google-site-verification: googleabbfd1327a3af7a3.html

Badili maisha yako sasa kwa kuwa na fikra sahihi.

Kujifunza zaidi juu ya maisha na mafanikio, nakualika kwenye kundi la whats app kujifunza kwa kina. Tututumie ujumbe kwa njia ya whats app kwenda 0687449428 kupata utaratibu wa kujiunga.

Apr 30, 2017

Je, Bado Unalalamika Kwenye Biashara Yako?

No comments :
Mbona unalalamika kila siku kwamba biashara yako ni ngumu? Kwani wewe ulianzisha biashara yako kwa lengo gani? Malalamiko kutoka kwa wajasiriamali imekuwa ni sehemu ya Maisha yao.
 Kila unapojaribu kuongea na wajasiriamali lazima usikie malalamiko mengi ikiwemo ukosefu wa mitaji ya kuendesha biashara. Watu wanalalamika eti hawafikiriwi, hakuna anayewajali na hawasaidiwi!
 Yawezekana ni kweli, lakini kwa yeyote mwenye malalamiko na aketi chini na ajiulize hili; “Ndiyo hakuna anayenijali, hakuna anayenifikiria na hakuna anayenisaidia, kwahiyo…...” 
Ukishajiuliza swali la “kwahiyo…” –bila shaka utaamua mojawapo kati ya haya: ama ni kuacha kufanya biashara au kuendelea na biashara”. Endapo utaamua kuacha biashara kero na malalamiko yako yote vitakuwa vimeishia hapo na kimsingi utaweza kuendelea na maisha mengine. 

Endapo utachagua kuendelea na biashara, maana yake ni kwamba matatizo unayolalamikia si makubwa kiasi cha kukuzuia kupata faida na pengine ndiyo maana umechagua kuendelea na biashara bila kujali matatizo na changamoto zilizopo.
Utamaduni wa kulalamika juu ya kazi tunazozifanya tumeurithi kutoka kwa watumishi hasa waajiriwa. Mfumo wa ajira duniani uko katika umbo la pembe tatu (piramidi). Ambapo unakuta mkubwa ni mmoja na chini yake kunakuwa na watu wengi kutegemea na ukubwa wa taasisi au kampuni husika iliyokuajiri. Mara nyingi watu walioko chini wakishindwa jambo lolote humsukumia yule aliyejuu ili afikiri na kutoa suruhisho kwaniaba ya wale wote anaowaongoza.

Kwa maana nyingine ni kwamba katika umbo hilo hapa juu, kuna mambo mengine huruhusiwi kuyafanya au kuyatolea maamuzi isipokuwa aliye juu yako. Pili, ukiwa mwajiriwa wa ngazi za chini kuna mambo ambayo yakikushinda unayapeleka kwa mkubwa wako kwa ajili ya ufumbuzi zaidi.

Kwahiyo, chimbuko la tabia ya kulalamika ni utaratibu wa kutegemea maamuzi ya aliye juu yako. Kama anayepaswa kuamua jambo fulani, hafanyi hivyo kwa wakati au akafanya maamuzi vibaya basi utakuta waajiriwa walioko chini wanafanyakazi kwa kunung’unika muda wote, wanalalamika muda wote wanasema hovyo muda wote na hasa wakiwa maeneo ya nje ya ofisi zao.

Ikumbukwe kuwa, kinachowapa waajiriwa uhalali wa kulalamika ni ule mfumo au utaratibu wa ajira duniani ambao unatoa nafasi kwa mwajiriwa kuweza kupeleka malalamiko yake ngazi za juu endapo ataona kuna mambo ambayo hayaendi sawa.

Katika mfumo mzima wa ajira “MKUU” ni mtu wa mwisho na hatutarajii halalamike kwasababu hakuna mtu mwingine aliye juu yake ambaye anatakiwa kumpelekea malalamiko, ingawaje wengine ujikuta nao wakilalamika kwa watu wa chini yao. Wewe kama ni “Mkuu” kazi yako ni kuamua na kutenda basi!

Unapoamua kuwa mjasiriamali au kuanzisha biashara ni kwamba wewe umejipa nafasi ya kuwa “MKUU”. Haijalishi biashara ni ndogo au ni kubwa kiasi gani bali wewe ni mkuu tu! Wewe ni kiongozi mkuu wa biashara unayoifanya, na pia wewe ni kiongozi mkuu wa maisha yako. 
Mafanikio ya biashara au mradi wako yanategemea sana maamuzi na kutenda. Kamwe tusiwaige waajiriwa, kwani wao wanayo sehemu ya kupeleka malalamiko—kwa viongozi wao au kwa wakuu wao katika utumishi. 
Sisi wajasiriamali ni tofauti na waajiriwa kwasababu hatufungwi na kitu chochote katika kuamua nini tufanye na nini tusifanye, ilimradi tu tunafuata sheria za nchi. 
Wajasiriamali tunao uhuru wa kurekebisha kile kinachotukera na kama ni kikubwa kiasi cha kutuletea hasara bado tunayo maamuzi ya kufunga biashara hiyo na tukaendelea na maisha mengine yanayotupa faraja.
Haipendezi hata kidogo mjasiriamali kulialia kila wakati. Wengi kilio chao ni kusaidiwa mtaji, kuonewa huruma, kubembelezwa n.k. sijui! lakini nionavyo mimi, hakuna atakayekufunga endapo utaamua kuacha ujasiriamali, badala yake wewe ndiye utapata hasara ukiacha au faida ukiendelea kufanya vizuri hicho unachofanya.
Eti unataka uwezeshwe na mtu ambaye shughuli zake tu zinategemea zaidi pesa unazomchangia kila mara, je hiyo inawezekanaje mtu huyo huyo akuwezeshe pesa?
Ndugu yangu umefika wakati sasa ujitambue na uache kulalamika kama waajiriwa. Kaa kimya huku ukizidi kufanya kazi zako zote kwa juhudi na maarifa. Pia, tekeleza majukumu yako kadiri ya uwezo wako wote. Jione kuwa wewe ni kiongozi mkuu na hakuna mtu mwingine mbele yako na hata juu yako.
Kuwa tayari kuwajibika kwa maamuzi na matendo yako unayofanya kila siku. Kila unapokabiliwa na changamoto usikimbilie kulia na kulalamika, usikimbilie kuacha bali ujiulize ni kwanini ulianzisha hiyo biashara unayofanya.
Pia, fikiria ni watu wangapi watafurahia kuona wewe unashindwa kufanikisha hicho unachokifanya. Ukitambua hili, nina hakika kuwa muda si mrefu utaanza kuona mafanikio yakianza kupatikana.
Endelea kujifunza kupitia hapa DIRA YA MAFANIKIO ili upate kufahamu mbinu za kujiongoza na siyo kulalamika kama waajiriwa.
MAKALA HII IMEANDIKWA NA CYPRIDION MUSHONGI WA MAARIFA SHOP BLOG.

No comments :

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.