiyo hasa unayotakiwa kuifanya, ambayo ndiyo itakayokupa ridhiko la moyo na mafanikio, ni kuangalia kiwango chako cha kuipenda na kuridhika nayo. Lakini pengine pia ni kupima au kujiuliza juu ya shughuli au kazi ambayo inaingia akilini mwako mara kwa mara. 

Siyo kuingia akilini kwa kufikiria kipato, hapana, bali kuingia akilini ukitamani kuifanya. Wakati mwingine hata kuona kama vile wale wanoifanya shughuli hiyo inayoitawala sana akili yako wamependelewa au kupata bahati. Shughuli hii inayotawala akili yako kwa muda mrefu, mara nyingi  huwa ndiyo shughuli iliyokuleta duniani.


Watu wanaofanya shughuli zilizowaleta duniani huwa wana mafanikio mkubwa sana, hata kama shughuli hizo zinaonekana ni za watu duni, wasio na kipato wala heshima katika jamii, lakini huweza kustawi kimapato na kuweza kuishi kwa utulivu wa nafsi. Mtu anapofanya kile ambacho ndicho kilichomleta duniani, kufanikiwa kwake ni lazima.

2. Tambua ‘hobi’ yako ni ipi.
Kuna wakati shughuli zilizotuleta hapa duniani ni yale mambo ambayo sisi huwa tuyachukulia kirahisi na kuyafanya kwa urahisi kwa sababu ya kujifurahisha. Utafiti mwingi kuhusiana na malengo yetu maishani, unaonyesha kuwa, yale mambo tunayoyaita ‘hobi’ zinaweza zisiwe ‘hobi’ bali ndiyo shughuli zetu za kutupa mafanikio ya kweli maishani.

Kwa mfano unaweza ukaona mtu ana kipaji kikubwa sana cha kuchora na akawa anakitumia katika kujifurahisha tu, mwenyewe anaita ‘hobi’ wakati ukweli ni kwamba, angeamua kuingia kwenye uchoraji kama shughuli kamili, angefanikiwa sana. Wakati mwingine hata zile tunazoziona kama ‘hobi’ zisizo na maana sana, wengine ni shughuli maalumu kwao na kubwa.

Kama unayo shughuli au jambo ambalo unalipenda sana na unalifanya kama ‘hobi’, jaribu kulikagua. Inawezekana kabisa isiwe ‘hobi’ kama unavyofikiri bali ndilo limefanya ukaletwa hapa duniani. Kumbuka hakuna shughuli ndogo, ya kijinga au haina faida, bali inategemea wewe unayeifanya unaifanya kwa sababu gani?

3. Kama haina umuhimu wa nje.
Kama mtu anaipenda shughuli ambayo ni wazi haijulikani wala kufahamika kwa nje nap engine hata iikfahamika ni kwa kudharauliwa sana nab ado mtu huyo akajivunia kuifanya shughuli hiyo, hii ni dalili nzuri ya mtu kuwa kwenye shughuli iliyomleta hapa duniani.

Kuna watu ambao huficha shughuli zao, hawataki wengine wakajua wanafanya shughuli gani. Huficha kwa sababu wanahisi aibu kwa kuamini kwamba hizo shughuli zao ni zenye pengine kudhalilisha. Hawaoni kama wanastahili kuzifanya, kwani kwao hizo ni shughuli za watu wa aina Fulani wa kiwango cha chini.

Mtu anapogundua kuwa, anahisi aibu kutaja shughuli yake kwa sababu anadhani ni shughuli duni, ni vizuri akaacha kufanya shughuli hiyo, kwani anapoteza muda wake wa bure. Kudhani shughuli mtu aifanyayo ni dhalilisho, ni dalili kubwa ya kwamba mtu huyoanafanya shughuli ambayo hakutakiwa kuigusa maishani mwake.

4. Kutambua matatizo siyo hoja.
Kama kweli shughuli ambayo unaifanya ndiyo imekuleta hapa duniani,ndiyo shughuli ambayo unatakiwa kuifanya, haeiwezi kuwa na matatizo. Siyo kwamba ukifanya shughuli hiyo, huwezi au shughuli yenyewe haiwezi kukumbwa na vikwazo, hapana. Bali yanapotokea matatizo hutakata tamaa na kusema ‘basi’. Badala yake matatizo hayo yatakusukuma kusonga mbele na kukusaidia kujikita zaidi kwenye shughuli hiyo.

