google-site-verification: googleabbfd1327a3af7a3.html

Badili maisha yako sasa kwa kuwa na fikra sahihi.

Kujifunza zaidi juu ya maisha na mafanikio, nakualika kwenye kundi la whats app kujifunza kwa kina. Tututumie ujumbe kwa njia ya whats app kwenda 0687449428 kupata utaratibu wa kujiunga.

Sep 21, 2015

Siri Nzito Katika Kufikia Mafanikio Makubwa.

No comments :
Katika maisha kila mtu hupenda kufanikiwa na kufikia mafanikio makubwa. Lakini pamoja na umuhimu huo ni wapo ambao hujikuta wakifanya yale yasiyotakiwa kufanywa ili kufikia mafanikio hayo. Mafanikio mazuri ni lazima yaanze na malengo. Bila kujiwekea malengo yatakayokuongoza kwenye mafanikio inakuwa ni kama kazi bure.
Katika mfano mzuri wakukueleza hili na ukanielewa vizuri ningependa leo nikusimulie kisa kimoja cha ndege Tai. Ndege huyu ni moja kati ya ndege aliyefanikiwa kuwa na uwezo mkubwa wa kuruka juu zaidi kuliko ndege wengine wote.  Siku moja mfugaji mmoja katika pitipita zake alibahatika kupata yai la Tai.  Alipofika nyumbani aliamua kuliweka yai lile kwenye mayai ya kuku ili litotolewe.
Ulipita muda wa siku ishirini na moja malengo ya mkulima yule yaliweza kufanikiwa pale yai lile lilipototolewa pamoja na mayai mengine ya kuku. Siku zote utambulisho wa kitu au mtu ni jamii aishiyo. Kuku wale pamoja na tai yule waliweza kuishi pamoja na hata kujita wote wana tabia za aina moja zinazofanana.
Siku moja sasa kuku alikuwa akitafuta chakula kwa ajili ya vifaranga wake.  Tai yule ambaye alikuwa  pamoja na kuku alimuona tai mkubwa akiwa angani na akamuuliza kuku yule ni ndege gani mbona yuko juu sana kuliko sisi? Kuku alimjibu na kusema yule ni tai ndege aliyebarikiwa sana kuliko ndege mwingine.
Tai mdogo hakushia hapo aliendelea kumhoji kuku kwa hiyo sisi hatuwezi kuruka na kuwa kama yeye?  Kuku alimjibu ni kweli hatuwezi sisi ni kuku hatuna uwezo huo. Kwa kuwa tai mdogo alishindwa kujitambua yeye ni nani aliweza kukata tamaa na kuamini kabisa ni kweli hawezi kufanana naye.

Tai yule aliendelea kuishi maisha yaleyale akiwa na kuku hadi siku ya mwisho alijikuta akiwa amekufa bila kutimiza malengo yake. Kitu kikubwa kilichomfanya hadi afe na hali hiyo ya kutokuweza kuruka ni kutokana na yeye kuamini asingeweza kuleta mabadiliko ya kuruka kumbe uwezo huo alikuwa nao tena mkubwa wa kufanya hivyo ingawa yeye hakujua.
Ni mambo gani ya kuweza kujifunza kupitia simulizi hii?
1. Kama unataka kufanya mambo makubwa katika maisha yako, jifunze kuamini fikra zako na kuwa wewe kama wewe. Ukisikiliza sauti nyingi za nje zitakuzuia kufika kule unakotaka kufika. Kwa mfano kama tai yule mdogo angejiamini angeweza kuruka lakini kwa bahati mbaya alikufa huku na uwezo wote akiwa nao. Kilichomkwamisha ni sauti ya kuku. Angalia hata hapo ulipo usije ukakwamishwa na kuku, wewe ni tai.
2. Kila wakati ni lazima kujiandaa na kujifunza kwa ajili ya mafanikio yako. Kama usipojiandaa na kujifunza utakufa na mambo mengi bila ya kuyatumia.
3. Upo umuhimu wa kuachana na mambo ya zamani yanayotushikilia na kutukwamisha. Acha kuaminishwa tena na mtu eti kuwa huwezi wakati uwezo huo unao tena mkubwa sana.
4. Watu wengi wanajikuta wakifa na kwenda makuburini bila kutimiza malengo yao makubwa waliyojiwekea kutokana na kutokuelewa uwezo ulio ndani mwao. Wapo waliokufa wakiwa na vipaji vikubwa vya mziki ndani yao, wengine walikufa wakiwa na vipaji vya mpira na wengine hata vya uandishi lakini kwa bahati mbaya hawakuweza kuvitumia vyote hivyo, kama tu ilivyokuwa kwa tai.
5. Tulizaliwe ili tushinde katika maisha na siyo tushindwe. Acha kujiona mnyonge katika dunia hii, kumbuka wewe ni mshindi na siyo mtu wa kushuindwa kama unavyojiona.
Yapo mengi ya kujifunza kupitia simulizi hiyo, lakini nimekushirikisha kwa sehemu ili kujifunza pamoja. Tafakari juu ya maisha yako na chukua hatua kubwa ya kutumia vipaji ulivyonavyo ndani mwako na kukufanikisha.
Nakutakia kila la kheri katika safari ya mafanikio yako na endelea kutembelea DIRA YA MAFANIKIO kujifunza na kuhamasika.
DAIMA TUPO PAMOJA MPAKA MAISHA YAKO YAIMARIKE,
Ni wako rafiki katika mafanikio,
Imani Ngwangwalu,
Kama una maoni, ushauri au changamoto yoyote inayokuzuia kufikia mafanikio yako wasiliana nami kwa email dirayamafanikio@gmail.com au simu 0713 048035 kwa ushauri na msaada wa haraka.  







No comments :

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.