google-site-verification: googleabbfd1327a3af7a3.html

Badili maisha yako sasa kwa kuwa na fikra sahihi.

Kujifunza zaidi juu ya maisha na mafanikio, nakualika kwenye kundi la whats app kujifunza kwa kina. Tututumie ujumbe kwa njia ya whats app kwenda 0687449428 kupata utaratibu wa kujiunga.

Sep 10, 2015

Siri Kubwa Iliyofichika Katika Mafanikio Ni Hii Hapa.

No comments :
Ninakumbuka ni miaka mingi sasa imepita wakati nikiwa darasa la tatu nilikuwa nikisumbuana sana na wazazi wangu kwa sababu ya shule. Kilikuwa ni kipindi ambacho nilitokea kuichukia shule na nilikuwa nipo tayari kwa lolote kuacha shule. Kwa kipindi hicho kwangu shule ilikuwa siyo sehemu ya kujifunza kama watoto wenzangu walivyoifurahia, kwangu ilikuwa ni mateso.
Karibu kila siku nilikuwa niliamshwa kwamba muda wa shule umefika. Na hata kama ikitokea kweli siku hiyo nilienda ilikuwa ni kwa kujikongoja sana. Sababu hasa zilizonifanya nichukie shule kwa wakati ule zilikuwa ni nyingi, lakini chache nilizokuwa nazo ni pamoja na baridi iliyokuwepo hasa nyakati za asubuhi, pia utamu wa usingizi na hiyo haitoshi nilikuwa nimechoshwa na umbali wa mahala shule ilipo. Zilikuwa ni sababu za kitoto kweli ingawa kwangu wakati ule zilikuwa za maana sana.
Nimekuwekea mfano huo sio kukufurahisha tu, bali kuna kitu ambacho ninataka tujifunze pamoja kutokana na maisha yetu ya kila siku. Mara nyingi wengi wetu huwa hatupo tayari kuvumilia mpaka mwisho kuelekea kwenye ndoto zetu. Wengi tunajikuta tunakuwa tuna sababu nyingi za kitoto kama nilizokuwa nazo mimi ambazo moja kwa moja zinatuzuia kwenye mafanikio.
Jaribu kujiuliza, ni mara ngapi umekuwa mtu wa visingizio na kuacha ndoto zako zikiyeyuka kutokana na sababu nyingi zisizo na maana ambazo umekuwa ukizishikilia? Ni mara ngapi ambapo umekuwa ukikosa hamasa na uvumilivu kwa kile unachokifanya na kuachia ndoto zako zikipita kirahisi eti kwa sababu ndogo tu kuwa huwezi hiki ama kile? Bila shaka umekuwa na sababu kama hizi  nyingi tu, tena zisizo na msaada kwako.

Ni kweli miongoni mwetu wapo watu ambao ni rahisi kujisikia na hatimaye kuamua kutokufanya mambo fulani kama nilivyokuwa mimi kutokana na sababu ndogondogo. Hawa ni watu wa kutokujisikia kufanya kitu hata kama kina manufaa na faida kwao kubwa. Kufanya kwao kunategemea sana na kujisikia. Kwa mfano leo hii kama ameamka amechoka basi, kazi nyingi zitalala ama hataweza kwenda kazini kabisa  kwa kisingizio hiki na kile. Kama ni kweli umeamua kufanya hivyo, hiyo yote ni sawa kwako kwa sababu maisha ni yako na kama ni mafanikio ni yako pia.
Unaweza ukawa unaona uvivu kufanya jambo fulani au ukahisi huwezi kabisa, lakini kitu peke unachotakiwa kufanya ili ufanikiwe ni kulianza jambo hilo au kitu hicho haijalishi unajisikiaje au unawaza nini kwenye kwenye kichwa chako. Mafanikio yote unayoyataka huwa yanaanza kwa kuanza, hapo ndipo ilipo siri ya wewe kuweza kusongambele. hakuna mafanikio yanayoanza kwa sababu hata siku moja, jaribu kuchunguza hilo utagundua uhalisia wake.
Inawezekana ukawa upo kwenye maisha magumu, huna mtaji na unaona kabisa haiwezekani kufanya kitu, lakini uwezo wa kubadilisha maisha yako unao kwa kuanza hivyohivyo. Acha kufanya kosa la kusubiri mambo yako yote yawe sawa ndiyo uanze utakuwa tayari umechelewa. Huna haja tena ya kusubiri kitu anza kutekeleza ndoto zako mara moja.
Kila mtu anauwezo mkubwa wa kufanikiwa na kufika kule anakotaka kufika ikiwa atatambua umuhimu wa kuanzia pale alipo. Kama umeamua kuanzisha mradi fulani, usiwaze sana kuanzisha mradi wa mamilioni mengi anza na kile kidogo ulichonacho na kisha ondoa sababu zako ulizonazo hata kama ni nzuri vipi.
Jenga tabia ya kuthamini kile unachokifanya na kisha ukifanye kwa nguvu zote bila kujali ni kidogo kiasi gani kifanye kwa ubora wa juu zaidi. Mafanikio yako utaanza kuyaona kwa kadri utakavyozidi kufanya. Hiyo kumbuka mafanikio yako yatakuja tu, hata kama unachofanya ni kidogo vipi. Kitu cha msingi kithamini na anzia hapo hapo, acha visingizio, wajibika na maisha yako na hapo utakuwa umegusa siri kubwa ya mafanikio yako.
Kwa makala nyingine nzuri zaidi endelea kutembelea DIRA YA MAFANIKIO kwa kujifunza kila siku na kuboresha maisha yako. Pia usiache kuwashirikisha wengine kuweza kujifunza kupitia mtandao huu.
Ni wako rafiki katika mafanikio,
IMANI NGWANGWALU,
0713 048 035,






No comments :

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.