Bila shaka umeshawahi kuona au kusikia juu ya watu ambao shughuli fulani wazifanyazo zinakumbwa na matatizo, wengine wote wakajitoa, lakini wao wakabaki peke yao na kuendelea nazo, kama kwamba hayo matatizo ndiyo waliokuwa wanayasubiri. Biashara inakumbwa na matatizo ya aina fulani ambapo kuendelea kwake ni kwa kubahatisha sana na wengi wazifunga biashara zao, lakini mwingine anaendelea kama vile hakijatokea kitu. Kazini na mahali pengine hali kama hiyo huweza kujitokeza pia.

Kama kweli shughuli unayoifanya ni yako kabisa haiwezi kutokea hata mara moja ukaiacha kwa sababu ya matatizo. Hata kama utaiacha ni kwa muda tu, kwani utajikuta unatafuta njia au mbinu ya kupata ufumbuzi wa matatizo hayo. Matatizo hayawezi kukukatisha tamaa kama ambavyo yanaweza kumkatisha tamaa mtu ambaye anaifanya shughuli hiyo kwa sababu za nje, ikiwemo kipato. Huyu anayeifanya kwa sababu ya kipato, umaarufu au madaraka na sababu nyingine, ndiye ambaye tatizo likitokea ni mwepesi kughairi na kubadili shughuli.

5. Kuwa na ridhiko la ubunifu au ugunduzi.
Kama kweli shughuli unayoifanya ndiyo ambayo ‘umeandikiwa’ kuifanya, utajikuta mara nyingi unakuwa mtundu nayo na kuvumbua au kugundua mambo mapya. Hata kama mambo hayo mapya hayakupi faida inayogusika au ya moja kwa moja kama ya kipato, bado uvumbuzi au ugunduzi huo utakufanya kuridhika zaidi kuliko yule ambaye angepata pesa na kufurahia kuridhika tu kwa sababu ya pesa.

Wengi wanapobuni au kuvumbua vitu kwenye shughuli zao hukata tamaa, kuvunjwa moyo, kuvunjwa nguvu na pengine kubadilisha shughuli zao hasa wanapoona kwamba hakuna mtu aliyeonyesha kutambua ugunduzi wao na pengine kuwapa zawadi au fedha. Ukiwa hivyo jua kabisa unafanya shughuli ambayo siyo yako na ambayo haijakuleta duniani.

Kugundua na kuvumbua kinachozungumzwa hapa kunaweza kuonekana kuwahusu watu wachache, wasomi au wenye taaluma maalumu, hapana. Mtu yoyote, katika shughuli yoyote anaweza kugundua au kuvumbua jambo jipya na la manufaa kwa shughuli yake, kwake mwenyewe na kwa wengine pia.

6. Nguvu ya wito.
Kuna wakati huwa tunajiuliza ni kwa nini baadhi ya watu ambao wanauwezo mkubwa  wa kubadili shughuli, bado wanang’ang’ania shughuli ambazo zinaonekana kuwa hazina hata matumaini kidogo ya baadaye? Kwa hapa ilifika mahali Fulani ambapo ualimu ulionekana kama vile kuufanya ni kujitafutia umaskini na balaa kubwa kimaisha.

Lakini ni jambo linaloweza kuonekana kama la kushangaa kugundua kuwa, kuna baadhi ya watu ambao wangeweza kufanya shughuli nyingine na kufanikiwa sana kimapato, lakini wameamua kuwa walimu kwa furaha kubwa, wewe mwenyewe ni shahidi umeshawahi kukutana na watu wa namna hiyo.

Hapa ndipo ambapo tunasema, mtu anafanya shughuli fulani kwa sababu ya wito, siyo kwa sababu ya kitu kingine. Mtu anajua wazi kwamba, shughuli aifanyayo inadharauliwa nap engine haina maslahi ya fedha, lakini yeye anajisikia vizuri, anaona fahari na anafurahia kuifanya. Wito maana yake ni mtu kufanya kile ambacho ndicho alichotakiwa kuja kukifanya hapa duniani, ambacho kwa hali hiyo kimemkaa moyoni na akilini.

Kumbuka, hakuna aliyekuja hapa duniani kufanya tu shughuli ambayo haimhusu, kila mtu ameletwa na shughuli yake. Kaa chini tafakari na utafute shughuli iliyokuleta hapa duniani itakupa mafanikio makubwa sana.

Ni wako rafiki,

IMANI NGWANGWALU,
0713 048035,

No comments :

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.